Ijumaa, 24 Oktoba 2025

BILA AMANI HAKUNA USTAWI WA WANANCHI: JAJI MKUU

  •  Wanawake kama viongozi timizeni wajibu wa kulinda amani, usawa katika jamii
  •  Asema kila Mtanzania ana haki ya kutambulika kwa jinsia yake

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa bila amani hakuwezi kuwa na ustawi wa wananchi jambo ambalo litasababisha jamii kushindwa kutekeleza shughuli zake za kila siku mfano kilimo na uvuvi.

Mhe. Masaju aliyasema hayo jana 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma,wakati alipokuwa akifungua Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) huku akiwataka Majaji na Mahakimu kama wanawake kama viongozi kutimiza wajibu wao wa kulinda amani hasa wanawake wanaofanya kazi katika Mahakama kudumisha Utawala wa Sheria.

“Hivyo bila kuwepo amani, hakuwezi kuwa na ustawi wa wananchi huwezi kwenda shambani, huwezi kwenda kulima, huwezi kwenda kuvua, huwezi kufunga ndoa, huwezi kwenda kwenye ibada huwezi kufanya hata na mambo ya uongozi, huwezi kufanya kazi, utafanyaje kazi wakati hakuna amani kwa hiyo wajibu wa wanawake katika kazi zenu na kama viongozi ni kusisitiza haya na hasa nyinyi wa Mahakamani ambao mna jukumu kubwa sana la kudumisha utawala wa sheria,” alisisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju alisema kuwa, amani ndio nguzo muhimu ya ustawi wa jamii na kuwataka wanawake ambao ni viongozi kusisisitiza kuhusu amani katika kutekeleza majukumu yao na hasa Mahakama ambayo ina jukumu kubwa la kudumisha utawala wa sheria.

Aidha, Jaji Mkuu, alizungumzia msingi wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwenye utawala, amani, utulivu na usalama pamoja na vipengele vyake vikuu vinne ikiwa ni pamoja na Utawala Bora na Haki, Serikali za mitaa imara zenye ufanisi pamoja na vingine ambavyo vina mchango mkubwa katika kutunza na kuendeleza usalama na ustawi wa Taifa.

Akizungumza kuhusu suala la Utawala wa Sheria, Mhe. Masaju alisema kuwa, “Utawala wa Sheria uliwekwa kwa sababu gani ni kutaka kushamirisha na kuhakikisha kwamba kunakuwa na ustawi wa wananchi ili watu waweze kufanya shughuli zao za kisiasa, kiuchumi na kijamii kwa amani na wakiwa huru lakini sizungumzii utawala wa sheria ambao sisi tumeutaja katika Ibara ya 26 katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.”

Katika upande mwingine, Jaji Mkuu alieleza kuwa Serikali na Vyombo vyote vya Umma vinatoa haki sawa kwa raia wote bila kujali rangi, kabila au dini ya mtu kama inavyotambulika katika Ibara ya 12 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba binadamu wote huzaliwa huru na wote ni sawa.

“Vyombo vyote vya umma vinatoa nafasi iliyo sawa kwa raia wote wake kwa waume bila kujali rangi kabila, dini au hali ya mtu, kwa kuangalia mtu unasema huyu wa dini fulani, sasa hiyo ni changamoto, kwa aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, rushwa, uovu au upendeleo vinaondolewa nchini, kwamba matumizi ya utajiri wa Taifa yanatilia mkazo maendeleo ya wananchi na hasa zaidi yalielekezwa kwenye jitihada za kuondoa umasikini, ujinga na maradhi,” alisema Mhe. Masaju.

Aliongeza kuwa, kila Mtanzania ana haki ya kutambulika kwa jinsia yake, na kuthaminiwa kupewa haki kama ilivyotajwa katika Ibara ya 12 (2) kwamba kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake.

“Mimi naamini tunapaswa kutambua na kuthamini hizi jinsia zetu kwa jinsi wanavyozaliwa anayezaliwa mwanaume ataitwa mwanaume, anayezaliwa mwanamke ataitwa mwanamke, vinginevyo tutashindwa kupata haki iliyotajwa katika Ibara ya 12 kwa sababu binadamu wote tumezaliwa huru na wote ni sawa,” alisema Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju aliwasisitiza pia TAWJA kusimamia uhuru wao wa kufanya maamuzi na kwamba wawe huru kufanya kazi kwa kuzingatia Katiba na Sheria bila kuburuzwa na mtu yoyote ili kuendelea kujenga jamii yenye ustawi amani na usawa.


 Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakifuatilia hotuba ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA)  iliyokuwa ikitolewa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha).


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha za pamoja na makundi mbalimbali ya Wanachama na Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama hicho. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya na Makamu Mwenyekeiti wa Chama hicho, Mhe. Victoria Nongwa.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni