Jumamosi, 27 Aprili 2024

WATUMISHI WAWILI WALIOKOMA UTUMISHI WAAGWA MAHAKAMA KUU SONGEA

Na Hasani Haufi- Mahakama, Songea.

Watumishi wawili wa Mahakama Kuu Songea, ambao ni Bi. Baina Chowo, Msaidizi wa Ofisi pamoja na Maurus Kapinga, Mlinzi ambao ajira yao imekoma kwa kustaafu kwa umri Machi 2024, wameagwa na watumishi wa Mahakama Kuu Songea.

Hafla hiyo iliyofanyika tarehe 25 Aprili, 2024, kwenye ukumbi wa wazi Mahakama Kuu Songea, iliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha. 

Viongozi wengine waliokuwepo ni Jaji wa Mahakama Kuu Songea, Mhe. Upendo Madeha, Naibu Msajili wa Mahakama Kanda ya Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele na Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Songea Bw. Epaphras Tenganamba.

Akizungumza katika hafla hiyo, Jaji Karayemaha aliwapongeza wastaafu hao kwa kuwa na subra na kufanya kazi na vizazi mbalimbali hadi kufikia umri wa kukoma utumishi wao bila kuingia katika shida wala misukosuko na mwajiri.

“Ninachoweza kusema kwa niaba ya watumishi wote wa Mahakama Kuu Songea, kuwa nawapongeza sana kwa subra mliyokuwanayo, kwani bila ya kuwa na subra msingeweza kufanya kazi na vizazi mbalimbali,” alisema.

Jaji Mfawidhi aliwashukuru kwa muda wao wote waliotumikia Mhimili wa wa Mahakama ya Tanzania na Taifa kwa ujumla na kudumisha upendo kwa watumishi wengine bila kuangalia wadhifa wake.

“Niwashukuru sana kwa muda wenu wote mliojitoa kutumikia Taifa na Mhimili wa Mahakama ya Tanzania, najivunia kuona mmedumisha upendo kwa kila mtu,” alisema.

Aidha, Mhe. Karayemaha aliwakabidhi wastaafu hao zawadi, ikiwa ni sehemu ya upendo na shukrani ambazo kwa kipindi cha utumishi wao walikuwa wakidumisha kwa wengine.

Naye Mhe. Madeha aliwaasa kuwa wachamungu na kuwasihi kutumia vizuri fedha za mafao watakazozipata ili ziendelee kuwajenga na kutafakali watazifanyia nini.

“Hongereni sana, kimsingi safari hii ni ndefu, hivyo aliyeifanikisha hii safari ni mungu, mnapaswa kuwa wachamungu. Bila kusahau, fedha mtakazozipata mzitumie vizuri, muwe na malengo nazo ili ziendelee kuwajenga na mtafakari kwa kina nanma ya kuzitumia,” alisema.

Alitumia nafasi hiyo kuwasihi watumishi wote kwa ujumla kujifunza kwa wastaafu hao na kufanya maandalizi ya kustaafu kwa kujishughulisha na shughuli za kijamii na kiuchumi kama kilimo, ufugaji na biashara ili kuweza kujikwamua katika maisha. 

“Tujifunze kwa wenzetu wanaostaafu, kwa kufanya maandalizi, pia mshahara wako uufanyie kitu cha maana, uwe na kitu cha kuonyesha. Tujishirikishe na shughuli zingine za kijamii na kiuchumi, anza kujifunza kilimo, kufuga na biashara,” alisema.

Kwa upande wa ke, Mhe. Nyembele alisisitiza upendo kwani ni agizo kutoka kwa Mungu linasema, ukiwa na upendo huwezi kumkwaza mtu na utamwombea mwenzio anapopatwa na shida au anapolielekea jambo fulani.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha akikabidhi zawadi kwa wastaafu (juu na chini).


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Songea, Mhe. Upendo Madeha akizungumza na wastaafu pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Songea (hawapo kwenye picha.)

Naibu Msajili wa Mahakama Kanda Songea, Mhe. Elizabeth Nyembele akitoa neno fupi kwa wastaafu hao.


Sehemu ya watumishi wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa hafla hiyo.

Wastaafu kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu Songea (wa pili kutoka kushoto na wa pili kutoka kulia) akiwemo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kanda ya Songea, Mhe. James Karayemaha (watatu kutoka kulia.) 

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

 

Ijumaa, 26 Aprili 2024

JAJI MKUU ASHIRIKI MAADHIMISHO MIAKA 60 YA MUUNGANO TANZANIA

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma leo tarehe 26 Aprili, 2024 ameungana na Watanzania nchini kote kuadhimisha miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliozaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Prof. Juma aliwasili katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam mapema asubuhi kuungana na Viongozi wengine wa Kitaifa na Kimataifa kwenye maadhimisho hayo ambayo Mgeni Rasmi alikuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan. 

Sehemu ya Viongozi wengine wa Kitaifa waliohudhuria maadhimisho hayo ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango.

Wengine ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Mhe. Kassim Majaliwa KassimSpika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Mawaziri wa Wizara mbalimbali, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Mikoa na Viongozi wengine.

Maadhimisho hayo yamehudhuriwa pia na Marais na wawakilishi kutoka Nchi mbalimbali za Bara la Afrika, ikiwemo kutoka Kenya, Uganda, Comoro, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Zimbabwe, Burundi, Zambia, Somaria, Namibia pamoja na Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini.

Gwaride maalum lililoandaliwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania, Polisi na Magereza limepamba maadhimisho hayo, licha ya mvua kubwa iliyokuwa inanyesha.Rais Samia amekagua gwaride hilo na kupokea salamu za utii.

Wakati wa maadhimisho hayo, gwaride hilo lilipita mbele ya Rais na wageni mbalimbali kwa mwendo wa pole na baadaye mwendo wa haraka na kushangiliwa na wananchi waliokuwa wamefurika kwa wingi katika Uwanja wa Uhuru.

Katika miaka 60 ya uhuruTanzania imefanikiwa kupiga hatua katika maendeleo katika nyanja mbalimbali, ikiwemo kuulinda uhuru na mipaka, kudumisha amani; kuimiraisha uchumi  na demokrasia na kuboresha huduma za kujamii.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliundwa tarehe 26 Aprili, 1964, ikiwa ni Muungano wa Mataifa mawili huru ya Jamhuri yaTanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar ambayo yaliingia mkataba wa Muungano mnamo mwaka 1964 na kuanzishwa Dola ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mkataba wa Muungano ulitiwa saini na aliyekuwa Rais wa Tanganyika, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, tarehe 22 Aprili, 1964 huko Zanzibar.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kulia aliyeangalia pembeni) akiwa na Viongozi wengine wa Serikali wakati wa maadhimisho ya miaka 60 ya muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wengine ni Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Tulia Ackson (katikati) na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Dotto Biteko. Picha chini ni sehemu ya Viongozi wengine waliohudhuria maadhimisho hayo.


Sehemu ya Wananchi (juu na chini) waliofurika kwenye Uwanja wa Uhuru kwenye maadhimisho hayo.


Gwaride maalum lililoandaliwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania, Polisi na Magereza likiingia katika Uwanja wa Uhuru kwenye maadhimisho hayo.

Kikosi ya Bendera katika gwaride maalum lililoandaliwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania, Polisi na Magereza kikitoa heshima mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan (hayupo kwenye picha) wakati wa maadhimisho hayo.

Mwalimu Julius Kambarage Nyerere (kushoto) na Sheikh Abeid Amani Karume (kulia) wakibadilishana Hati za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar tarehe 27 Aprili, 1964.

 



 

 







 

WANAFUNZI WA SHULE YA MSINGI BANGWE WAVUTIWA KUSOMA SHERIA

Na Aidan Robert-Mahakama, Kigoma

 Wanafunzi wa Shule ya Msingi Bangwe wamepatiwa elimu kuhusu Sheria na huduma zitolewazo na Mahakama, ambapo wameonesha bashasha isiyo na kifani wakitamani kufahamu sifa za kuwa Hakimu au Jaji.

 

Akitoa elimu ya Mahakama kwa wanafunzi hao waliotembelea Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma leo tarehe 25 Aprili, 2024 Msadizi wa Sheria wa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma ambaye pia ni Katibu wa Kamati ya Elimu kwa Umma, Mhe. Victor Kagina amewaeleza wanafunzi hao kuwa, ili mtu awe Hakimu takwa la msingi ni masomo ya Sheria kwa kiwango cha Shahada.

 

 Amewasihi kuwa, wasome kwa bidii huku kipaumbele chao kiwe nidhamu na utii ili kufikia ndoto zao ili nao waje kuwa Majaji na Mahakimu wa siku zijazo.

 

Aidha, wanafunzi hao waliomba kufahamu kuwa Jaji au Hakimu wanapewa na nani mamlaka ya kutoa hukumu kwa wanadamu wenzao. Akijibu swali hilo, Mhe. Kagina amewajuza Wanafunzi hao kwamba, Majaji na Mahakimu hupata mamlaka ya kutoa hukumu kutoka kwenye Katiba na Sheria, Taratibu na Kanuni mbalimbali za Nchi.

 

Kadhalika, wanafunzi hao walihitaji kufahamishwa juu ya muundo wa Mahakama, ambapo Mhe. Kagina amewafundisha kuwa, kuna Mahakama ya Mwanzo, Mahakama ya Wilaya, Mahakama ya  Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani ambapo ameongeza kuwa, Mahakama ya Rufani ndio Mahakama ya juu katika utoaji wa haki nchini Tanzania.

 

 “Shughuli ya msingi ya Mahakama ni pamoja na kusikiliza mashauri na kutoa uamuzi wa haki kwa wakati bila upendeleo kwa mtu yeyote,” amesisitiza Mhe. Kagina.

 

Mmoja kati ya wanafunzi hao alihitaji kufahamu, ni watu gani wanaostahili kupata huduma za kimahakama, ambapo Mhe. Kagina aliwajulisha kuwa, ni mtu yeyote mwenye uhitaji wa huduma hizo kwa matakwa yake ama kwa matakwa ya Jamhuri, huku akitoa mifano ya wanaokuja mahakamani kwa mashauri ya madai na wale wanaoletwa Mahakamani kwa matakwa ya kisheria hususani kwa mashauri ya jinai. 

 

Na kwa upande wake Mwalimu wa shule hiyo, Bw.Alexander Toyi, ameushukuru Uongozi wa Mahakama Kuu Kigoma  kupokea maombi ya kutembelea Mahakama hiyo, kwakuwa wamejifunza na kufahamu huduma zitolewazo na Mahakama.

 

 Vilevile amemshukuru Mkufunzi wa wanafunzi hao, Mhe Victor Kagina, kwa ubora na msingi mkubwa wa elimu aliyoitoa kwa wanafunzi hao kuwa itakuwa chachu kwa maendeleo ya masomo yao shuleni.

 

Msadizi wa Sheria wa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kigoma ambaye pia ni Katibu wa Kamati ya Elimu kwa Umma, Mhe. Victor Kagina akifafanua jambo kwa wanafunzi wa darasa la saba wa shule ya msingi Bangwe-Kigoma waliofika kutembea Mahakama Kuu Kigoma leo tarehe 25 Aprili, 2024 kwa lengo la kujifunza.


 

Picha ya wanafunzi na mwalimu wao wakiwa wameketi katika ukumbi wa Mahakama ya wazi uliopo kwenye jengo la Mahakama Kuu Kigoma wakimsikiliza kwa makini Mhe. Victor Kagina, alipokuwa akifundisha.

 

Picha ya Mwanafunzi, Dorcas Alfonce (kulia) akimuuliza swali Mhe. Victor Kagina, ambaye alikuwa akitoa majibu hapo kwa hapo kwa wanafunzi hao wa darasa la saba katika shule ya msingi Bangwe-Kigoma.


 

Picha ya pamoja ya Msaidizi wa Sheria wa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kigoma ambaye pia ni Katibu wa Kamati ya Elimu kwa Umma, Mhe. Victor Kagina (katikati) na kushoto ni Mwalimu wa Darasa la Saba katika Shule ya Msingi Bangwe, Bw. Alexander Toyi, na kulia ni Mkutubi Msaidizi wa Mahakama Kuu Kigoma, Bi. Magdalena Ndumbili na nyuma yao ni wanafunzi wa Darasa la Saba kutoka Shule ya Msingi Bangwe Kigoma.

 

(Habari hii imehaririwa na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma)

Alhamisi, 25 Aprili 2024

JAJI KIONGOZI: TEHAMA IMEPUNGUZA MUDA WA SHAURI KUKAA MAHAKAMANI NA MLUNDIKANO

 Na Magreth Kinabo-Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Mohamed Siyani amesema matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika mchakato wa usikilizaji wa mashauri, yamesaidia kupunguza muda wa shauri kuwa mahakamani na mlundikano wa mashauri, hivyo ni hatua ambayo Mahakama inapaswa kujivunia

Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 25 Aprili, 2024 na Mhe. Siyani wakati akitoa hotuba yake ya ufunguzi wa kikao cha tatu cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu Masjala Kuu katika ukumbi wa hoteli ya Alexander mjini Iringa.

Mwaka 2023, kwa mfano; Mahakama ilikuwa na mlundikano wa asilimia nne (4), hata hivyo kufikia mwezi Machi, 2024 mlundikano wa mashauri umepungua hadi kufikia asilimia tatu (3). TEHAMA pia imewezesha muda wa kumaliza mashauri unaopimwa kila mwisho wa mwaka kupungua. 

Kwa mfano mwaka 2023 mahakama ilitumia wastani wa siku themanini na nne (84) kukamilisha usikilizwaji na utoaji wa maamuzi kwa shauri, ukilinganisha na siku 95 kwa mwaka 2022. Haya ni mafanikio makubwa tunayopaswa kujivunia,” amesema Jaji Kiongozi

Aidha Mhe. Jaji Siyani kupitia baraza hiloamesisitiza juu ya umuhimu wa watumishi wote kukumbuka malengo tuliyojiwekea kama taasisi katika kutoa huduma kwa wananchi sambamba na kufahamu mipango ya kufanikisha malengo hayo ili kuwezesha kila mmoja kushiriki kikamilifu kutekeleza mipango hiyo. Malengo makuu yameainishwa katika mpango Mkakati wa Mahakama tunaoutekeleza sasa ambayo ni kupunguza muda wa mashauri kuwa Mahakamani na kuongeza imani kwa wananchi kwa kutoa huduma bora kwa wakati. 

Kwa hiyo kila mmoja wetu anao wajibu wa kuhakikisha malengo hayo yanatimia katika viwango stahiki. Ni vyema watumishi wa mahakama wakafahamu vigezo vinavyotumika kupima ufanisi wetu wa kazi  ili kila mmoja aweze kujua jinsi ya kuchangia katika vipimo hivyo na hii itatutoa katika utendaji kazi kwa mazoea na hivyo kutekeleza majukumu yetu kimkakati. Hili ni muhimu kwa sababu, jukumu la kuhakikisha lengo la kutoa haki sawa kwa wote na kwa wakati linafikiwa, ni la kila mmoja wetu,amesisitiza.

Akizungumzia kuhusu Baraza hilo la wafanyakazi, amesema ni fursa ya kisheria kwa watumishi kujadiliana na menejimenti ya taasisi yao juu ya masuala mbalimbali ya msingi yanayohusu tija na ufanisi kwa upande mmoja; na maslahi yao kama watumishi kwa upande mwingine. Kwa hiyo; mabaraza haya ni chombo cha ya kusikiliza changamoto za wafanyakazi lakini ni mashine ya kuchakata changamoto hizo kwa lengo la kuimarisha mazingira ya kazi kwa faida ya pande zote mbili. 

Mhe. Jaji Siyani amewakumbusha umuhimu wa kufanya kazi kwa uadilifu na uweledi. Huku akisema mambo haya mawili ni kama ibada, hatuwezi kuacha kukumbushana kila tunapokutana

Nitumie fursa hii kuwapongeza watumishi wote wa mahakama kote nchini wanaoendelea kuchapa kazi kwa juhudi, uadilifu, akili na weledi licha ya changamoto zilizopo. Ninatambua yapo matukio machache yanayoashiria ukosefu wa maadili. Niwahakikishie uongozi wa Mahakama utaendelea kuchukua hatua stahiki dhidi ya vitendo hivyo ili kulinda hadhi ya mhimili wetu na kujenga imani ya wananchi kwa taasisi hii,” amesema

Aliwataka watumishi hao kujenga umoja, amani na mshikamano miongoni mwaoKwa kuwa mambo haya matatu ni muhimu na ya msingi kwa mendeleo ya taasisi yoyote.Hivyo ni lazima sote tuepuke majungu na mambo yanayoweza kuharibu mahusiano yetu. Badala ya watu kupiga ubuyu kazini, ni bora wapige kazi. 

Jaji Kiongozi huyo amefafanua kuwa mahusiano kazini yanaweza kujengwa kwa njia nyingi. Moja wapo ni ushiriki wa michezo na uanzishwaji wa vikundi vya mazoezi, hivyo  kupitia baraza hilaliwaomba viongozi wa mahakama kote nchini, kuanzisha utaratibu wa mazoezi kazini pamoja na michezo katika muda ambao hautaathiri majukumu ya kazi.

Amewasihi wajumbe wa baraza hilo kuwa wa kwanza kubadilika kutokana na elimu watakayojifunza, kisha waifikishe wenzao waliobaki vituoni, ili nao iwasaidie kubadilika na hatimaye mabadiliko hayo yaongeze tija katika utekelezaji wa kazi zao.

 Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania,Mhe. Mustapher Mohamed Siyani akisisitiza jambo wakati akiongea na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kuu - Masjala Kuu.

  Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) wakifuatilia mjadala wakati wa kikao hicho.

 Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) (juu na picha mbili chini) wakiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustapher Mohamed Siyani (mwenye miwani aliyekaa katikati)


 

 

 

WATUMISHI WA MAHAKAMA WASISITIZWA KUWA WAADILIFU, WELEDI

Na Lusako Mwang’onda-Mahakama, Iringa

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania wametakiwa kufanya kazi kwa ueledi na uadilifu wa hali ya juu wakiwa katika majukumu yao ya kuwatumikia wananchi. 

Hayo yamesemwa leo tarehe 25 Aprili, 2024 na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustafa Mohamed Siyani wakati wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu (Masjala Kuu) kilichofanyika mjini hapa katika Hoteli ya Mount Royal Villa. 

Mhe. Siyani amesema si vyema kwa mtumishi wa Mahakama kuwa na uadilifu unaotiliwa shaka maana hali hiyo hushusha Imani ya wananchi kwa Mahakama.

Jaji Kiongozi, ambaye kikanuni ndiyo Mwenyekiti wa Kikao hicho amesema, “imani ya wananchi ni kubwa sana kwa Mahakama, hivyo uongozi wa Mahakama hautamfumbia macho mtu yeyote ambaye kwa namna yeyote ile atataka kuitia doa Imani waliyonayo wananchi kwa muhimili huu”.

Kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi ambacho kikanuni kinakuwa chini ya uenyekiti wa Jaji Kiongozi kimehudhuriwa pia na Viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) na kwa upande mwingine viongozi na wawakilishi wa Chama cha Wafanyakazi yaani TUGHE nao walikuwepo kuwasilisha hoja za Wafanyakazi.

Kikao hicho cha Baraza la Wafanyakazi kimetoka na maazimio mbalimbali, ikiwemo Matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kuendelea kupewa kipaumbele katika uendeshaji wa shughuli mbalimbali za kimahakama. 

Naye mwenyekiti wa kikao hicho, amesisitiza kuwa kufanya kazi kwa weledi katika zama hizi ni lazima kuendane na matumizi ya TEHAMA. 


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustafa Mohamed Siyani akisisitiza jambo wakati akiongea na wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Mahakama Kuu - Masjala Kuu.

Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) wakifuatilia mjadala wakati wa kikao hicho.

Mtendaji wa Mahakama ya Kuu ya Tanzania (MMK), Bw.Leonard Magacha akifuatilia kwa makini mijadala mbalimbali wakati wa kikao hicho cha Baraza.

Makundi mbambali ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) (juu na chini) wakiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustafa Mohamed Siyani (mwenye miwani aliyekaa katikati).

Makundi mengine ya Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (Masjala Kuu) (juu na picha mbili chini) wakiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Mustafa Mohamed Siyani (mwenye miwani aliyekaa katikati).


Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam).