· Kamati yaridhishwa na hatua za awali
za ujenzi.
· Yaipongeza Mahakama na Serikali
kuendelea kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi.
Na
Innocent Kansha – Mahakama, Njombe.
Kamati
ya Bunge ya Katiba na Sheria leo tarehe 13 Machi, 2024 imekagua Mradi wa Ujenzi
wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki IJC' kinachojengwa mkoani Njombe chenye thamani ya
shilingi takribani Bilioni 7.6 mradi unaotekelezwa na Mahakama ya Tanzania.
Akizungumza
wakati wa zoezi la ukaguzi wa kituo hicho Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya
Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Kizito Muhagama amesema mradi huo ni moja ya
miradi mikubwa inayotekelezwa nchini kupitia Wizara ya Katiba na Sheria na Mtekelezaji wa mradi ni Mhimili wa Mahakama.
“Mradi
huu ni wa kutoa huduma za sheria kwenye jengo moja ‘Integrated Justice Centre’ ambapo
Mahakama za ngazi mbalimbali zinakuwa katika jengo moja ili kurahisisha
upatikanaji wa haki kwa wananchi lakini pia wanaotoa haki waweze kutekeleza
wajibu wao na majukumu yao kwa namna ambayo ni jumuishi na rahisi zaidi,”
ameeleza Mhe.Dkt. Muhagama.
Mhe.
Dkt. Muhagama amesema, hatua ya ujenzi inayoendelea katika Mradi huo ni
asilimia 5 ni kama hatua za awali za ujenzi na kwa maelezo Kamati iliyopewa
kutoka Serikalini na kwa Mkandarasi ni sawa kwa maana kwamba ujenzi upo ndani ya
muda uliokusudiwa kimkataba.
“Mradi
hauna changamoto za moja kwa moja unazozigusa Serikali kwenye utekelezaji wake.
Kamati ilidhani kuna changamoto za upatikanaji wa vibali kwa maana ya misamaha
ya kodi na Mkandarasi ametuhakikishia kwamba hicho siyo kikwazo katika utekelezaji
wa mradi huo, ni imani yangu pamoja na wajumbe wa kamati hii kwamba Mradi upo
vizuri na utaisha kwa muda uliopangwa,” amesisitiza Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya Bunge.
Kamati
imempongeza Rais wa Jamhuri ya Mhungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa kuthubutu na kwa kuamua kwa dhati kabisa kusogeza huduma ya utoaji
haki kwa wananchi wa Tanzania ambao wanahitaji huduma hiyo inayotekelezwa mkoani
Njombe na maeneo mengine nchini, amesema Mbunge huyo kwa niaba ya Kamati.
“Lakini
hii ni hatua kubwa sana ya kuboresha mifumo ya utoaji haki nchini ikizingatiwa
kwamba, tunaendelea kuijenga Tanzania ambayo ina hali ya utulivu na amani ya
kutosha,” amesema Mhe. Muhagama.
Aidha,
Mhe. Dkt. Muhagama ameongeza kuwa, kwakuwa Mradi huo umeshuhudiwa na Wabunge wa Kamati
hiyo kwa pamoja ni imani yao kuwa changamoto zozote zitakazojitokeza
zitatolewa taarifa kwa ukaribu zaidi ili wakati wa kupanga bajeti zisaidie kutatuliwa
kwa mwaka ujao wa fedha ambao utahusu pia uendelezaji na ujenzi wa miundombinu
ya utoaji haki kwa Watanzania.
Kwa upande wake, Waziri wa Katiba na Sheria
Mhe. Dkt. Pindi Chana amesema ukaguzi huo wa Kamati ya Bunge ya
Katiba na Sheria unaenda sambamba na maelekezo ya Rais Samia ya kuboresha miundombinu
ya utoaji haki kwa maana ya “Reforms & Rebuilding” ili Watanzania wote
wapate haki kwa usawa na kwa wakati kama ilivyokusudiwa.
“Kamati
hii ya Bunge inatusaidia sana mawazo mapendekezo ya namna bora ya kuboresha
shughuli za utoaji haki kupitia Serikali na Mahakama. Japo kuwa tunajua jukumu
la Bunge ni kupitisha bajeti, kutunga sheria na kuisimamia Serikali. Hivyo leo
tupo katika jukumu mojawapo la Bunge la kusimamia Serikali ‘Oversight role’ ya
kupitia Kamati ya Bunge baada ya kupitisha Bajeti hii ndiyo kazi ya Kamati,”
amesema Mhe. Dkt. Chana.
Mhe.
Dkt. Chana amesema, kupitia Wizara ya Katiba na Sheria imedhamiria kuhakikisha
utawala wa sheria unakuwa ni miongoni mwa vipaumbele vya Serikali.
“Tunataka
kuona wawekezaji wakija wawe na imani na Utawala wa Sheria, tunataka Watanzania
waishi kwa amani, kwa uhuru kusiwepo na changamoto za kijinai na pale
zinapojitokeza basi tuwe na miundombinu ya kudhibiti na kukabiliana nazo,”
Mhe.
Dkt. Chana ameongeza kuwa miundombinu hiyo inayojengwa inakwenda sambamba na
matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kuendana na kasi
ya ukuaji wa teknolojia Duniani hasa katika eneo la utoaji haki, ikiwa ni
pamoja na mradi wa ujenzi wa IJC Njombe.
Naye, Mkadiriaji Majengo kutoka
Mahakama ya Tanzania, Bw. Abdallah Nalicho akifanya
wasilisho fupi la Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) mkoani
Njombe, amesema kuwa ujenzi wa kituo hicho umezingatia mahitaji mbalimbali
yanayoendana na uhalisia na matarajio ya wananchi watakaopata huduma za haki ndani
ya jengo hilo. Kwa kupunguza gharama za uendeshaji wa mashauri, kuokoa muda na
kuongeza uwazi na uwajibikaji kwa watoa haki.
“Mathalani
usanifu wa jengo hili umezingatia mahitaji ya watu wenye mahitaji maalum mfano;
walemavu, watoto, akina mama wanaonyonyesha na wajawazito, wazee wasiojiweza na wadau
mbambali katika mnyororo wa utoaji haki wanaosaidiana na Mahakama (waendesha
mashtaka, mawakili wa kujitengemea, watoa ushauri wa kisheria, ustawi wa jamii,
dawati la jinsia na Mahakama maalum kwa ajili ya watoto waliokinzana na Sheria,”
ameongeza Bw. Nalicho.
Akielezea faida za ziada za ujenzi wa Kituo hicho, Bw. Nalicho amesema kimesaidia kutoa
ajira kwa wataalum wa masuala ya ujenzi wapatao 23 na wafanyakazi
wasio wataaluma wa ujenzi wenyeji wa Mkoa wa Njombe na hivyo kukuza na kuongeza
kipato cha wananchi kupitia Mradi huo.
Mwenyekiti wa Kamti ya Bunge ya Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Joseph Kizito Muhagama(wa pili kulia) akizungumza na Waandishi wa Habari wakati wa ukaguzi wa Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) mkoani Njombe leo tarehe 13 Machi, 2024.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Pindi Chana akizungumza na Wanahabari wakati wa ukaguzi uliofanywa na Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria kwenye Mradi wa ujenzi wa IJC mkoani Njombe.
Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Pindi Chana akizungumza na wanahabari wakati wa ukaguzi wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria wakikangua ujenzi wa mradi wa IJC mkoani Njombe.
Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria wakichangia wasilisho la taarifa ya Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kinachojengwa mkoani Njombe na Mahakama ya Tanzania.
Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria wakichangia wasilisho la taarifa ya mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kinachojengwa mkoani Njombe na Mahakama ya Tanzania.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Pindi Chana akichangia jambo wakati wa kuwasilisha taarifa fupi ya Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha utoaji haki mkoani Njombe wakati wa ukaguzi wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria.
Mkadiriaji Majengo kutoka Mahakama ya Tanzania, Bw. Abdallah Nalicho akifanya wasilisho fupi la Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) mkoani Njombe.
Mkadiriaji Majengo kutoka Mahakama ya Tanzania, Abdallah Chande Nalicho akifanya wasilisho fupi la Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) mkoani Njombe.
Mwenyekiti wa Kamtai ya Bunge ya Katiba na sheria Mhe. Dkt. Joseph Kizito Muhagama (katikati) akisema jambo wakati wa wasilisho la mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki mkoani Njombe wakati wa ukaguzi wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria mkoani Njombe.
Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Katiba na sheria wakifuatilia wasilisho la taarifa ya mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kinachojengwa mkoani Njombe na Mahakama ya Tanzania. Kulia ni Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Pindi Chana.
Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Katiba na sheria wakifuatilia wasilisho la taarifa ya mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kinachojengwa mkoani Njombe na Mahakama ya Tanzania. Kulia ni Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Pindi Chana.
Mwenyekiti wa Kamti ya Bunge ya Katiba na sheria Mhe. Dkt. Joseph Kizito Muhagama (katikati) akifuatilia wasilisho la Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki mkoani Njombe wakati wa ukaguzi wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria mkoani Njombe.
Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Njombe, Bw. Yusuph Msawanga akitoa taarifa ya maendeleo ya Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki mkoani Njombe wakati wa ukaguzi wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria mkoani Njombe.
Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Katiba na sheria wakiwasili katika eneo la Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) mkoani Njombe leo tarehe 13 Machi, 2024.
Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria wakiwasili katika eneo la Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) mkoani Njombe leo tarehe 13 Machi, 2024.
(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)