Ijumaa, 24 Oktoba 2025

MAJAJI NA MAHAKIMU WANAWAKE MNA WAJIBU WA KULETA USAWA KATIKA JAMII; JAJI MKUU

 ·       Awasisitiza Majaji, Mahakimu Wanawake kusimamia maadili ya jamii

·       Asisitiza usawa kati ya Mwanamke na Mwanaume

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amesema Majaji na Mahakimu Wanawake nchini wana wajibu mkubwa wa kusimamia haki za binadamu, maadili ya jamii na usawa wa kijinsia ili kuleta ustawi katika jamii.

Akizungumza jana tarehe 23 Oktoba, 2025 wakati akifungua Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) kwenye ukumbi wa Mikutnao wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Mhe. Masaju alisema kupitia mafunzo hayo ni muhimu wakaweka mikakati thabiti itakayowezesha kufikia ustawi katika jamii.

“Ninachoona ni kwamba ninyi TAWJA mnajitambua, wajibu wenu leo ni kuja na mikakati ambayo itawezesha kutatua hizi changamoto ambazo zimekuwa zinajitokeza kwenye haya masuala yanayowahusu na hasa haki za binadamu wote ambao humo wanajumuishwa Wanawake na Wanaume wakiwa wa umri mbalimbali, wengine watu wazima, wengine wazee na wengine Watoto kwa mfano kuna changamoto hii ya makosa unyanyasaji wa kijinsia,” alisema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju alibainisha kuwa, kumekuwa na makosa ya unyanyasaji wa kijinsia na wakati fulani kumekuwa na tafsiri ambayo sio sahihi kwamba jinsia inawahusu Wanawake tu, lakini ni pamoja na wanaume, na hata wanaume kwa wakati au namna fulani nao wananyanyaswa na wa jinsia tofauti.

“Ninatambua kwamba tatizo la unyanyasaji wa wanawake pengine ni wa kiwango kikubwa kuliko ukilinganishwa na unyanyasaji wa wanaume, lakini na wanaume wananyanyaswa isipokuwa tu wanavumilia, jamii yetu imeweka mfumo ambao mwanaume hapaswi kuonekana kama ni dhaifu vile lakini wanavumilia tu na wakati fulani wanapoteza maisha mapema na wakishapotea ndio tunawatambua umuhimu wao, mimi nawashauri muendelee kuwajali wakiwa hai, nawahakikishia kila mmoja anamuhitaji mwenzake, mwanaume anamuhitaji sana mwanamke na mwanamke anamuhitaji sana mwanaume,” alisisitiza Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju aliongeza kwa kusisitiza kuhusu usawa wa kijinsia ambapo amesema hata Nembo ya Taifa ya Tanzania nayo imeonesha umuhimu kwa kuwa ina Bibi na Bwana, “Mimi si mtaalamu sana wa masuala ya nembo za Taifa japo najua nembo za taifa za Mataifa yote Duniani lakini Tanzania ni ya pekee, Nembo ya Taifa letu inamtambua Mwanaume na Mwanamke na usawa unaanzia pale kama binadamu na wote wanapewa uhuru wa rasilimali za Nchi, hawa ndio wananchi wanaounda Taifa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama inavyoelezwa kwenye Ibara ya 1 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inasema (i) Tanzania ni Nchi moja nayo ni Jamhuri ya Muungano na Ibara ya 2 (1) inaeleza; Eneo la Jamhuri ya Muungano ni eneo lote la Tanzania Bara na eneo lote la Tanzania Zanzibar na pamoja na sehemu yake ya Bahari ambayo Tanzania inapakana nayo.”

Alisema kupitia Nembo hiyo, kila mmoja anaonekana akiwa ameshika Pembe ya Ndovu ambayo ndio utajiri urithi wa Taifa la Tanzania na kiwango cha pembe walichoshika ni sawa kwa hazitofautiani kwa urefu ama ufupi, juu ya nembo hiyo pia kuna Taifa la Tanzania ambao ndio wanamiliki rasilimali za Taifa na nyingine zilizomo kwenye nembo hiyo....

Jaji Mkuu alisema, misingi ya umoja kati ya umoja Mwanaume na Mwanamke ilishawekwa tangu Taifa lipate uhuru na ndio ilipokuja kauli ya ‘Uhuru na Umoja’ hivyo, Mwanaume na Mwanamke wanaounda Taifa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwa wanaheshimiana, watakuwa huru na wamoja, na kila mmoja amepewa fursa ya kufaidi matunda ya uhuru na rasilimali za nchi na stahili zake nyingine zote.

“Sasa wajibu wetu sisi TAWJA ni kutambua changamoto zinazofanya tusifikie hayo malengo ambayo yapo tangu kuasisiwa na kwa Taifa hili na yamesisitizwa pia katika Katiba Ibara ya 7, 8, 9, 11 lakini pia Ibara ya 22; Ibara ya 22 na 24 zinasema; kila mtu anayo haki ya kufanya kazi; hivyo; mtaendelea kutambua changamoto zipi zinazofanya kwa mfano wanawake wakose hizo fursa,” alisisitiza Mhe. Masaju.

Aliongeza kwamba, Ibara (2) inasema; ‘kila raia anastahili fursa na haki sawa kwa masharti ya usawa ya kushika nafasi yoyote ya kazi na shughuli yoyote iliyo chini ya mamlaka ya Nchi; “hivyo nyie kama Viongozi mtajifunza ni namna gani mtaweza kuimarisha fursa ya ku ‘access’ hivi vitu maana havitakuja kwa upendeleo,” alisisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju alisema, Majaji na Mahakimu hao wao kama Wanasheria wanaofahamu Katiba na Sheria mbalimbali wana nafasi kubwa ya kuwa chachu ya mabadiliko chanya katika kuimarisha usawa na heshima ya kijinsia katika Taifa.

“Ibara ya 24 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu kumilika mali inasema; ‘kila mtu anayo haki ya kumiliki mali na haki ya hifadhi ya mali yake aliyo nayo kwa mujibu wa sheria’,” alisema Jaji Mkuu huku akiongeza kuwa hata mwanamke ana haki ya kumiliki mali kama vile Ardhi na kadhalika.

Aidha, Mhe. Masaju alibainisha kwamba, Ibara ya 7 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema, ‘Bila kujali masharti ya Ibara (2) ya Ibara hiyo, Serikali, vyombo vyake vyote na watu wote au mamlaka yoyote yenye kutekeleza mamlaka ya utawala, Madaraka ya kutunga sheria au Madaraka ya Utoaji haki watakuwa na jukumu na wajibu wa kuzingatia, kutia maanani na kutekeleza masharti yote ya sura hiyo, na Ibara ya 8 inasema Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii...’

Mhe. Masaju amekihakikishia Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) kuwa Mahakama ya Tanzania itaendelea kuwaunga mkono jitihada zinazofanywa na Chama hicho katika kuleta usawa wa kijinsia.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) (hawapo katika picha) wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama hicho jana tarehe 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju wakati wa hafla ya Ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha za pamoja na makundi mbalimbali ya Wanachama na Waratibu wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mafunzo kwa Waratibu wa Chama hicho. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA), Mhe. Barke Sehel na kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya na Makamu Mwenyekeiti wa Chama hicho, Mhe. Victoria Nongwa.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akisalimiana na Majaji Wastaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania ambao pia ni Wanachama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake Tanzania (TAWJA) jana tarehe 23 Oktoba, 2025. Kulia ni Mhe. Dkt. Atuganile Ngwalla na katikati ni Mhe. Joaquine De-Mello.












 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni