Jumanne, 28 Machi 2017

MAHAKAMA YASHAURIWA KUWAJENGEA UWEZO WATUMISHI WAKE WA NGAZI ZOTE



 
 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tanga Mhe. Imani Abood akielezea utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Miaka Mitano wa Mahakama ya Tanzania katika Kanda ya Tanga leo ofisini kwake jijini Tanga.



Na Lydia Churi-Mahakama, Tanga
Mahakama ya Tanzania imeshauriwa kuwa na Mpango endelevu wa kuwajengea uwezo watumishi wake wa ngazi zote ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Tanga Mhe. Imani Abood alitoa ushauri huo leo jjini Tanga alipokuwa akielezea utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Miaka Mitano wa Mahakama ya Tanzania katika Kanda yake.

Alisema pamoja na kuwa Mahakama inaendesha mafunzo mbalimbali kwa watumishi wake lakini mafunzo hayo hayana budi kutolewa kwa watumishi wote kuanzia ngazi ya chini mpaka ngazi ya juu kabisa katika Mahakama.

Akizungumzia nguzo ya pili ya Mpango Mkakati wa Mahakamainayohusu upatikanaji wa haki kwa wakati, Mhe. Abood alisema ni muhimu suala la mafunzo likapewa kipaumbele hasa kutokana na kukua kwa sayansi na Teknolojia.

Alisema , hivi sasa katika Mahakama  upo ushahidi wa kielekitroniki unaotolewa hivyo ni muhimu mafunzo yakatolewa ili kuleta ufanisi katika suala zima la utoaji wa haki.

Akizungumzia mikakati iliyowekwa na kanda yake ili kuondosha mashauri mahakamani kwa wakati, Jaji Abood alisema wanakusudia kuziwekea umeme Mahakama za Mwanzo kupitia Wakala wa Umeme Vijijini (REA) na kuwapatia Mahakimu wote katika kanda yake vitendea kazi kama vile laptops na printer ili ziwarahisishie kutoa hukumu kwa wakati.

Alisema hivi sasa Mahakimu katika Mahakama za Mwanzo hulazimika kupeleka hukumu walizoandika kwa mkono ili zikachapishwe kwenye Mahakama za wilaya ambapo kuna umeme.

Alisema licha ya changamoto hizo, bado watumishi wa Mahakama Kuu kanda ya Tanga wanakuwa wakifanya kazi kwa bidii na Mahakimu kuhakikisha hukumu zinatolewa kwa wakati ikiwa ni pamoja na na wananchi kupatiwa nakala za hukumu ndani ya siku 21 zilizopangwa.

 Mkakati mwingine uliowekwa ili kuondosha mashauri mahakamani ni pamoja na, kufanya vikao na Mahakimu wafawidhi wa wilaya pamoja na wadau wa Mahakama ili kurahisisha kazi kwa kuwa kila mdau anaposhughulikia eneo lake shauri huisha mapema.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni