- Yafanya pia uchaguzi wa Viongozi
Na ASHA
JUMA-Mahakama Morogoro
Chama cha Mahakimu
na Majaji Tanzania (TMJA) Mkoa wa Morogoro hivi karibuni kiliungana na Wafanyakazi
wengine duniani kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani inayofanyika kila mwaka
tarehe 1 Mei, kwa kufanya mkutano maalum uliofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya
Kongamoyo mkoani Morogoro.
Maadhimisho hayo
yalilenga kuwakutanisha pamoja Majaji na Mahakimu kwa ajili ya kusherehekea
siku hiyo muhimu kwa kubadilishana
uzoefu, pamoja na kujengeana uwezo kupitia mafunzo mbalimbali ya kitaaluma
yanayohusu utendaji kazi wa Mhimili wa Mahakama.
Miongoni mwa mada
zilizotolewa ni Muhtasari wa Utamaduni wa Mahakama (Judicial Culture)
nchini Tanzania, ambapo washiriki walipata fursa ya kujifunza kuhusu
misingi, maadili, mila na taratibu zinazoongoza utendaji kazi wa vyombo vya
utoaji haki.
Ilielezwa kuwa
utamaduni wa Mahakama unajengwa juu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, sheria mbalimbali pamoja na kanuni na miongozo ya Mahakama.
Msingi huo ni muhimu katika kuhakikisha haki inatendeka kwa usawa na
ufanisi. Mada hii iliwasilishwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga.
Aidha, mada
nyingine iliyowasilishwa ni Muhtasari wa Sifa na Tabia Muhimu za Uongozi
katika Mhimili wa Mahakama (Overview on Judicial Leadership Attributes),
iliyolenga kuwajengea washiriki uelewa kuhusu sifa zinazopaswa kuzingatiwa na Viongozi wa Mahakama.
Baadhi ya sifa
hizo ni pamoja na uadilifu, hekima na busara katika kufanya maamuzi, uwazi na
uwajibikaji, uwezo wa kusimamia haki kwa usawa, pamoja na kuwa na uongozi wenye
maadili na mfano bora kwa wengine. Mada hii ilitolewa na Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Rose Ebrahim.
Baada ya mafunzo
hayo, wajumbe walipata nafasi ya kufanya uchaguzi wa Viongozi mbalimbali wa TMJA kwa Mkoa wa Morogoro.
Katika uchaguzi huo, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Aisha Sinda, alichaguliwa
kuwa Mwenyekiti na
Mhe. Mbaraka Mchopa akachaguliwa kuwa Makamu
Mwenyekiti. Nafasi ya Katibu ilichukuliwa na Mhe. Joseph Ngwega,
Mhe. David Luvanga akachaguliwa kuwa Mwakilishi wa Taifa, na Mhe. Latifa Kassim
Mohammed kuchukua nafasi ya Mhazini.
Kwa ujumla, maadhimisho hayo yamekuwa na mafanikio makubwa kwa kuimarisha mshikamano miongoni mwa wanachama wa TMJA, kuongeza uelewa wa kitaaluma na kuweka msingi imara wa uongozi bora ndani ya Mhimili wa mahakama mkoani Morogoro.
Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Morogoro, Mhe. Aisha Sinda aliye chaguliwa kuwa Mwenyekiti TMJA Morogoro.
Mhe. Mbaraka Mchopa aliye chaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti.
Mhe. Joseph Ngwega aliye chaguliwa kuwa Katibu.
Mhe. David Luvanga aliye chaguliwa kuwa Mwakilishi wa Taifa.
Mhe. Latifa Kassim
Mohammed aliyechukua nafasi ya Mhazini.
Mahakimu pamoja na
Majaji wakiwa katika viwanja vya Kongamoyo.
HABARI HII IMEHARIRIWA NA FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni