Ijumaa, 6 Juni 2025

WATUMISHI MAHAKAMA KANDA YA MOSHI WAPATIWA MAFUNZO KUONGEZA TIJA, WELEDI KAZINI

Na CAREEN INOSHI NA JAMES KAPELE- Mahakama, Moshi

Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Moshi, hivi karibu ni iliendesha mafuzno kwa Watumishi, lengo likiwa kuongeza weledi na kuchochea ufanisi katika jukumu la msingi la utoaji haki kwa Wananchi.

Mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Kiwanda cha Sukari (TPC) yalishirikisha Majaji, Mahakimu na Watumishi wengine. Jaji Mfawidhi, Mhe. Dkt Lillian Mongella alikuaw Mgeni Rasmi kwenye mafunzo hayo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Mhe. Mongella aliwahimiza Watumishi kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo kwa kuwa mada zilizokuwa zimeandaliwa zilikuwa zinalenga kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kila siku.

 “Shabaha yetu ni kuwajengea uwezo Watumishi wetu wa Mahakama katika maeneo muhimu yanayogusa maadili, uwajibikaji, afya ya akili, uhifadhi wa mazingira, usimamizi wa rasilimali za umma na uwekezaji binafsi,” alisema.

Mafunzo hayo yalihusisha mada mbalimbali ikiwemo Maadili katika Utumishi na Uwajibikaji kazini, Mapambano dhidi ya Rushwa, Afya ya Akili kwa Watumishi wawapo kazini, Uhifadhi wa mazingira na Mapambano dhidi ya ujangili na mada ya Uwezekaji na Ujasiriamali binafsi kwa watumishi.

Wawezeshaji wa mada hizo walitoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, TAKUKURU, KINAPA, UTT na KCMC. Alikuwepo pia Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha, Mhe. Ilvin Mgeta ambaye alitoa mada kuhusu Maadili ya Utumishi wa Mahakama.

Akitoa mada kuhusu Mapambano dhidi ya Rushwa, Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Kilimanjaro, Kamanda Musa Chaulo aliipongeza Mahakama kwa maboresho yaliyofanyika ambayo yameongeza ufanisi mkubwa wa shughuli za kimahakama na kupunguza malalamiko kwa kiasi kikubwa.

Akihitimisha mafunzo hayo, Jaji wa Mahakama Kuu Moshi Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo kwa Kanda ya Moshi, Mhe. Safina Simfukwe aliwashukuru Wawezeshaji wote waliotoa mada na kuwahimiza washiriki kuonyesha matokeo chanya katika majukumu yao ya kila siku baada ya mafunzo hayo.  

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi, Mhe. Dkt. Lillian Mongella akifungua mafunzo hayo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha, Mhe. Ilvin Mgeta akiwasilisha mada wakati wa mafunzo, huku Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Moshi wakifuatilia mafunzo hayo.

Picha ya pamoja ya Viongozi wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi.

Mahakimu, Wasajili na Viongozi wa Mahakama wakila kiapo cha ahadi ya uadilifu baada ya kukamilika kwa mafunzo hayo. Zoezi hilo liliongozwa na Viongozi Waandamizi kutoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Kaskazini.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Moshi, Mhe. Safina Simfukwe akizungumza wakati wa kuhitimisha mafunzo hayo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni