Jumapili, 14 Machi 2021

MAHAKAMA YAPONGEZWA KWA MATUMIZI MAZURI YA RASILIMALI

 Na Lydia Churi-Mahakama, Njombe, Morogoro

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa matumizi mazuri ya rasilimali yanayodhihirishwa na hali nzuri ya miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama inayoendelea kwenye maeneo mbalimbali nchini.

Wajumbe wa kamati hiyo wametoa pongezi hizo wakati wa ziara yao ya kukagua baadhi ya miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama katika mikoa ya Dodoma, Njombe na Morogoro. Mkoani Dodoma, wajumbe hao walikagua ujenzi wa majengo ya Mahakama ya Mwanzo Kibaigwa, Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe na jengo la Mahakama Kuu Jumuishi kanda ya Morogoro.

“Tunaipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kujenga majengo mazuri katika maeneo mbalimbali nchini, majengo haya ni ya viwango vya nchi ya uchumi wa kati” alisema Makamu Mwenyeikiti wa Kamati hiyo Mhe. Najma Murtaza Giga.

Mhe. Giga alisema ubora wa majengo ya Mahakama unatokana na maono ya mbeleni ambapo jengo la Mahakama ya Mwanzo lililojengwa  linaweza kutumika kutoa huduma za Mahakama ya wilaya pindi eneo husika linapopanda hadhi na kuwa wilaya huku akitolea mfano jengo la Mahakama ya Mwanzo Kibaigwa lililopo kwenye wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma.

Mjumbe mwingine wa Kamati hiyo ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Singida Magharibi Mhe. Elibariki Kingu alisema kamati imeona thamani ya fedha (value for money) katika miradi ya Mahakama ambayo iko katika ubora unaokubalika hasa katika matumizi ya fedha za wananchi.

“Majengo ni mazuri, tunampongeza Waziri wa Katiba na Sheria pamoja na uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kazi nzuri”, alisema huku akiongeza kuwa Mahakama ni Mhimili wa utoaji haki hivyo endapo kuna matumizi mazuri ya fedha za Umma ni kiashiria kuwa hata haki itatendeka ndani ya majengo hayo.

Aidha, wajumbe wa kamati hiyo pia wanatarajiwa kutembelea na kukagua ujenzi wa majengo ya Mahakama Jumuishi (Intergrated Justice Centre) wilayani Temeke jijini Dar es salaam na mkoani Arusha na baadaye kutembelea Mahakama za wilaya za Chemba na Bahi mkoani Dodoma. 

Mahakama ya Tanzania inaendelea na ujenzi wa majengo ya Mahakama katika maeneo mbalimbali nchini yakiwemo majengo sita ya Mahakama Kuu Jumuishi katika miji ya Arusha, Mwanza, Dodoma, Morogoro na Dar es salaam.

Majengo mengine ni ya Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama za wilaya na Mahakama za Mwanzo katika maeneo mbalimbali nchini yakiwemo Lindi, Njombe, Katavi, Sikonge, Bahi, Chemba na Mahakama za Mwanzo kadhaa zikiwemo Kibaigwa-Dodoma, Nyakibimbili-Bukoba, Matili-Songea, na Kimbe-Tanga.

Aidha, Mahakama imekamilisha ujenzi wa majengo mawili ya Mahakama Kuu katika mikoa ya Kigoma na Mara, Mahakama za Hakimu Mkazi katika mikoa ya Simiyu, Geita, Pwani pamoja na Mahakama za wilaya zaidi ya 16 katika maeneo mbalimbali nchini. 

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wakiingia kwenye jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe kwa ajili ya kukagua. Aliyewaongoza wajumbe hao ni Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba. Kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Najma Martaza Giga.
Jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe likiwa katika hatua za mwisho za ukamilishwaji wake.
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kukagua jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe. 


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba akieleza jambo kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria walipotembelea jengo la Mahakama Kuu Jumuishi leo mkoani Morogoro. 

Mbunge wa jimbo la Singida Magharibi Mhe. Elibariki Kingu akifafanua jambo kwa Wajumbe wenzake wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria walipotembelea jengo la Mahakama Kuu Jumuishi Morogoro linaloendelea kujengwa. Kushoto ni Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji wa Mahakama ya Tanzania Bw. Erasto Uisso. 
Mwanasheria Mkuu wa Serikali Prof. Adelardus Kilangi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba. Wa tatu kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa wizara ya Katiba na Sheria Bw. Amon Mpanju.  
Baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba wakiwa na Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (wa tano kushoto).
 Jengo la Mahakama Kuu Jumuishi lililopo Morogoro linalotarajiwa kukamilika hivi karibuni
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kukagua jengo hilo.   

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni