Jumatatu, 26 Machi 2018

KUNDI LA PILI LA MAJAJI WA MAHAKAMA KUU YA TANZANIA WAENDELEA NA MAFUNZO KUHUSU MASHAURI YANAYOHUSU KATIBA NA MATUMIZI YA TEHAMA KATIKA UTOAJI HAKI



Na Mary Gwera
Jumla ya Majaji 32 wa Mahakama Kuu ya Tanzania wanaendelea kupatiwa Mafunzo jijini Arusha lengo likiwa ni kuboresha huduma ya utoaji haki nchini.

Katika mahojiano maalum na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto yaliyofanyika Machi 26, 2018 katika Ukumbi wa Mikutano wa AICC jijini Arusha, Mhe. Jaji Dkt. Paul Kihwelo amesema kuwa Majaji hao wanaoshiriki katika Mafunzo hayo ni wa awamu ya pili.

“Mafunzo haya ya siku tano (5) yaliyoanza Machi 24 na kumalizika Machi 28, 2018 yamejikita katika maeneo mawili ambayo ni ‘Namna ya uendeshaji wa Mashauri ya Kikatiba’ na ‘Matumizi ya TEHAMA katika kutoa haki,” alisema Mhe. Kihwelo.

Mhe. Jaji Kihwelo alisema kwa kuwa moja ya Vipaumbele vya Mahakama katika Mpango Mkakati wake ni pamoja na Matumizi ya TEHAMA, hivyo wameona ni vyema kutoa mafunzo kwa awamu ka Waheshimiwa Majaji na Watumishi wengine ili kujua matumizi ya TEHAMA na changamoto zake.

Mkuu huyo wa Chuo amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo Waheshimiwa Majaji juu ya maeneo hayo na vilevile kujenga taswira chanya ya Mahakama.

“Katika mafunzo haya, Waheshimiwa Majaji wamepewa ufafanuzi juu ya Sera ya TEHAMA ya Taifa pamoja na mifumo ili  wanapotumia Vifaa vya TEHAMA pamoja na mifumo yake iliyopo Mahakamani wazingatie taratibu na miongozo kama zilivyoainishwa katika Sera hiyo,” alifafanua Mhe. Jaji Kihwelo.

Mhe. Kihwelo aliendelea kusema kuwa baada ya Mafunzo hayo kukamilika wanatarajia kuwa na uelewa wa pamoja ili kurahisisha utekelezaji wa lengo la Mahakama ya kuwa Mahakama mtandao ‘e-Judiciary’.

Aidha Mhe. Jaji Kihwelo aliongeza kuwa wanatarajia Weledi wa Majaji kuongezeka juu ya namna bora zaidi ya uendeshaji wa Mashauri ya Kikatiba.

“Mashauri ya Kikatiba ni Mashauri ambayo hupelekwa Mahakamani kupinga ukiukwaji wa Katiba au kudai haki ya Kikatiba,” alifafanua Mhe. Kihwelo.

Mhe. Jaji Kihwelo anafafanua zaidi kuwa Mashauri ya Kikatiba ni mashauri ambayo hufunguliwa Masjala Kuu ya Mahakama Kuu inapokaa kama Mahakama ya Kikatiba na huendeshwa na Majaji watatu.


Mafunzo haya ya Waheshimiwa Majaji yameandaliwa na Mahakama ya Tanzania kwa ufadhili wa fedha za Mradi wa Benki ya Dunia na kuratibiwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.
 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu-Kanda ya Mtwara, Mhe. Jaji Fauz Twaib (kushoto) akifurahia jambo na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama-Lushoto, Mhe. Jaji Dkt. Paul Kihwelo.

Baadhi ya Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu wanaoshiriki katika Mafunzo wakiwa katika kazi ya kikundi ‘group work’, Mafunzo hayo yanafanyika AICC mkoani Arusha.

Majadiliano yakiendelea.
Waheshimiwa Majaji wakiendelea kujadiliana.

(Picha na Mary Gwera)
 
 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni