Jumanne, 29 Januari 2019

MAJAJI WAPYA WA MAHAKAMA YA RUFANI NA MAHAKAMA KUU WAAPISHWA


Na Magreth Kinabo, Mahakama

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amewataka Majaji wapya aliowaapisha kutenda haki kwa mujibu wa sheria.

Akizungumza katika hafla ya kuwaapisha Majaji hao iliyofanyika Januari 29, Ikulu jijini Dar es Salaam, Mhe. Rais amesema  kazi ya kusimamia haki ni ngumu, hivyo inahitaji kumtanguliza Mwenyezi Mungu.

“Mna jukumu kubwa la kusimamia haki, lakini mkamtangulize Mwenyezi Mungu, mkasimamie haki iliyo ya kweli,” alisema Rais Magufuli.

Kwa upande wake Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amempongeza na kumshukuru Mhe. Rais kwa kufanya uteuzi wenye idadi kubwa ya wanawake.  

Mhe. Samia alisema kwa idadi hiyo ya Majaji wanawake anaamini masuala mbalimbali yaliyokubaliwa katika Mkutano wa Arusha kuhusu Mahakama na Jinsia pamoja na ule wa Zanzibar wa Majaji wanawake yatatekelezwa ipasavyo.

Awali kabla ya kumkaribisha Mhe. Rais, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Profesa Ibrahim Hamis Juma amesema uteuzi wa Majaji wapya umeongeza idadi yao kutoka 66 hadi kufikia 81.  

Ametoa wito kwa Majaji wapya kufanya kazi kwa bidii na unyenyekevu wa hali ya juu huku akiwataka kujali na kulinda afya zao za mwili, akili na roho. Amesisitiza pia juu ya utayari wao wa kufanya kazi kwenye kituo chochote cha kazi watakachopangiwa.

Aidha Mhe. Jaji Mkuu ameonyesha kuwepo kwa hitaji la Majaji wengi Zaidi na kuainisha sababu za hitaji hilo. 

“ Bado upo umuhimu wa Majaji kuongezeka hadi kufikia 100 au150 kwa kuwa uelewa wa haki umeongezeka na wanachi wanaijua haki na wanakwenda Mahakamani na pia ujenzi wa majengo ya Mahakama sehemu mbalimbali za nchi utaleta hitaji la kuwa na Majaji wengi zaidi,” alisema Jaji Mkuu.

Katika hafla hiyo, Rais Magufuli  aliwaapisha Majaji sita wa Mahakama ya Rufani, ambao ni Mhe. Winfrida Korosso, Mhe. Barke Sahel, Mhe. Lugano Mwandambo, Mhe. Dkt. Mary Calorine Levira, Mhe. Ignas Kitusi na Mhe. Rehema Sameji. 

Rais pia amewaapisha Majaji wa Mahakama Kuu, ambao ni Mhe. John Kahyoza , Mhe. Suzan Mkapa, Mhe. Fahamu Mtulya, Mhe Cyprian  Mkeha, Mhe. Wilbard Mashauri, Mhe. Dustan Ndunguru,  Mhe. Seif Kulita,  Mhe. Upendo Madeha.

Wengine ni Mhe. Yohane Masara,  Mhe. Mustapha Ismail, Mhe. Athman  Kirati, Mhe. Zephrine  Galeba, Mhe. Ntemi Kirikamajenga, Mhe. Juliana Masabo na Mhe. Lilian Mongela.

Katika hafla hiyo Majaji wapya, Wakuu wa Wilaya 2 na Wakurugenzi Watendaji wa Wilaya 10 walikula kiapo cha uadilifu  kwa viongozi wa umma.  
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Mhe. Jaji Winifrida Korosso kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, kabla ya uteuzi wake, Mhe. Jaji Korosso alikuwa Jaji Mfawidhi, Mahakama Kuu-Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Mhe. Jaji, Dkt. Mary Caroline Levira kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, kabla ya uteuzi huu Mhe. Jaji, Dkt. Levira alikuwa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Mhe. Ignas Kitusi kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, kabla ya uteuzi huu, Mhe. Jaji Kitusi alikuwa Jaji Mfawidhi, Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma.


Mhe. Rais akimpongeza Mhe. Jaji Kitusi mara baada ya kumuapisha.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Mhe. John Kahyoza kuwa Jaji wa Mahakama Kuu, kabla ya uteuzi wake, Mhe. Kahyoza alikuwa Msajili wa Mahakama ya Rufani (T).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Mhe. Suzan Mkapa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, kabla ya uteuzi wake Mhe. Mkapa alikuwa Naibu Katibu Mkuu Hazina.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Mhe. Upendo Madeha kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, kabla ya uteuzi wake Mhe. Madeha alikuwa Hakimu Mkazi Mfawidhi, Mahakama ya Hakimu Mkazi Shinyanga.

Pichani ni Wahe. Majaji Wateule wakisubiri kuapishwa rasmi.

Baadhi ya Waheshimiwa Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu pamoja na Wageni wengine wakifuatilia sherehe za kuapishwa kwa Wahe. Majaji wapya wa Mahakama hizo. 
 Wahe. Majaji wapya wa Mahakam ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania wakila kiapo cha maadili mara ya kuapishwa.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na Wahe. Majaji pamoja na Viongozi wengine aliowateua, katika hotuba Mhe. Rais amewataka Viongozi hao kufanya kazi kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizopo.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza na Wahe. Majaji wapya walioapishwa, amemshukuru Mhe. Rais kwa uteuzi wa Majaji hao.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wahe. Majaji wapya pamoja na  Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, wa tatu kushoto ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, wa tatu kulia ni Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, wa pili kulia ni Katibu Mkuu Kiongozi, Eng. John Kijazi, wa pili kushoto ni Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi, wa kwanza kushoto ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa ni Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Suleiman Jaffo na wa kwanza kulia ni Jaji Kiongozi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wapya walioapishwa na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watendaji Wakuu wa Mahakama ya Tanzania.

(Picha na Mary Gwera, Mahakama)



 

 


 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni