Jumatano, 14 Aprili 2021

WADAU WAOMBWA KUUNGANA NA MAHAKAMA KATIKA MATUMIZI YA TEKNOLOJIA

 Na Lydia Churi-Mahakama- Kilimanjaro

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewaomba wadau wa Mahakama kuungana na Mhimili huo katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kusogeza haki karibu zaidi na wananchi.

Akizungumza katika mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na wadau wa Mahakama mkoani Kilimanjaro, Jaji Mkuu wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume hiyo aliwaambia wadau hao kuwa Mahakama tayari imeshaingia kwenye matumizi ya Tehama na mfumo hauwezi kukamilika endapo wadau wake watakuwa nje ya mfumo huo.

“Mahakama na wadau, wote wanao wajibu wa kutoa haki kwa wakati, wadau ni sehemu ya mnyororo wa utoaji haki hivyo kukiwa na dosari yoyote katika mnyororo huo, haki haiwezi kupatikana kwa wakati”, alisema Jaji Mkuu.

Alisema endapo wadau wa Mahakama watawekeza kwenye matumizi ya Tehama, wajibu wa utoaji haki utakuwa bora Zaidi. Akitolea mfano wa janga la ugonjwa wa COVID 19, Jaji Mkuu alisema Mahakama ilifunga vifaa vya Tehama kwenye Magereza mbalimbali nchini hatua iliyowezesha mashauri mengi Zaidi kusikilizwa.

Alisema uzoefu uliotokana na janga la COVID unaonesha ni kwa kiasi gani Teknolojia inaweza kusaidia kurahisisha shughuli za utoaji haki. Aliongeza kuwa kwa mujibu wa wataalam, dunia inaweza kukumbwa na majanga mengine, ugonjwa wa COVID si janga la mwisho kuikumba dunia na changamoto ni kwa namna gani Mahakama na wadau wanaweza kutumia Tehama kuwavusha katika majanga mbalimbali yanayoweza kutokea.

“Teknolojia inasogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi na wananchi bila ya kutegemea majengo peke yake, katika karne hii ya 21 haki haitegemei majengo, mwananchi anaweza kupata taarifa kupitia simu yake ya mkononi, hana ulazima wa kufika mahakamani”, Jaji Mkuu alisisitiza matumizi ya Tehama.

Aidha, Jaji Mkuu pia ametoa rai kwa wadau hao kuwa mstari wa mbele katika kuzibadilisha sheria zilizopitwa na wakati ili ziendane na hali ya sasa kwani kwa kufanya hivyo wataisaidia jamii kuifikia haki kwa wakati.

“Sheria zetu zilitungwa katika maudhui ya karne ya 20, dunia ya wakati huo ilikuwa ni dunia ya karne ya 20 hivyo wadau tujisomee, tubadilike na tuangalie sheria zetu zinazohitaji kufanyiwa marekebisho”, alisema.

Wakati huo huo, Jaji Mkuu amewataka wadau wa Mahakama kuongeza matumizi ya vipimo vya vinasaba (DNA) ili kupunguza malalamiko yanayotokana na mashauri ya ubakaji. Amewataka wapelelezi kutokutumia nguvu katika kukusanya Ushahidi badala yake watumie sayansi na teknolojia.

Jaji Mkuu alisema Sheria imeruhusu matumizi ya kipmo hicho muda mrefu sasa lakini hakifanyiki. “Ni nadra sana DNA kuchukuliwa wakati wa tukio”, alisema.

Kuhusu matumizi ya Video katika kukusanya Ushahidi, Prof. Juma alisema sheria ilishabadilishwa kuruhusu mahojiano ya mtuhumiwa na polisi kwa njia ya video ili kuondokana na malalamiko ya kubambikiziwa kesi. Alisema sheria iko mbele lakini taratibu bado ni zile zile za zamani hivyo amewataka wadau kuliangalia suala hilo kwa mapana yake.  

Tume ya Utumishi wa Mahakama inafanya ziara katika Mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara kwa lengo la kuitangaza na kutoa elimu kwa wadau wa Mahakama wakiwemo wajumbe wa kamati za Maadili za Mikoa na Wilaya ambao ni wakuu wa Mikoa na wakuu wa Wilaya.

Tume ya Utumishi ya Mahakama imeundwa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 113 kwa lengo la kusimamia mambo muhimu yanayohusu Mhimili wa Mahakama. Wajumbe wa Tume hiyo ni pamoja na Jaji Mkuu wa Tanzania (Mwenyekiti), Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji moja wa Mahakama ya Rufani anayeteuliwa na Rais, Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, na wajumbe wengine wawili wanaoteuliwa na Rais.

 Baadhi ya kazi za Tume hiyo ni pamoja na kumshauri Mhe. Rais katika uteuzi wa Majaji wa Mahakama Kuu, kumshauri Rais kuhusu masuala ya nidhamu, mishahara na maslahi ya Majaji, na kushauri kuhusu ajira za Mahakimu na kusimamia nidhamu yao.

Wadau wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye mkutano kati yao na Tume ya Utumishi wa Mahakama mkoani Kilimanjaro. Mkutano huo unalenga kuwakutanisha wadau na Mahakama ili kubadilishana uzoefu, kuitangaza Tume hiyo na kujadili changamoto mbalimbali za utoaji Haki nchini. 
Baadhi ya watumishi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na wadau wa Mahakama mkoani Kilimanjaro. Mkutano huo unalenga kuwakutanisha wadau na Mahakama ili kubadilishana uzoefu, kuitangaza Tume hiyo na kujadili changamoto mbalimbali za utoaji Haki nchini. 
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo jana mjini Moshi.
Wadau wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kwenye mkutano kati yao na Tume ya Utumishi wa Mahakama mkoani Kilimanjaro. 

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Mhe. Anna Mughwira akiwa kwenye Mkutano wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na Wadau wa Mahakama mkoani Kilimanjaro. Mkutano huo unalenga kuwakutanisha wadau na Mahakama ili kubadilishana uzoefu, kuitangaza Tume hiyo na kujadili changamoto mbalimbali za utoaji Haki nchini. Kulia ni Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni