Alhamisi, 18 Aprili 2024

MSAJILI MKUU AOMBA USHIRIKIANO KWA VIONGOZI NA WATUMISHI

Na Innocent Kansha- Mahakama

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya amemshukuru mtangulizi wake Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Wilbert Chuma kwa nasaa nzuri alizompatia ambazo zitamsaidia kumjenga akiwa anatekeleza jukumu la kuhudumia nafasi ya Msajili Mkuu na kuomba apewe ushirikiano kutoka kwa viongozi na watumishi wote wa Mahakama ya Tanzania.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhiwa Ofisi ya Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 18 Aprili, 2024 jijini Dar es salaam, Mhe Nkya amesema umuhimu na majukumu ya ofisi ya Msajili Mkuu ni kuratibu na kuongoza shughuli zote za uendeshaji wa mashauri kwani ndiyo jukumu mama la Taasisi.

“Niahidi nitatekeleza majukumu yangu ya Msajili Mkuu kulingana na kiapo changu nilichoapa mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan mnamo tarehe 4 Aprili, 2024, lakini vilevile kwa kutumia uwezo alionijalia Mwenyezi Mungu kadri nitavyoweza nitajitahidi kutumia maarifa yangu na weledi wangu na kushirikiana na viongozi wengine wa Mahakama kuhakikisha Ofisi ya Msajili Mkuu inatekeleza majukumu yake ipasavyokwa,” amesema Mhe. Nkya

Mhe. Nkya alimshukuru mtangulizi wake Jaji Chuma kwa jitihada kubwa alizozifanya kwani katika kipindi chake cha kuhudumu kama Msajili Mkuu mambo mengi sana yamefanyika na pia kuna mambo mengi sana ambayo yataendelea kufanyika ambayo ni takribani mambo 43 yaliyowasilishwa kwenye ripoti ya makabidhiano.

“Wakati Jaji Chuma anatoa hotuba yake nilichukua tu mambo nane kumbe alitaja haraka haraka lakini mzigo niliokuwa nao mbele yangu kwa kweli ni mzigo mkubwa kwa hiyo nitaomba ushirikiano katika kutimiza majukumu ya Ofisi ya Msajili Mkuu,” ameongeza Mhe. Nkya.

Mhe. Nkya ameishukuru Tume ya Mahakama ya Tanzania inayoongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma kwa kupendekeza jina lake kwa Mhe. Rais ili ateuliwe kuwa Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania.

Naye, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel kwa niaba ya Mahakama amemshukuru Jaji Chuma kwa kutenga muda na kupangua ratiba zake kwa ajili ya kuja kushiriki hafla hiyo muhimu ya makabidhiano ya Ofisi ya Msajili Mkuu wa Mahakama.

“Napenda kukushukuru wewe binafsi kwa kunipa ushirikiano wa hali ya juu kwani wakati naapishwa kuwa Mtendaji Mkuu wa Mahakama tarehe 21 Agosti 2021 ulinipokea na kunisaidia kujua shughuli za Mahakama kwa haraka zaidi,”ameongeza Prof. Ole Gabriel.

Mtendaji Mkuu amesema Jaji Chuma alitoa ushirikiano wa kipekee katika eneo la kuimarisha mahusiano kati ya watumishi wa kimahakama na wele wasio wa kimahakama ‘Judicial Officers & Non-Judicial Officers’, hilo lilikuwa jambo kubwa lililomsaidia Mtendaji Mkuu kutekeleza majukumu yake kwa urahisi zaidi.

“Tayari tumeshateta na Msajili Mkuu mpya ili tuendeleze morali hiyo kwani ni jambo ambalo ni la msingi sana katika utendaji wa Taasisi ya Mahakama inayotoa huduma ya haki kwa wananchi,” ameongeza Prof. Ole Gabriel.

Aidha, Prof. Ole Gabriel amemuhakikishia Msajili Mkuu Mpya kuendelea kumpa ushirikiano wa kutosha kama ambavyo alikuwa akifanya kwa mtangulizi wake, Ofisi ya Mtendaji Mkuu ambaye pia ni Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama itakupa ushirikiano wa kutosha kutenda kazi zako za kila siku kwani sisi sote tunajenga nyumba moja na hatuna haja ya kugombania fito.

“Nichukue nafasi hii kipekee nimshukuru Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha Mhe. Sylvester Kainda aliyekaimu shughuli za ofisi ya Msajili Mkuu kwa kipindi chote hicho alinipa ushirikiano wa hali ya juu na kutenda kazi za Mahakama kama ilivyokusudiwa,” amesema Mtendaji Mkuu.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania mara baada ya hafla fupi ya kukabidhiwa ofisi ya Msajili Mkuu, (wa pili kulia) ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza Mhe. Wilbert Chuma, (wa pili kushoto) ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho Mhe. Dkt. Angelo Rumisha, (wa kwanza kulia) ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha Mhe. Sylvester Kainda na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (wa kwanza kushoto).
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (katikati waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza Mhe. Wilbert Chuma, (wa kwanza kushoto) na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (wa kwanza kulia).

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (katikati waliokaa) akizungumza na watanzania kupitia vyombo vya habari wakati wa hafla ya kukabidhiwa Ofisi ya Msajili Mkuu jijini Dar es salaama.



Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza Mhe. Wilbert Chuma (wa kwanza kulia) akimkabidhi nyenzo za vitendea kazi Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Nkya (wa kwanza kushoto) akishudia tukio hilo ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (mwenye miwani).


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza Mhe. Wilbert Chuma (katikati aliyekaa katikati) akizungumza na watanzania kupitia vyombo vya habari wakati wa hafla ya kukabidhi Ofisi ya Msajili Mkuu jijini Dar es salaama.

(Picha na Innocent Kansha- Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni