● Yafanya mafunzo yazingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050
● Yadhamiria kuimarisha haki, usawa wa kijinsia nchini
Na HALIMA MNETE, Mahakama-Dodoma
Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba 2025 kimeanza kufanya mafunzo maalum kwa Waratibu wa Kikanda wa chama
hicho, ambayo yamelenga kuimarisha uongozi, usimamizi na uwajibikaji katika
kulinda haki za kijinsia na za binadamu.
Mafunzo hayo yalifanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao
Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, ambapo mgeni rasmi alikuwa Jaji
Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa TAWJA ambaye
pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Barke Sehel, alisema kuwa kufanyika kwa
mafunzo hayo kuongeza uwezo wa Waratibu wa Mkoa katika uratibu, mawasiliano, na
utekelezaji wa programu za kikanda.
“Tunatarajia kuwa kupitia waratibu hawa, TAWJA itaimarika na
kuwa kinara katika ulinzi wa haki za binadamu na usawa wa kijinsia nchini,”
alisema Mhe. Sehel.
Aliwataka washiriki wa mafunzo hayo kutumia fursa hiyo
kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuweka mikakati ya pamoja itakayosaidia
kuboresha ushiriki wa wanawake katika uongozi, si tu ndani ya Mahakama bali pia
katika jamii kwa ujumla.
Kwa mujibu wa Mhe. Sehel, TAWJA imejikita katika kupambana
na unyanyasaji wa kijinsia kwa kutoa elimu, kuhamasisha jamii na kushirikiana
na Taasisi mbalimbali ili kuhakikisha haki za wanawake na watoto zinalindwa.
Aliongeza kuwa, takwimu zinaonyesha mashauri ya unyanyasaji
wa kijinsia bado ni changamoto nchini, jambo linalohitaji juhudi endelevu za
wadau wote katika kutoa elimu na kufungua mashauri kwa wakati.
Mhe. Sehel alitumia nafasi hiyo kumshukuru Jaji Mkuu wa
Mahakama ya Tanzania kwa kukubali mwaliko wa kuwa mgeni rasmi na kwa kuonyesha
utayari wa kuunga mkono juhudi za chama katika kukuza nafasi ya mwanamke ndani
ya mfumo wa Mahakama na jamii kwa ujumla.
Mafunzo hayo ya siku mbili yamefadhiliwa na Mahakama ya Tanzania kupitia
ofisi ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama, hatua inayodhihirisha ushirikiano mkubwa
unaolenga kutimiza Ibara ya 9 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
inayosisitiza heshima ya utu, usawa wa binadamu na haki sawa kwa wote bila
ubaguzi.
Mada mbalimbali zitawasilishwa kwenye mafunzo hayo ya siku mbili, ikiwemo Dhamira na Vipaumbele vya Kimkakati vya TAWJA, Uimarishaji wa Uanachama na Ushiriki wa Kikanda, Haki za Kijinsia na Uongozi, Ufuatiliaji na Tathmini, pamoja na Uhamasishaji wa Rasilimali na Uendelevu. Mada hizo zinalenga kuendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025/2050 inayohimiza utawala bora, amani, usalama, na fursa sawa kwa wote.




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni