Ijumaa, 5 Januari 2018

IFAHAMU DIVISHENI YA MAKOSA YA RUSHWA NA UHUJUMU UCHUMI YA MAHAKAMA KUU YA TANZANIA

        Serikali yatimiza azma yake ya kuanzisha Mahakama ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi

Na Lydia Churi- Mahakama ya Tanzania
Moja ya ahadi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli katika kampeni za uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 ni kuanzishwa Mahakama itakayokuwa ikishughulika na kesi za ufisadi ikiwa  ni mkakati wake wa kupambana na ufisadi pamoja na matumizi mabaya ya fedha za Umma. Ikiwa ni miaka miwili (2) sasa tangu kuingia kwake madarakani, tumeshuhudia Mahakama hiyo inayoshughulika na Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ikianzishwa Julai 7, 2016, ikiwa ni Divisheni ya Mahakama Kuu ya Tanzania.

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha Sheria ya Marekekebisho mbalimbali ambayo pamoja na mambo mengine inampa Jaji Mkuu Mamlaka ya kuanzisha Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ya Mahakama kuu ya Tanzania. Akiwasilisha Muswada wa Sheria hiyo Bungeni mjini Dodoma, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. George Masaju alisema, “ Divisheni Maalum ya Mahakama kuu itakuwa na Majaji na Watumishi wengine ambao wanahusika moja kwa moja na uendeshaji wa kesi za Rushwa na Uhujumu Uchumi, Hatua hii itawezesha kesi hizi kusikilizwa kwa urahisi na kwa haraka”, alisema Mhe. Masaju.
Kuanzishwa kwa Divisheni hii kunaifanya Mahakama kuu ya Tanzania kuwa na  jumla ya Divisheni nne sasa. Divisheni nyingine za Mahakama kuu ya Tanzania ni ile ya Biashara iliyoanzishwa mwaka 1999 ilifuatiwa na ya Ardhi mwaka 2001, na mwaka 2007 ilianzishwa Divisheni ya Kazi.  

Sheria zilizoanzisha Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi  
Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ilianzishwa kufuatia mabadiliko ya Sheria ya Uhujumu uchumi, sura namba 200 ya sheria za Tanzania yaliyofanyika kupitia sheria namba 3 ya mwaka 2016. Kifungu namba tatu (3) cha Sheria ya Uhujumu Uchumi, kama ilivyofanyiwa marekebisho kupitia sheria namba 3 ya mwaka 2016 kinaanzisha Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi katika ngazi ya Mahakama Kuu.

Sehemu ya Jengo la Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ya Mahakama Kuu ya Tanzania lililopo Sinza jijini Dar es salaam.

Usajili wa Kesi katika Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi
Utaratibu wa kusajili kesi katika Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ya Mahakama Kuu ya Tanzania unafanyika kwa hatua mbili. Usajili wa mashauri katika hatua ya kwanza ufanyika katika Mahakama zote za Hakimu Mkazi/Wilaya hapa nchini. Hatua hii inalenga kutoa nafasi kwa upande wa Jamhuri kukamilisha upelelezi na taratibu zote za awali  za kesi za rushwa na uhujumu uchumi. Katika hatua ya kwanza, iwapo shtaka linalomkabiri mshtakiwa  linahusisha kiasi cha fedha kinachozidi  shilingi za Kitanzania milioni kumi, mshtakiwa  atapaswa kuwasilisha maombi yake ya dhamana kwenye Masjala za  Divisheni ambazo zinapatikana kwenye kila jengo la kanda ya Mahakama kuu, ispokuwa Dar es salaam ambapo Divisheni ina jengo lake maalumu. Maombi ya dhamana katika hatua ya kwanza yanafanyika Mahakama kuu kwa kuwa Mahakama za Hakimu Mkazi/Wilaya hazina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi ispokuwa kwa kibali maalumu kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashtaka nchini.

Hatua ya pili ya usajili wa kesi unafanyika katika masjala zote za Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ya Mahakama kuu baada ya Mkrugenzi wa Mashtaka nchini kuwasilisha taarifa ya Mashtaka. Hatua hii ufuatia kukamilika kwa upelelezi na taratibu zingine za awali katika hatua ya kwanza. Baada ya kuwasilishwa kwa taarifa ya mashtaka usajili wa kesi ufanyika na taratibu za kusikiliza kesi husika huanza mara moja.

Kwa mujibu wa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi Mhe. Charles Magesa, kati ya mwaka 2016 na 2017, mpaka kufikia Novemba 30, 2017 jumla ya mashauri 117 yaliyosajiliwa kwa ajili ya maombi ya dhamana yamesikilizwa na kutolewa uamuzi katika masjala mbalimbali za Divisheni nchini. Alisema kati ya hayo yaliyotolewa uamuzi ni  mashauri 39 ya kanda ya Dar es salaam, Dodoma 15, Iringa 8, Mbeya 10, Mtwara 14, Songea 19, Shinyanga 3 na Tabora 1.   

Mhe. Magesa alisema jumla ya mashauri 14 ya maombi ya dhamana yako katika hatua mbalimbali za usikilizwaji ambapo masjala ya Dar es salaam ina mashauri11, Songea 2 na Dodoma 1 ambayo yanaendelea kusikilizwa kwenye Mahakama hiyo.

Akizungumzia mashauri yaliyokamilika upelelezi wake, Naibu Msajili huyo alisema Mkurugenzi wa Mashtaka nchini tayari amekamilisha na kuwasilisha taarifa za mashtaka za kesi tatu (3) katika masjala ya Divisheni ya Dar es salaam. Taratibu za kusikiliza hoja za awali za kesi hizo zitafanyika na kukamilika kabla ya Desemba 15, 2017 na usikilizaji wa mashauri hayo utafanyika mwanzoni mwa mwezi Februari, 2018.
  
Mamlaka ya Mahakama katika kusikiliza kesi za Rushwa na Uhujumu Uchumi 
Mahakama hii  imepewa Mamlaka ya kusikiliza mashauri ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, aidha Divisheni hii ina mamlaka ya kusikiliza mashauri ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ambayo thamani yake au kiwango cha fedha ni kuanzia shilingi za kitanzania bilioni moja na kuendelea. Aidha, Divisheni ina mamlaka pia ya kusikiliza makosa yote yaliyo orodheshwa katika jedwali la sheria ya uhujumu uchumi  yanayoangukia katika  vifungu vya sheria mbalimbali zilizopo kwenye jedwali sheria ya uhujumu Uchumi bila kujali thamani au kiwango cha fedha. Baadhi ya sheria hizo ni pamoja na Sheria ya kuzuia utakatishaji fedha, sheria ya udhibiti wa madawa ya kulevya, Sheria ya kuzuia ugaidi na sheria ya uhifadhi wa wanyamapori.

Sheria nyingine ni ile ya Uvuvi wa bahari kuu, sheria ya madini, sheria ya silaha na milipuko, sheria ya udhibiti wa silaha, sheria ya misitu na sheria ya petrol. Sheria nyingine ni ya Mafuta na gesi, sheria ya makosa ya mtandao na sheria ya miamala ya kielektroniki.

Divisheni hii ya Mahakama kuu ambayo ni maalum kwa Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi pia inaendeshwa kwa mujibu wa kanuni zilizotolewa la Serikali Namba 267 la tarehe 9/9/2016. Kanuni hizo pamoja na mambo mengine zinaelekeza mambo mbalimbali kama vile taratibu za ufunguaji mashauri, uendeshaji wa mashauri.
Kwa mijibu wa kanuni hizo,ukomo wa muda wa kusikiliza mashauri katika Divisheni ni kipindi kisichozidi miezi tisa (9) tangu kuwasilishwa kwa taarifa ya mashtaka. Aidha, ukomo wa muda wa kusikiliza mashauri unaweza kuongezwa kwa kipindi kisichozidi miezi sita endapo kutakuwa na sababu maalum zitakazopelekea shauri kushindwa kumalizika ndani ya kipindi cha miezi tisa (9).

Mipaka ya kuisajili kesi za Rushwa na Uhujumu Uchumi nchini   
Divisheni hii inayo masjala kumi na nne ambapo mashauri yanaweza kusajiliwa katika masjala yoyote nchini. Masjala hizi ziko katika kanda 14 za Mahakama Kuu ya Tanzania zilizoko kwenye miji ya Tanga, Mwanza, Dodoma, Arusha, Moshi, Sumbawanga, Songea, na Mtwara, Dar es salaam, Tabora, Mbeya, Bukoba, Iringa na Shinyanga.  






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni