Ijumaa, 30 Aprili 2021

WADAU WA HAKI JINAI WATAKIWA KUTOA USHIRIKIANO ILI HAKI IWEZE KUTENDEKA – JAJI KIONGOZI

Na Innocent Kansha – Mahakama Makete.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania ametoa rai kwa wadau wote wa Mahakama hususani wa haki Jinai kujipanga vizuri na kutekeleza wajibu wao wa kisheria kuwahudumia wahalifu ili kuisaidia Mahakama kuweza kutoa haki kwa wakati na kwa wote.

Akizindua rasmi Jengo la Mahakama ya Wilaya Makete mkoani Njombe mnamo Aprili 28, 2021 Mhe. Dkt. Feleshi alisema kila linapoanzishwa eneo la kiutawala kwa mujibu wa sheria Mahakama ya Wilaya inapaswa kuwepo na kutoa huduma kwa wananchi, hivyo ni wito wa Mahakama kwa wadau wake kama vile Ofisi ya Mwendesha Mashitaka, Polisi na Magereza kuhakikisha wanatoa ushirikiano wa hali na mali ili haki ionekane ikitendeka kwa wananchi.

“linapokuja swala la haki jinai popote utakapopeleka huduma ni lazima Magereza, Ofisi ya Mwendesha Mashitaka pamoja na Polisi wawe wamejipanga kuwaleta wahalifu au kuwachukua na kuwapeleka kule ambako wanatakiwa kuhifadhiwa kwa mujibu wa taratibu”, aliongeza Jaji Kiongozi.

Jaji Kiongozi alisema yote hayo yatawezekana kwa kuzingatia misingi ya haki bila kushadadia na kutoruhusu matumizi mabaya ya sheria kama vile kunyima watu dhamana kwa makosa yanayo dhaminika au kutoa mashariti magumu ya dhamana. Lengo la Mahakama ni kuona kwamba mtu kuwa na kesi kusiathiri shughuli zake za kiuchumi lakini vilevile shughuli za kifamilia na mahusiano yake katika kijamii inayomzunguka.

Niwakumbushe watumishi wa Mahakama kutunza jengo hilo zuri na la kisasa, na kuendelea kuboresha huduma zenu kwa wateja na wadau wote watakao pata huduma hapa, pamoja na haya yote Mahakama imeazimia kusimamia maadili ya watumishi wa Mahakama kwani ni ukweli usiopingika kwamba mafanikio ya Taasisi hutokana na watumishi wachapakazi na wenye maadili, alisisitiza Jaji Kiongozi.

Mhe. Dkt. Feleshi aliwahakikishia wananchi na wadau wa Mahakama kwamba, Mahakama inao mfumo mzuri na mathubuti wa kushughulikia kero na malalamiko kwa mfano kila Mahakama ina rejista maalumu ya kupokelea malalamiko pia Viongozi wa Mahakama wenye dhamana hiyo kama Mahakimu Wakazi Wafawidhi, Maafisa Utumishi na Tawala na Watendaji.

Aidha, Jaji Kiongozi alisema kwa mtu yeyote ambaye hawezi kuwasilisha lalamiko lake moja kwa moja mahakamani, Mahakama ipo wazi kupimwa na kuchunguzwa na vyombo vingine, kwahiyo Mahakama inasisitiza kwamba iwapo kuna vitendo visivyofaa vinavyofanywa na watumishi vinaweza kuwasilishwa Takukuru na kwenye Mamlaka zingine za kiuchunguzi ili vikibainika hatua zichukuliwa dhidi ya vitendo hivyo.

“Ni imani yangu pia kuwa Wananchi na wadau wetu wa Mahakama watapata mahitaji yao ya msingi kwenye mazingira bora kabisa wakati mashauri yao yanasikilizwa na hata pale watakapokuwa wanasubiri kupata huduma”, alibainisha Jaji Kiongozi.

 

Majengo haya ya kisasa yapo kwa sababu moja kubwa ya kuwarahisishia wananchi kupata huduma. Tunawahakikishia kwamba tutaendelea kuwatendea haki wananchi ili maana halisi ya umuhimu wa majengo haya ionekane kwa wananchi wetu tunaowahudumia, alisistiza Jaji Kiongozi.

 

Wakati huo huo, Mkuu wa Wilaya ya Makete Bi. Veronica Kessy alisema watumishi watao bahatika kufanya kazi kwenye jengo hilo watakuwa wamefarijika na kufanya kazi kwa utulivu lakini pia hata wananchi wataofika kupata huduma hapa wataamini kweli Serikali ipo

 

“Serikali ya Wilaya imefarijika sana kushiliki kwenye uzinduzi wa jengo hili na mara kwa mara tulikuwa tunafika kuona namna ujenzi ulivyokuwa ukiendelea tukihakikisha kwamba thamani ya jengo hili inaendena na kiwango cha pesa halisi, hii yote ilikuwa ni kuhakikisha kwamba hakuna fedha ya serikali inayokwenda kupote kwani ni kodi ya wananchi”, alisema Mkuu wa Wilaya.

 

Naye, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa Mhe. Pentelni Mlisa Kente alisema anapenda kumshukuru Mkuu wa Wilaya na Kamati yake ya Ulinzi na Usalama, hii ni kutona na kwamba ukilinganisha Wilaya za Wanging’ombe na Njombe takwimu zinaonyesha kuwa matukio ya mauaji na ubakaji ni machache sana kwa yale yanayotufikia Mahakama Kuu.

 

“Uwepo wa jengo hili la kisasa sio kwamba Mahakama imejiandaa ili wananchi wengi waje washitakiwe hapa la hasha hata kama hapatakuwepo na kesi nyingi Mahakimu wetu hawata lala tutashirikiana na wanasheria wa halmashauri na viongozi wengine hata kutoa elimu kwa wananchi kwani kutoa elimu ya kisheria ni moja ya kazi yetu”, aliongeza Jaji Mfawidhi.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya Makete mkoani Njombe Wengine ni Mkuu wa Wilaya ya Makete Bi. Veronica Kessy (wa kwanza kushoto), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa Mhe. Pentelni Mlisa Kente (wa tatu kulia) pamoja na viongozi waandamizi wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa.


Muonekano wa Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Makete lililozinduliwa rasmi na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi  Aprili 28,2021.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akifunua kitambaa kuashiria uzinduzi rasmi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya Makete mkoani Njombe Wengine ni Mkuu wa Wilaya ya Makete Bi. Veronica Kessy (wa kwanza kushoto).


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akipanda mti  kuashiria uzinduzi rasmi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya Makete mkoani Njombe

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi akifafanua jambo mbele ya wageni waalikwa na wananchi (hawapo pichani) waliohudhulia uzinduzi rasmi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya Makete mkoani Njombe

Baadhi ya wananchi na watumishi wa Mahakama waliohudhuria wakifuatilia hotuba ya Mgeni Rasmi (hayupo pichani) wakati wa uzinduzi rasmi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya Makete. 


Meza Kuu wakiwa kwenye picha ya pamoja na makundi ya Wachungaji na watumishi wa Mahakama walishiriki hafla ya uzinduzi rasmi wa Jengo la Mahakama ya Wilaya ya Makete.

Picha na  Innocent Kansha - Mahakama 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni