Jumanne, 27 Septemba 2022

WATUMISHI KITUO JUMUISHI MOROGORO WAPATA ELIMU YA ZIMAMOTO NA UOKOAJI

Na Evelina Odemba-Morogoro

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani hapa limeendesha mafunzo ya kukabiliana na majanga ya moto kwa watumishi wa Mahakama katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro ili kuweza kujiokoa wao wenye pamoja na mali zingine.

Mafunzo hayo yalioandaliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe yalishirikisha wadau wengine wa Mahakama, ikiwemo jeshi la Polisi, Magereza, Mawakili wa Kujitegeme na Makampuni ya Usafi na Ulinzi yanayohudumu katika Kituo hicho.

Akifungua mafunzo hayo yalitofanyika hivi karibuni, Mhe Ngwembe alisema wanataka kuhakikisha watumishi wote wa Mahakama na watendaji wengine wanakuwa na uelewa wa kuweza kujikoa. Alisema Serikali imetumia fedha nyingi katika ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki, hivyo ni jukumu lao kuhakikisha wanavitunza na kuvilinda na majanga ya moto.

Naye Mkaguzi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Emmanuel Ocheng, ambaye alimwakilisha Kamanda wa Jeshi hilo mkoani Morogoro aliupongeza uongozi wa Mahakama kwa kuja na wazo hilo la kutoa mafunzo hayo kwa watendaji wake.

Sanjari na hilo, Mkaguzi Ocheng alisema jengo hilo la Kituo Jumuishi limekuwa mfano wa kuigwa kwa majengo yote ndani ya mkoa wa Morogoro kutokana na kuwa miundombinu yote muhimu ya kupambana na moto. Alisema Jeshi hilo litaendelea kushirikiana na Mahakama hiyo katika kutoa elimu ya uzimaji moto kwa wananchi kutokana na nafasi watakayopatiwa.

Ameishauri jamii kupitisha michoro ya nyumba zao kwa jeshi hilo kabla ya kuanza ujenzi ili kusaidia kuweka sahihi miundombinu ya uzimaji moto ili kujiepusha na majanga hayo. Mkaguzi Ocheng alitumia fursa hiyo kuwaomba watendaji wa Kituo Jumuishi kukagua mara kwa mara vifaa vyao vya kuzimia moto katika magari yao.

Mafunzo hayo ya siku moja yametoa fursa kwa watumishi wa Mahakama na watendaji wengine kujifunza aina za moto, vifaa vya kuzimia na jinsi ya kuvitumia. Watendaji hao walionyesha kuridhika na kufurahia elimu hiyo tofauti na hapo awali walivyokuwa wakielewa suala hilo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe akifanya zoezi la kuzima moto kwa vitendo wakati wa mafunzo hayo.
 Mkaguzi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Emmanuel Ocheng (picha juu) akitoa maelezo namna ya kushika kizimamoto huku watumishi wa Mahakama katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro pamoja na wadau wa Mahakama (picha chini) wakifuatilia elimu inayotolewa juu ya namna ya kukabiliana na majanga ya moto.

Mtumishi wa Mahakama, Bi. Shany Kapinga akifanya kwa vitendo zoezi la uzimaji moto. Pembeni ni watumishi pamoja na wadau wakishuhudia namna moto unavyozimwa.


Mwonekano wa mbele wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Morogoro.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni