Jumanne, 13 Novemba 2018

MAHAKAMA, TPSF KUWA NA JUKWAA LA PAMOJA KUJADILI CHANGAMOTO ZA KIBIASHARA


Na Mary Gwera, Mahakama
Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) imepanga kuwa na Jukwaa la pamoja kujadili masuala ya msingi ya biashara yenye lengo la kukuza uchumi wa Taifa.

Akizungumza na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Juma Novemba 12, Mwenyekiti wa Bodi ya TPSF, Bw. Salum Shamte alimshukuru Mhe. Jaji Mkuu kwa kukubali pendekezo la kuwa na Jukwaa hilo.

“Jukwaa hili ambalo tumependekeza kufanyika mara nne (4) kwa mwaka litasaidia TPSF na Mahakama ya Tanzania kujadili changamoto kwani kuna Mashauri ya Kibiashara ambayo kimsingi yakimalizwa mapema biashara zitaendelea na hatimaye uchumi utakua,” alisema Bw. Shamte. 

Mbali na Jukwaa, Mwenyekiti huyo ambaye aliambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF pamoja na Wajumbe wa Bodi wa Taasisi hiyo ambao walimtembelea Mhe. Jaji Mkuu kwa lengo la kujitambulisha, aligusia pia juu ya ucheleweshaji wa baadhi ya Mashauri ya Kibiashara Mahakamani.

“Napenda kupongeza jitihada zinazofanywa na Mahakama katika kuendelea na maboresho ya huduma zake, hata hivyo napenda kugusia baadhi ya mashauri ya biashara yanayochukua muda mrefu, hivyo Mhe. Jaji Mkuu tunaomba uliangalie hili kwa jicho ya kipekee,” alieleza Mwenyekiti huyo wa TPSF.

Kwa ujumla ujumbe huo uligusia masuala kadhaa yote yakiwa na lengo la kuboresha na kukuza Sekta ya biashara na uwekezaji nchini ambayo Mahakama pia ina mchango katika kufanikisha hili.

Kwa upande wake Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma aliwahakikishia Wajumbe hao juu ya kasi ya maboresho mbalimbali ambayo Mahakama inaendelea kufanya mojawapo ikiwa ni matumizi ya TEHAMA.

“Kwa sasa, Mahakama ya Tanzania ina baadhi ya mifumo mbalimbali inayofanya kazi, kama Mfumo wa Utunzaji Takwimu kwa njia ya Kielektroniki (JSDS), ‘e-filling’ na kadhalika, na mingine hivyo tunahitaji ushirikiano na Wadau katika kuhakikisha kuwa Mahakama inatimiza jukumu lake la utoaji haki,” alieleza Mhe. Jaji Mkuu.

Mhe. Jaji Mkuu alisema Mahakama ya Tanzania ipo tayari kuipitisha TPSF kuhusu mifumo hiyo kuona jinsi gani inafanya kazi.

Aidha; Mhe. Jaji Mkuu aliutoa hofu ujumbe huo juu ya kasi ya Mahakama katika kushughulikia mashauri yanayoletwa Mahakamani huku akieleza juu ya Mikakati ya Mahakama katika kukabiliana na mlundikano wa mashauri  kwa kila ngazi ya Mahakama huku akitoa wito kwa Mawakili na Wadau wengine wa Mahakama kuendana sambasamba na kasi hiyo.

Katika kuhakikisha kuwa Mahakama inafikia malengo ya kumaliza mlundikano imejiwekea mikakati mbalimbali ikiwemo kupanga muda wa kumaliza kesi kwa kila ngazi ya Mahakama.

Kwa upande wa Mahakama za Mwanzo  kesi zisizidi miezi sita (6), Mahakama za Wilaya/Mkoa kesi zisizidi mwaka mmoja na kwa upande wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu kesi zisizidi umri wa miaka miwili (2).

 Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (pichani) akizungumza na Ujumbe kutoka TPSF na Viongozi wa Mahakama (hawapo pichani) ofisini kwake, Mahakama ya Rufani (T) jijini Dar es Salaam.
Wajumbe wakimsikiza Mhe. Jaji Mkuu.
Mwenyekiti wa Bodi ya TPSF, Bw. Salum Shamte (kushoto) akizungumza jambo, kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF, Bw. Godfrey Simbeye.
Sehemu ya Wajumbe wa Kikao wakifuatilia.
Jaji Kiongozi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Feleshi akichangia jambo katika Mazungumzo kati ya Mahakama ya Tanzania na  TPSF. Katikati ni Mtendaji Mkuu, Mahakama ya Tanzania, Mhe. Hussein Kattanga na kushoto ni Msajili Mkuu, Mahakama, Mhe. Katarina Revocati.
Mtendaji Mkuu, Mahakama ya Tanzania, Mhe. Hussein Kattanga akizungumza jambo, kulia kwake ni Msajili Mkuu, Mahakama ya Tanzania, Mhe. Katarina Revocati.
Mtendaji Mkuu, Mahakama ya Tanzania, Mhe. Hussein Kattanga (aliyenyoosha mkono) akiwaonesha Wajumbe kutoka TPSF Bango la Mapambano dhidi ya rushwa lililoandaliwa na Mahakama ya Tanzania ikiwa ni moja mikakati ya Mapambano dhidi ya Rushwa.
Jaji Mkuu wa Tanzania (kushoto) akimkabidhi zawadi ya nakala za vitabu vya Mpango Mkakati wa miaka mitano (5) wa Mahakama ya Tanzania kwa Mwenyekiti wa Bodi ya TPSF, Bw. Salum Shamte.

(Picha na Mary Gwera, Mahakama)
 
 
 
 
 
 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni