Alhamisi, 11 Februari 2021

MAAFISA TEHAMA MAHAKAMA WAPONGEZWA KWA KAZI NZURI

Na Ibrahim Mdachi, IJA-Lushoto

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe.Jaji, Dkt. Paul Kihwelo amewapongeza Maafisa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania kuwa sehemu ya ajenda ya kuhakikisha lengo la Mahakama la utoaji wa haki kwa wakati linaendelea kutekelezwa.

Akifungua rasmi Mkutano wa mwaka wa Maafisa hao mapema Februari 8, 2021 Mhe. Jaji Kihwelo alisema kuwa amefurahishwa kuona pamoja na uwepo wa changamoto mbalimbali ikiwemo ya gonjwa la homa ya mapafu unaosababishwa na virusi vya korona (COVID 19)  Mahakama bado imeendelea kutoa huduma zake kwa wananchi.

 “Mahakama ya Tanzania chini ya uongozi thabiti wa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Juma kupitia kurugenzi ya TEHAMA na mikakati mbalimbali iliyopo imeendelea kuwa miongoni mwa Mahakama katika nchi chache zilizoweza kuendelea kutoa huduma zake za kimahakama kwa kuitumia vyema tasnia ya TEHAMA kupitia njia mbalimbali za kimtandao,” alisema Jaji Kihwelo

 Aidha, Mkuu huyo wa Chuo aliwahamasisha maafisa hao kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kuhakikisha wanaweka mazingira mazuri ili kuweza kupambana na changamoto zinazoikumba tasnia ya TEHAMA kwa kuzigeuza kuwa fursa ya kujijenga na kujiimarisha zaidi.

 Mkutano huo wa mwaka unaofanyika katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto unalenga katika kutathmini utekelezaji wa shughuli mbalimbali za TEHAMA mahakamani.

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Jaji Dkt. Paul F. Kihwelo akisisitizia jambo wakati akitoa hotuba yake ya ufunguzi wa Mkutano wa mwaka kwa Maafisa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania kutathmini utekelezaji wa shughuli mbalimbali za TEHAMA.

Mkurugenzi wa TEHAMA, Mahakama ya Tanzania, Bw. Enock Kalege akizungumza na Maafisa TEHAMA wa Mahakama wanaoshiriki katika Mkutano huo.

 Mkurugenzi wa TEHAMA, Mahakama ya Tanzania, Bw. Enock Kalege akitoa neno fupi la ukaribisho kwa mgeni rasmi katika Mkutano wa mwaka kwa Maafisa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania uliofanyika katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto.

Afisa TEHAMA Mwandamizi wa Mahakama ya Tanzania, Bw. Allan Machella akizungumza jambo na Washiriki wa Mkutano huo.

  Meza Kuu katika picha ya pamoja na Maafisa TEHAMA wa Mahakama ya Tanzania mara baada ya kufunguliwa rasmi Mkutano hao Chuoni Lushoto.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni