Alhamisi, 3 Julai 2025

JAJI MKUU MASAJU ASISITIZA MAADILI, UADILIFU KWA MAWAKILI WAPYA

Na FAUSTINE KAPAMA na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju amewahimiza Mawakili wapya kuzingatia maadili, uadilifu na weledi na kuishi viapo vyao wanapotekeleza majukumu yao katika muktadha mzima wa utoaji haki kwa Wananchi.

Mhe. Masaju, ambaye ni Jaji Mkuu wa tisa wa Tanzania na Jaji Mkuu wa saba Mtanzania, ametoa wito huo leo tarehe 3 Julai, 2025 baada ya kuwapokea na kuwakubali waombaji 449 kuwa Mawakili wa Kujitegemea.

Hili ni tukio lake la kwanza tangu alipoapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu tarehe 15 Juni, 2025, kuwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania.

Katika hotuba yake kwenye sherehe hiyo ya uapisho iliyofanyika katika ukumbi wa Jiji Mtumba Jijini Dodoma, Jaji Mkuu Masaju amewakumbusha Mawakili kuwa taaluma ya sheria ni wito wa kuhudumia wananchi kwa haki na sio njia ya kujinufaisha binafsi.

“Mnaingia kwenye taaluma nyeti inayogusa maisha ya watu. Haki ya mwananchi inaweza kupatikana au kupotea kupitia maneno yenu. Kuweni waadilifu, wenye maadili, na waaminifu kwa wito wenu,” amesema Mhe. Masaju kwa msisitizo.

Ameongeza kuwa Mawakili wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kutetea haki za wanyonge, kulinda Katiba na kushiriki kikamilifu katika mageuzi ya kimahakama yanayoendelea nchini.

Hafla hiyo imehudhuriwa na Viongozi wa Mahakama, wakiwemo Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania. Alikuwepo pia Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wakili Mkuu wa Serikali.

Wengine ni Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Mashtaka nchini, mwakilishi wa Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), familia za Mawakili wapya na Wadau mbalimbali wa sekta ya sheria.

Uapisho huo unaashiria mwanzo mpya kwa Mawakili hao katika kujenga jamii yenye haki, usawa na utawala bora wa sheria.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju-juu na chini-akizungumza kwenye sherehe ya kuwapokea na kuwakubali Mawakili wa Kujitegemea wapya 449 leo tarehe 3 Julai, 2025 jijini Dodoma.


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa utambulisho wa wageni mbalimbali.
Sehemu ya Mawakili wapya-juu na chini-wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa sherehe hiyo.


Viongozi mbalimbali, wakiwemo Majaji Wastaafu wakiwa kwenye sherehe hiyo. Picha chini ni wageni mbalimbali wakifuatilia kilichokuwa kinajiri.


Meza Kuu inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju.

Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania-juu na chini-wakiwa kwenye sherehe hizo.


Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa sherehe hiyo. Kushoto ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa na kulia ni Naibu Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sundi Fimbo.


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni