Jumanne, 18 Julai 2023

MAKUBALIANO UPATIKANAJI MAAMUZI, SHERIA KIDIJITALI YASAINIWA

 Na Arapha Rusheke-Mahakama Kuu, Dodoma

Tume ya Kurekebisha Sheria na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali wamesaini makubaliano na Taasisi ya Habari za Kisheria Afrika, the African Legal Information Insitute (AfricanLII), kuhusu ushirikiano kwenye masuala ya upatikanaji kwa urahisi wa nyaraka za kisheria kwa njia ya kidijitali, ikiwemo maamuzi ya Mahakama na Sheria mbalimbali.

Katibu wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Bw. Grifin Mwakapeje na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dkt. Evaristo Longopa ndiyo waliotia saini makubaliano hayo kwa upande wa taasisi za Tanzania, huku Mwakilishi AfricanLii, Bw. Greg Kempe akisaini kwa niaba ya taasisi yake. Katika hafla hiyo, Mahakama ilishiriki kama mdau na mzoefu katika eneo hilo.

Hafla ya utiaji saini wa makubaliano hayo ilifanyika hivi karibuni jijini hapa siku ya kwanza ya warsha ya siku mbili kuhusu utoaji na upatikanaji endelevu wa sheria kwa njia ya kidijitali. Warsha hiyo ilifunguliwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damasi Ndumbaro.

Akizungumza wakati anafungua warsha baada tukio hilo, Mhe. Dkt. Ndumbaro alisema utiaji saini wa makubaliano hayo utahakikisha sheria zote za Tanzania zinazotungwa na Bunge na sheria ndogo zinapatikana kwenye mifumo ya kidijitali.

“Mradi huu pia utasaidia wananchi na taasisi za Serikali ambazo zinatumia Sheria mbalimbali kuweza kuzipata kiurahisi, tunatumia mapinduzi ya teknolojia kuhakikisha tunapeleka haki kirahisi na kwa wepesi kwa kila Mtanzania,” alisema Waziri wa Sheria na Katiba.

Warsha hiyo ya siku mbili iliandaliwa na GIZ, AfricanLii na Laws Africa na washiriki wake ni Mahakama ya Tanzania, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Seriali Tume ya Kurekebisha Sheria, Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Ofisi ya Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali na Wizara ya Katiba na Sheria.

AfricanLII na Laws Africa zimekuwa zikisaidia upatikanaji wa maamuzi na Sheria nchini Tanzania kupitia Mfumo wa Taarifa za Maamuzi na Sheria wa TanzLII (www.tanzlii.org) tangu 2018.

Mfumo huo wa TanzLII umesaidia kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa maamuzi na Sheria na kuwa ni mfano wa mifumo bora ya kisheria barani Afrika na Duniani. AfricanLII na Laws Africa wamependekeza ushirikiano wa taasisi mbalimbali katika kutunza Sheria na maamuzi ya Mahakama katika mfumo huo kwa pamoja.

Katibu wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Bw. Grifin Mwakapeje (kulia) na Mwakilishi AfricanLii, Bw. Greg Kempe wakisaini mkataba huo.

Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dkt. Evaristi Longopa (kulia) na Mwakilishi AfricanLii, Bw. Greg Kempe wakionyesha mkataba huo.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (aliyesimama)akieleza jambo wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji AfricanLII, Bi.Mariya Badeva-Bright akisikiliza maoni kutoka kwa wadau katika warsha hiyo.
Mwakilishi kutoka ofisi ya mpiga chapa akichangia mada katika warsha hiyo.
Wadau mbalimbali waliohudhuria warsha hiyo wakifuatilia kwa makini mada mbalimbali zilizokuwa zinatolewa.
Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa katiba na Sheria, Mhe Dkt. Damasi Ndumbaro (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria warsha hiyo.
Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa katiba na Sheria, Mhe Dkt. Damasi Ndumbaro (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Meza Kuu ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe Dkt. Damasi Ndumbaro (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na sekretarieti ambayo imeandaa warsha hiyo.

(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni