Jumanne, 9 Septemba 2025

JAJI KIONGOZI AHIMIZA HAKI KATIKA UHIFADHI WANYAMAPORI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani amewakumbusha Wadau wa Haki Jinai kwenye uhifadhi wa Wanyamapori kuzigatia haki wanapotekeleza majukumu yao katika ngazi mbalimbali.

Mhe. Dkt. Siyani ametoa wito huo leo tarehe 9 Septemba, 2025 alipokuwa anazungumza kabla ya kumkaribisha Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, kufungua Kikao Kazi cha Wadau hao kinachofanyika kwa siku tatu jijini hapa.

Jaji Kiongozi amewaambia washiriki wa Kikao Kazi hicho kuwa Mahakama imepewa jukumu la mwisho la kutoa haki, lakini haki haianzii mahakamani, bali huanzia kwenye hatua mbalimbali, ikiwemo katika utoaji wa taarifa za makosa ya jinai.

‘Haki inatakiwa kuonekana katika upelelezi, ukamataji, uamuzi wa kushtaki au la, uandaaji wa mashtaka na uendeshaji wa mashauri yenyewe kabla ya Mahakama kutoa uamuzi. Kwa msingi huo, sisi sote tunashiriki kazi ya kutoa haki katika hatua mbalimbali,’ Mhe. Dkt. Siyani amesema.

Amebainisha kuwa msingi wa kazi hiyo ni Mungu na Wadau hao wanajua vizuri kuwa Dini zote zinahubiri haki na haki inayohubiriwa hawamtendei Mungu, bali wanapaswa kutendeana wao wenyewe kama binadamu, lakini na viumbe vingine ambavyo Mungu kwa utashi wake ameviumba.

Jaji Kiongozi ametumia fursa hiyo pia kuwakumbusha Wapelelezi katika vyombo vyote nchini na Waendesha Mashtaka kuwa wanapotekeleza wajibu wao, Katiba inawataka kuongozwa na mambo matatu makubwa, ikiwemo dhamira ya kutenda haki.

‘Kwa kila kinachofanyika, katika hatua zote za kusimamia haki, kila mmoja wetu atangalize swali hilo kwenye nafsi yake; la kwanza ni nini dhamira yake. Je, amebeba dhamira ya kutenda haki, amejiepusha na matumizi mabaya ya taratibu za kutoa haki…

‘… na je, anachokifanya kinabeba maslahi ya umma? Rai yangu kwenu ni kuwa kila wakati tuzielekeze dhamira zetu ndani ya mipaka hiyo na kufanya chochote nje yake ni kukosa uzalendo kwanchi yetu,’ Mhe. Dkt. Siyani amesema.

Akizungumzia umuhimu wa Wanyamapori, Jaji Kiongozi ameeleza kuwa kibailojia, na kwa mujibu wa Convention of Biological Diversity (CBD) 1992, thamani inayoletwa na Wanyamapori ni pamoja na thamani za kiikolojia, thamani za kijenetiki, kijamii, kisayansi, kielimu, kitamaduni, burudani, na thamani za kisanii.

Hata hivyo, amesema, ingawa wamejaribu kuwapa Wanyamapori thamani ya kifedha, ukweli ni kwamba thamani ya Wanyamapori haiwezi kufafanuliwa kwa fedha.

‘Thamani hii kubwa ndiyo iliyotufanya tukutane kwa ajili ya kuhakikisha mgongano wa maslahi ya sasa ya mwanadamu unaotishia uwepo wa wanyama unashughulikiwa kwa wivu na nguvu kubwa ya pamoja,’ Mhe. Dkt. Siyani amesema.

Amebainisha pia kuwa Wanyamapori ni zawadi kwa nchi nyingi duniani na kwa Tanzania wana sifa nyingine za kipekee mbazo zinautofautisha urithi huo na nchi nyingine na kutoa mfano uhamaji wa Nyumbu Serengeti ni tukio la aina yake lenye mkusanyiko mkubwa zaidi wa Wanyama duniani.

Mifano mingine ni uwepo wa viumbe adimu kama vile Faru weusi waliohatarini kutoweka, Tumbili wa Kipunji, Simba wengi zaidi barani Afrika, kundi kubwa la Tembo huko Tarangire, na moja ya ngome kubwa za mbwa mwitu wa Kiafrika huko Selous.

‘Kutokana na umuhimu huu wa kipekee, tumekutana hapa kujadiliana na kubadilishana uzoefu juu ya namna bora ya kulinda urithi huu kwa kila mmoja wetu kama Taasisi kutimiza wajibu wake,’ Jaji Kiongozi amesema.

Kikao Kazi hicho kinawaleta pamoja Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania,Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania, Wadau wa Haki Jinai kutoka Shirika la Hifadhi za Taifa [TANAPA], Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Jeshi la Polisi, Taasisi ya Kudhibiti na Kupambana na Rushwa [TAKUKURU] na Viongozi na Watendaji wengine kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi.

Kauli mbiu ya Kikao Kazi hicho inasema, ‘Haki kwa mazingira: Kuongeza ushirikiano kati ya Mahakama na Teknolojia katika kupambana na uhalifu wa Wanyamapori nchini Tanzania [Justice for Nature: Enhancing Judicial and Technological synergy in combating wildlife crime in Tanzania.]

Mada mbalimbali zitawasilishwa na Wawezeshaji ambao waliobobea kwenye masuala ya uhifadhi, ikiwemo mafanikio na changamoto katika ulinzi wa Wanyamapori Tanzania, matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano [TEHEMA] katika mfumo wa haki jinai na ulinzi wa wanyamapori.

Mada nyingine ni, Mianya, Changamoto na fursa za maboresho na matumizi ya sayansi katika uendeshaji wa mashauri yahusishayo uhalifu dhidi ya Wanyamapori, mchango wa Mahakama katika ulinzi na matumizi anuai ya rasilimali zetu, kukuza utalii, lakini pia tahadhari dhidi ya msongo wa mawazo utokanao na kazi.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani [juu na chini] akizungumza kwenye ufunguzi wa Kikao Kazi cha Wadau wa Haki Jinai kwenye masuala ya uhifadhi wa Wanyamapori nchini.



Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa utambulisho wa wageni mbalimbali kabla ya ufunguzi rasmi wa Kikao Kazi hicho.


Sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania [chini na picha mbili juu] wakiwa kwenye Kikao Kazi hicho.


Wadau wa Haki Jinai kwenye masuala ya uhifadhi wa Wanyamapori [juu na picha mbili chini] wakiwa kwenye Kikao Kazi hicho.


 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni