Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha
Naibu
Msajili Mfawidhi wa
Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Amir Msumi amesema kuwa ushirikiano baina ya Mahakama na Jeshi la
Polisi ni muhimu ili kuhakikisha mashauri ya jinai yanayoletwa mahakamani
yanasikilizwa mapema ipasavyo kuepuka kuchelewesha haki za watu pamoja na
kuzuia mlundikano wa mashauri usio wa lazima.
Mhe. Msumi aliyasema hayo hivi karibuni alipokuwa
akifungua Mafunzo ya Kubadilishana Uzoefu Kuhusu Utaratibu wa Ufunguaji na Uendeshaji wa Mashauri ya Jinai katika Mahakama za Mwanzo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo
Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) jijini Arusha.
Akizungumza
wakati wa ufunguzi, Naibu Msajili alieleza kuwa, mafunzo hayo yalilenga
kuongeza uelewa, kuimarisha weledi na kukuza ushirikiano kati ya Mahakama na Jeshi
la Polisi lengo likiwa ni kuhakikisha
mashauri ya jinai yanashughulikiwa kwa haraka, ufanisi na kwa mujibu wa sheria.
“Nawaomba washiriki kutumia
kikamilifu fursa hii
ya mafunzo kwa kuuliza maswali, kujadili changamoto na kubadilishana mbinu bora
zinazoweza kusaidia kuboresha huduma za utoaji haki katika ngazi ya Mahakama za
Mwanzo,” alisisitiza Mhe.
Msumi.
Akiwasilisha mada, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Themi, Mhe. Julieth Mbise alieleza kuwa, zipo changamoto nyingi zinazokwamisha uendeshaji wa haki jinai, ikiwemo kasoro katika hati za mashtaka, ucheleweshaji wa vielelezo, kutokuwepo kwa walalamikaji mahakamani na kutofuatwa kwa taratibu za upelelezi.
Mhe. Mbise alisisitiza kwamba,
ushirikiano madhubuti kati ya Mahakama na Polisi ni muhimu ili kuhakikisha haki
inatolewa kwa wakati na kuimarisha imani ya wananchi kwa vyombo vya utoaji
haki.
Naye Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya
Arusha, ASP Mahita Omary alizungumzia changamoto zinazolikabili Jeshi la Polisi
katika kushughulikia mashauri kuwa, ni pamoja na watuhumiwa kujidhamini, adhabu
ndogo zinazotolewa na Mahakama pamoja na Mahakama kuahirisha mashauri bila
kujali kwamba mashahidi wameletwa kwa ajili ya shauri husika kusikilizwa.
Akizungumzia kuhusu suala la
watuhumiwa kujidhamini wenyewe katika Mahakama za Mwanzo, ASP Mahita alisema
kuwa, pamoja na kwamba dhamana ni haki ya mtuhumiwa kwa makosa yenye dhamana, Mahakama
imekuwa ikitoa dhamana bila kuwa na taarifa za kina za mtuhumiwa na mdhamini
wake, hali ambayo husababisha mtuhumiwa kutorudi mahakamani na Mahakama
kulazimika kutoa tena hati ya kukamatwa mtuhumiwa huyo kwa Jeshi la Polisi.
Akitoa
neno la kufunga mafunzo hayo,
Hakimu
Mkazi
Mfawidhi
wa Mahakama
ya Wilaya ya Arusha, Mhe.
Sheila Manento aliwahimiza
washiriki kuzingatia uadilifu na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao,
akibainisha kuwa hakuna haki bila uaminifu.
Aliwataka
pia washiriki kuendeleza kujifunza kila mara ili kuendana na mabadiliko ya
dunia ya sasa na kuwapongeza
waandaaji wa mafunzo hayo kwa maandalizi bora na kuwashukuru washiriki wote kwa
nidhamu na ushirikiano
waliouonesha.
Kikao hicho kililenga kujadili
changamoto, kueleza athari zake katika upatikanaji wa haki na kutoa mapendekezo
ya uboreshaji, ikiwemo kuongeza ushirikiano kati ya Mahakama na Jeshi la
Polisi, mafunzo endelevu kwa askari na matumizi ya Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano (TEHAMA) katika kutoa taarifa kwa walalamikaji.
Mafunzo
haya yaliandaliwa na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Mwanzo katika Wilaya ya
Arusha, ambazo ni Mahakama ya Mwanzo Themi, Arusha Mjini na Terat na kuratibiwa
na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Arusha.
Wajumbe mbalimbali walihudhuria mafunzo hayo wakiwemo
Mahakimu Wakazi wote wa Mahakama za Mwanzo katika Wilaya ya Arusha pamoja na
wawakilishi kutoka Jeshi la Polisi.
Washiriki wa mafunzo baina ya Mahakama za Mwanzo wilayani Arusha na Jeshi la Polisi wakiwa katika picha ya pamoja. Mafunzo hayo yalifanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni