Jumapili, 6 Aprili 2025

JAJI MFAWIDHI BUKOBA AONGOZA BARAZA LA WAFANYAKAZI LA KANDA HIYO

Na AHMED MBILINYI, Mahakama-Bukoba

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Bukoba, Mhe. Immakulata Banzi hivi karibuni aliongoza Kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Kanda kujadili mambo mbalimbali ya kiutendaji na utumishi.

Akiwakaribisha wajumbe katika kikao hicho, Mhe. Banzi aliwaomba kuwa huru kuchangia na kutoa maoni mazuri yatakayolisaidia Baraza hilo kufikia maazimio yenye tija siyo tu watumishi wa Kanda hiyo bali pia wafanyakazi wa Mahakama ya Tanzania kwa ujumla.

“Niwashukuru wajumbe kwa kuhudhuria kwenye Kikao cha Baraza hili, ushiriki wenu ni muhimu sana kwani michango ya mawazo mtakayotoa itasaidia kufikia maazimio yenye tija yatakayopelekwa kwenye Baraza Kuu siyo kwa manufaa yetu sisi bali pia watumishi wa Mahakama kwa ujumla,” alisema Mhe. Banzi.

Wakati wa Baraza hilo, wajumbe walijadili masuala mbalimbali yakiwemo mapitio ya bajeti, ukomo wa bajeti, utekelezaji wa bajeti, changamoto za utekelezaji wa bajeti, kupokea na kujadili hoja za watumishi na pia majibu na ufafanuzi ulitolewa na viongozi mbalimbali.

Kadhalika Mhe. Banzi alisisitiza kwa watumishi wote kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu, ushirikiano kwa watumishi na wadau wa mahakama, na   kuwakumbusha kujiendeleza kielimu katika taaluma zao pamoja na matumizi ya TEHAMA.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Viongozi Waandamizi wa Mahakama hiyo akiwemo, Naibu Msajili Mahakama Kanda ya Bukoba, Mhe. Saidi Mkasiwa, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba, Bw. Lothan Simkoko, wajumbe kutoka wilaya zote za Mkoa wa Kagera.

Wajumbe wengine ni Katibu wa TUGHE wa Mkoa wa Kagera, Bw.  Edward Mwashitanda aliyeelezea faida za kutumia Mabaraza ya Wafanyakazi katika kutatua changamoto za watumishi.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Bukoba, Mhe. Immaculata Banzi (katikati) akiongoza Kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Kanda hiyo kilichofanyika tarehe 04 Aprili, 2025. Kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi, Bw. Lucas Mwilu na kushoto ni Katibu wa Baraza la Wafanyakazi Bukoba, Bi. Febronia Serapion.

Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Bukoba, Bw. Lothan Simkoko akiwasilisha taarifa ya Utendaji kazi wa Mahakama Kanda ya Bukoba ya mwaka wa fedha 2024/2025.

Kaimu Afisa Bajeti wa Mahakama Kanda ya Bukoba, Bw. Rojas Rwanyumba akiwasilisha Taarifa ya Bajeti ya Mahakama Kanda ya Bukoba 2024 /2025.

Katibu wa TUGHE Mkoa wa Kagera, Bw. Edward Mwashitanda mwenye (kushoto) akichangia mada katika Baraza la wafanyakazi Kanda ya Bukoba kulia ni Afisa Tawala Mwandamizi Mahakama ya Wilaya Bukoba, Bi. Luciana Lucas.

Picha ya juu na chini ni wajumbe walioshiriki kwenye Kikao wa Baraza la Wafanyakazi kilichofanyika katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Bukoba wakifuatilia kwa makini kinachoendelea kwenye mkutano huo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni