Alhamisi, 19 Septemba 2024

JAJI EBRAHIM AFUNGA MAFUNZO YA WAKUFUNZI UTATUZI WA MIGOGORO YA UCHAGUZI

Na Innocent Kansha- Mahakama

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe. Rose Ally Ebrahim amewakumbusha Majaji na Mahakimu waliopata mafunzo ya Wakufunzi ya namna bora ya utatuzi wa migogoro ya uchaguzi ‘Election Dispute Resolution’ kutoa elimu hiyo kwa Maafisa wengine kwa kuzingatia ujuzi na weledi walioupata ili kupata mwongozo na maarifa ya pamoja wakati wa utatuzi wa migogoro hiyo.

Mhe. Ebrahim ametoa wito huo leo tarehe 19 Septemba, 2024 jijini Dar es salaam alipokuwa anafunga mafunzo hayo ya siku tatu yenye lengo la kuwaandaa Majaji na Mahakimu kuongeza weledi wa namna bora ya utatuzi wa migogoro ya uchaguzi yaliyoendeshwa jijini Dar es salaam kwa ufadhili wa Taasisi ya Kimataifa Inayoshughulika na Mifumo ya Uchaguzi (IFES) na kuendeshwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama – Lushoto (IJA).

Mhe. Ebrahim amesema mafunzo hayo siyo tu yametoa fursa ya elimu ya namna bora ya kutatua migogoro ya uchaguzi bali yamewawezesha kujenga uwezo wa namna bora ya kuwaelimisha Maafisa Mahakama wengine ambao hawakupata fursa ya kushiriki mafunzo hayo.

“Mafunzo haya ya Wakufunzi yameongeza chachu ya kuhakikisha ujuzi huu unawafikia wengine kwa usahihi na ufanisi mkubwa ili kila Afisa Mahakama atende yale yanayopaswa kutimizwa wakati wa utatuzi wa migogoro ya uchaguzi kwa weledi mkubwa. Hivyo basi wale wote tuliopata mafunzo haya tuna jukumu la kuhakikisha tunawafundisha wenzetu ambao hawakushiriki mafunzo hayo moja kwa moja,” amesema Jaji Ebrahim.

Aidha, Mhe. Ebrahim amesema mafunzo hayo yamejenga msingi wa uelewa wa pamoja wa namna bora ya kuendesha na kutatua migogoro ya uchaguzi katika viwango vinavyokubalika kisheria kwa kuzingatia msingi wa haki, ufanisi na uwazi katika kila mamlaka za kimahakama wakati wa kutatua migogoro hiyo.

“Mashauri yatokanayo na migogoro ya uchaguzi yana changamoto nyingi na ni nyeti huku yakivuta hisia za watu wengi hasa katika nchi zinazozingatia mifumo ya kidemokrasia. Kupitia mafunzo haya ya Wakufunzi wa utatuzi wa migogoro ya uchaguzi yametuongeza ujuzi na shime ya uelewa wa namna bora ya utatuzi wa migogoro ikiwa ni sehemu pia ya namna ya kuelimisha maafisa Mahakama wenzetu mbinu hizi za kiufundi tulizofundishwa,” amesisitiza Mhe. Jaji Ebrahim

Mhe. Ebrahim ameongeza kuwa, kupita mafunzo yamewakumbusha mambo ya msingi ikiwemo kusimamia uhuru wa Mahakama, kufanya maamuzi bila upendelelo ikizingatiwa kwamba haki wakati wote ndiyo itasimamia utatuzi wa migogoro ya uchaguzi.

Kwa upande wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Salma Mussa Maghimbi akitoa neno la shukurani kwa niaba ya washiriki wa mafunzo ya wakufunzi ya namna bora ya utatuzi wa migogoro ya uchaguzi amesema kipindi cha siku tatu za mafunzo hayo ni muhimu sana kwa Mahakama katika jitihada za kustawisha maendeleo ya utoaji haki nchini.

“Tunatambua kwamba ili nchi yoyote iweze kuendelea inahitaji serikali imara inayotokana na uchaguzi huru na wa haki, kwa kipindi cha mafunzo haya tumejifunza mambo mengi ya muhimu yatayokuwa ya msingi kwa Mahakama kama chombo huru kisichokuwa na upande wakati wa utatuzi wa migogoro ya uchaguzi,” amesema Jaji Maghimbi.

Mhe. Maghimbi amesema mafunzo hayo yameibua mambo ya msingi ya kuyazingatia wakati wa utatauzi wa migogoro ya uchaguzi ikiwemo suala la muda, kutambua sheria zinazohusika na namna bora ya kuzitumia kabla ya uchaguzi, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi, pia kutambua aina ya migogoro ya uchaguzi kama ina asili ya jinai ama madai.

Mafunzo hayo ya wakufunzi wa utatuzi wa migogoro ya uchaguzi yaliwajumuisha jumla ya washiriki 32 wakiwemo Majaji, Naibu wasajili, Mahakimu Wakazi wa mikoa na Wilaya nchini.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe. Rose Ally Ebrahim akitoa nasaha kwa washiriki (hawapo pichani) wakati wa kufunga rasmi Mafunzo ya siku tatu kwa Wakufunzi wa utatuzi wa migogoro ya uchaguzi leo tarehe 19 Septemba, 2024 jijini Dar es salaam.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara Mhe. Rose Ally Ebrahim akifafanua jambo kwa washiriki wakati wa kufunga rasmi Mafunzo ya siku tatu kwa Wakufunzi wa utatuzi wa migogoro ya uchaguzi leo tarehe 19 Septemba, 2024 jijini Dar es salaam.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Salma Mussa Maghimbi akitoa neno la shukurani kwa niaba ya washiriki wa mafunzo ya wakufunzi ya namna bora ya utatuzi wa migogoro ya uchaguzi

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es salaam Mhe. Salma Mussa Maghimbi akitoa neno la shukurani kwa niaba ya washiriki wa mafunzo ya wakufunzi ya namna bora ya utatuzi wa migogoro ya uchaguzi.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Kimataifa Inayoshughulika na Mifumo ya Uchaguzi (IFES) nchini Tanzania Bw. Lamin Lighe akitoa neno kwa washiriki wa mafunzo hayo yaliyohitimishwa leo jijini Dar es salaam. 

Mkurugenzi wa Taasisi ya Kimataifa Inayoshughulika na Mifumo ya Uchaguzi (IFES) nchini Tanzania Bw. Lamin Lighe akisisitiza jambo kwa washiriki wa mafunzo hayo yaliyohitimishwa leo jijini Dar es salaam. 

Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya wakufunzi wa namna bora ya utatuzi wa migogoro ya uchaguzi wakifuatilia hotuba ya kufunga mafunzo hayo.




Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya wakufunzi wa namna bora ya utatuzi wa migogoro ya uchaguzi wakifuatilia hotuba ya kufunga mafunzo hayo.


Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya wakufunzi wa namna bora ya utatuzi wa migogoro ya uchaguzi wakifuatilia hotuba ya kufunga mafunzo hayo.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni