Alhamisi, 3 Julai 2025

TUKIO LA KWANZA LA JAJI MKUU MASAJU

  • Awapokea, awakubali Mawakili wapya zaidi ya 400

Na FAUSTINE KAPAMA na ARAPHA RUSHEKE- Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju leo tarehe 3 Julai, 2025 amewapokea na kuwakubali waombaji 449, wakiwemo wanaume 252 na wanawake 197, kuwa Mawakili wapya wa Kujitegeme.

Hili ni tukio kubwa la kwanza kwa Mhe. Masaju kulifanya tangu alipoapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tarehe 15 Juni, 2025, kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania.

Sherehe hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Jiji uliopo Mtumba katika Ofisi za Serikali na kuhudhuriwa na Majaji wa Mahakama ya Rufani, Majaji wa Mahakama Kuu na Viongozi wengine wa Mahakama.

Walikuwepo pia Viongozi wengine, akiwemo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, mwakilishi wa Mkurugenzi wa Mashtaka, Wakili Mkuu wa Serikali, Viongozi wa Baraza la Elimu ya Sheria na Wananchi kwa ujumla.

Miongoni mwa Mawakili hao wapya, 81 ni wale waliopata msamaha wa kutohudhuria Shule ya Sheria kwa Vitendo baada ya kuhudumu katika masuala ya kisheria kwa muda mrefu.

Yupo pia mmoja aliyefaulu mtihani wakuwa Wakili na wengine 367 waliofaulu katika Shule ya Sheria kwa Vitendo.

“Kwa mamlaka niliyopewa na Sheria ya Mawakili Sura 341, Kifungu cha 16 (4) natamka kwamba wale wote ambao majina yao yamesomwa hapa wamekubaliwa kuwa Mawakili na wameingizwa rasmi kwenye daftari la Mawakili kuanzia leo tarehe 3 Julai, 2025," amesikika Jaji Mkuu akitangaza mara baada ya kuwakubali na kuwapokea Mawakili hao wapya.

Tukio hilo la kuwapokea na kuwakubali Mawakili hao wapya 449 lililofanywa na Jaji Mkuu linafĂ nya idadi ya Mawakili nchini kuongezeka na kufikia 13,446.

Baada ya kukubaliwa, Jaji Mkuu wa Tanzania aliwatunuku vyeti vya uwakili na kusema, “Kwa mamlaka niliyopewa na Sheria ya Mawakili Sura 341, Kifungu cha 16 (4), nawatunuku vyeti vya uwakili nyinyi wote Mawakili mliopokelewa na kukubaliwa kuwa Mawakili.”

Kisha Mawakili hao walikula kiapo cha uadilifu mbele ya Msaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa. Msajili wa Mahakama Kuu amewakumbusha Mawakili ambao bado ni watumishi wa umma kujiepusha na vitendo vya kuanza kutetea wateja hadi hapo watakapofika ukomo katika utumishi wao.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju-kushoto-akiwapokea na kuwakubali Mawakili wapya 449 leo tarehe 3 Julai, 2025 jijini Dodoma. Picha chini, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa akiratibu zoezi hilo.

Mawakili wapya-juu na picha mbili chini-wakitoa heshima kwa Jaji Mkuu baada ya kupokelewa na kukubaliwa kuwa Mawakili wa Kujitegemea.

Majaji wa Mahakama ya Rufani, wakiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mchecha Masaju-katikati- na Mahakama Kuu ya Tanzania-juu na chini-wakipokea heshima kutoka kwa Mawakili wapya.

Jopo linaloongozwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari-katikati likipokea heshima kutoka kwa Mawakili hao wapya. Picha chini ni Viongozi wa Baraza la Elimu ya Sheria.

Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa-kushoto-akiwaongoza Mawakili wapya kula kiapo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni