Jumatatu, 1 Julai 2024

MAHAKAMA KUU MASJALA KUU YAPATA NAIBU MSAJILI MWANDAMIZI MPYA

Na INNOCENT KANSHA-Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani ametoa rai kwa Maafisa Mahakama kufanya kazi kwa kuzingatia weledi, uadilifu na kujituma kwa bidii wanapohakikisha wanatimiza majukumu yao kwa nafasi wanazozitumikia.

Akizungumza katika hafla fupi ya kumwapisha Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sundi Fimbo. Hafla iliyofanyika Mahakama Kuu Masjala Kuu jijini Dar es Salaam, leo tarehe Mosi Julai, 2024. Mhe. Siyani amesema kuwa, uteuzi huo umezingatia historia ya utendaji kazi wake na Mahakama ina imani na uwezo wake wa kutenda kazi kwa nafasi aliyopewa.

“Uteuzi huu ulizingatia historia ya utendaji kazi wake, nafasi hii ya kuwa Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania ina majukumu mengi zaidi kuliko yale ambayo Mhe. Fimbo amekuwa akiyafanya akiwa Kanda ya Dar es salaam na Divisheni nyingine alizopita kabla ya hapa,” amesema Jaji Kiongozi.

Mhe. Siyani amesema kuwa, ni nafasi ambayo inahusisha zaidi kupanga mipango mbalimbali ambayo itasaidia Mahakama Kuu na Mahakama zingine zote zilizopo chini yake kupiga hatua, siyo kupiga hatua kurudi nyuma ni kupiga hatua kwa kwenda mbele.

“Nitumie fursa hii kuwakumbusha Maafisa Mahakama wote kwamba, uteuzi uliofanyika na teuzi zingine zote zitakazokuja baada ya huu, hazitazingatia mtu ana umri gani wa kufanya kazi mahakamani.Teuzi zitatazama sana mchango ambao mtu huyo anaweza kuutoa kwa Mahakama, zitazingatia ni kwa namna gani mtu huyo anaweza kutuunganisha na kutufanya tusonge mbele,” amesema Jaji Kiongozi.

Aidha, Mhe. Siyani ameongeza kuwa, zama za kutazama umri wa mtu aliokaa mahakamani ili kumfikiria kwa nafasi nyingine ni zama zilizopitwa na wakati na amewataka Maafisa Mahakama na wasio Maafisa Mahakama walielewe jambo hilo ikiwa ni ujumbe mahususi kwa kila mtumishi.

Jaji Kiongozi amewataka watumishi wa Mahakama wanaofanya kazi katika maeneo mbalimbali nchini kutofanya kazi kwa mazoea. Macho ya viongozi yanaweza kuwa yanawaona watumishi huo lakini hayawasomi, watumishi wanapaswa kufanya kazi kwa weledi na ufanisi mkubwa na kwa kupitia njia hiyo ndiyo pekee itakayosaidia mtumishi kuonekana, amesisitiza Jaji Kiongozi

Jaji Kiongozi ametoa ushauri kwa Naibu Msajili Mwandamiazi huyo, kwa kumweleza kuwa, wakati wa kutimiza majukumu yake miongoni mwa mambo mengi ni lazima kuzingatia vipaumbele na kipaumbele kimoja kikubwa ni kuhakikisha Mahakama hairudi nyuma kwenye mambo yote ya msingi ya matumizi ya Teknolojia ya Hababri na Mawasiliano (TEHAMA).

“Ukilala ukiamuka, ukiota ndoto, ukiweweseka muda wote fikiri na utambue ni namna gani tutafika kwenye safari tuliyokwisha kuianza ya kuhakikisha huduma za haki tunazozitoa zinatolewa kwa utaratibu tofauti na ule ambao tumekuwa nao hususani kupitia matumizi ya TEHAMA,” amesisitiza Jaji Kiongozi.

Jaji Kiongozi ameongeza kuwa, Mhe. Fimbo atapaswa kushirikiana na Viongozi wengine na hususani Kurugenzi ya Usimamizi wa Mashauri kuhakikisha Mpango Kazi wa Uendeshaji Mashauri na shughuli nyingine za Mahakama zinaimarika (The Court Busness Process)

Akimwagia sifa za kiutendaji Naibu Msajili Mwandamizi mpya huyo, Jaji Kiongozi amesema kuwa, “nafahamu umekuwa kinara na kiongozi mahiri katika utendaji kazi ukiwa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es salaam, umefanya kazi vizuri sana na kujitoa kwako ndiyo kumefanya wengine wakuone...

Usibweteke, sasa ndiyo wakati wa kuonesha kwamba nilikuwa natumikia eneo dogo la kitaasisi sasa naweza kufanya zaidi. kajikite katika kutekeleza majukumu yako kwa kushirikiana na wenzako utakao wakuta katika kutekeleza majukumu hayo na wote watakusaidia. Usimbague mtu yoyote ushirikiano ndiyo chachu ya mafanikio,”ameongeza Mhe. Siyani

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Salma Maghimbi amempongeza Mhe. Sundi Fimbo kwa kuteuliwa katikati ya watu wengi wenye sifa za kushika nafasi ya Naibu Msajili Mwandamizi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu.

“Mimi niliyekuwa nafanya naye kazi naona uteuzi huu ni sahihi kabisa kutokana na uwezo wake wa kusimamia na kuratibu shughuli zote za uendeshaji wa Mashauri Mahakama Kuu Kanda na Mahakama zote zilizopo chini ya Kanda yetu ya Dar es salaam, hata kama angepatikana kwa kupiga kura ningepiga kura mara nyingi iwezekanavyo ili apatikane yeye,” amesema Mhe. Maghimbi.

Mhe. Maghimbi akawakumbusha Maafisa Mahakama wote kufanya kazi kwa bidii kwa sababu mtu anapofanya kazi juhudi zake zile anazozifanya zinakuwa zinaonekana na hazijifichi. Kwa sasa Mpango Kazi wa Mahakama upo katika kipindi cha mpito kutoka kwenye karatasi ngumu kwenye kidijiti.

Kitu cha muhimu kuliko vyote ni kupokea hayo mageuzi na kuyakumbatia kwa kuyafanyia kazi ili yawe sehemu ya maisha kazini, Maafisa Mahakama wote tukiweza kufanya hilo basi tutaweza kufanya kazi kwa urahisi zaidi.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (kulia) akimwapisha Mhe. Sundi Fimbo (aliyeshika Biblia) kuwa Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Hafla hiyo iliyofanyika Mahakama Kuu Masjala Kuu jijini Dar es Salaam, leo tarehe Mosi Julai, 2024.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (aliyekaa mbele) akitoa neno mara baada ya uapisho huo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani akizungumza na viongozi waandamizi mbalimbali wa Mahakama (hawapo pichani) waliohudhuria hafla hiyo ya uapisho ofisini kwake jijini Dar es salaam mara baada ya uapisho.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Salma Maghimbi akitoa neno wakati wa hafla ya uapisho.


Sehemu ya Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania waliohudhuria katika hafla fupi ya kumwapisha Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu Mhe. Sundi Fimbo (wa kwanza kulia).

Sehemu ya Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania waliohudhuria katika hafla fupi ya kumwapisha Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu Mhe. Sundi Fimbo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (wa pili kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na wananchama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) mara baada ya hafla hiyo ya uapisho.



Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Naibu Wasajili mara baada ya hafla fupi ya uapisho wa Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu Masjala Kuu Mhe. Sundi Fimbo (wa tatu kushoto waliosimama). Wengine Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Salma Maghimbi (wa kwanza kulia walioketi) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (wa kwanza kushoto waliokaa).
 

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Wasajili na Naibu Wasajili mara baada ya hafla fupi ya uapisho wa Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu Masjala Kuu Mhe. Sundi Fimbo (wa tatu kushoto waliosimama). Wengine Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es salaam, Mhe. Salma Maghimbi (wa kwanza kulia walioketi) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya (wa kwanza kushoto waliokaa).
 
(Picha Innocent Kansha-Mahakama)














Hakuna maoni:

Chapisha Maoni