Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe.
Augustine Rwizile ameongoza watumishi na wadau wa Mahakama mkoani
humo kusherehekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini katika viunga
vya Mahakama hiyo.
Akizungumza katika hafla hiyo jana tarehe 02 Februari, 2026,
Mhe. Rwizile alisema kuwa, Mahakama inayo malengo na mikakati inayoendana na
kasi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 katika kuimarisha mifumo mbalimbali ya
haki, maendeleo ya uchumi wa Taifa na kuboresha
utendaji kazi wa Mahakama.
“Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imetoa fursa kwa wananchi wake
kufanya kazi kwa uhuru, kuishi kwa mshikamano na utengamano katika kudumisha
haki, amani na kuheshimiana. Dira hiyo pia imelenga wananchi wenye maarifa,
ujuzi unaohitajika katika Karne ya 21 ya Sayansi na Teknolojia ili waweze
kushiriki kikamilifu shughuli za maendeleo kwa makundi yote ya Wazee, Wanawake,
Vijana, watu wenye ulemavu na makundi yote maalum, Dira hiyo imewapa nafasi,”
alisema Jaji Rwizile.
Jaji Rwizile alisema kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka
2050, imesimamia misingi mikuu mitano ambayo ni Demokrasia, Haki na Uhuru, Amani
na Umoja kama msingi wa maendeleo ambapo Mahakama huchukua jukumu kubwa la
kutatua migogoro inayotokana na misingi hiyo katika maisha ya kila siku.
Aidha, aliongeza kwa kusema kwamba, “Dira hiyo inatathmini na kulinda
muungano wetu, ambao ni tunu ya Taifa na watu wote kuheshimiana na kuchangia
katika kufanikisha malengo ya pamoja ya Kitaifa, vilevile utajiri na rasilimali za nchi zitumike kikamilifu rasilimali zake kwa manufaa ya Taifa
na ustawi wa wananchi wake, kwamba rasilimali tulizonazo zinapaswa kulindwa ili
zitunufaishe wote kwa pamoja na msingi wa mwisho ni Utamaduni na Maadili ya Taifa
ambapo Dira hiyo inatuhimiza kuhifadhi utamaduni uliopo kulinda, kukuza maadili
na utamaduni chanya unaotutambulisha Kitaifa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na
vijavyo.”
Mhe. Rwizile aliongeza kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050
imeonesha kuwa, miaka 25 ijayo Tanzania
itakuwa na Mahakama zenye hadhi na kuheshimika Dunia nzima, ili kufikia hilo
lazima Mahakama itende haki bila kuona hali ya mtu kiuchumi, katika jamii,
kutochelewesha haki bila sababu za msingi, kutoa fidia stahiki kwa watu
waliofanyiwa makosa na watu wengine kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge,
kukuza usuluhishi kwa migogoro inayoletwa Mahakamani, kutenda haki bila
kufungwa na masharti ya kiufundi katika utoaji haki.
Kwa upande wake Wakili wa Serikali, Bw. George Kalenda alisema
kuwa, Kaulimbiu ya Siku ya Sheria ya mwaka huu isemayo, ‘Mchango wa Mahakama
katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa,’’ inazitaka Taasisi zinazosimamia haki
kujipanga kutekeleza malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 kwa
kushirikiana kwa pamoja ili kuisaidia Mahakama kutenda haki na kutoa mchango wa
Mahakama katika ustawi na maendeleo ya Taifa.
“Tunatakiwa kuwajibika katika shughuli zetu za kila siku ili
kufikia malengo yetu jumuishi katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya
Maendeleo katika ustawi wa Taifa, Utawala wa Sheria, kutenda haki, kuheshimu
haki za binadamu, uhuru wa Mahakama, weledi na uadilifu katika kusimamia haki
Mahakamani,” alisema Bw. Kalenda.
Naye, Mwenyekiti wa Jukwaa la Mawakili wa Kujitegemea, Bw.
Eliutha Kivyiro alisema kuwa, malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ni pamoja na kukuza Taifa jumuishi lenye
ustawi wa haki na linalojitegemea, hivyo, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS)
ni Taasisi muhimu katika kufikia malengo ya Dira hiyo katika kuisaidia Mahakama
kutenda haki mapema ipasavyo.
Aliongeza kuwa, ili kufikia malengo ya Mahakama ya kuchangia
ustawi na maendeleo ya Taifa ameshauri kuimarisha uwezo wa Wanataaluma na Taasisi
katika utatuzi wa migogoro kwa njia zote ikiwemo usuluhishi,
“Aidha Mahakama inatoa mwongozo wa kisheria katika vyombo vingine ili kuendenda
katika misingi ya sheria ili kuleta ustawi wa Taifa na maendeleo ya wananchi,
inapotoa haki kwa wakati bila kupoteza muda kwa namna yoyote.”
Wadau waliohudhuria Maadhimisho ya Kilele cha Siku ya Sheria nchini ni pamoja na Watumishi wa Kanda hiyo, Mawakili wa Serikali, Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, Viongozi wa Dini, Wakuu wa Taasisi za Umma, Chuo cha Mafunzo Kigoma (KTC), Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mlole, Wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wavulana Kigoma, wananchi kutoka sehemu mbalimbali ya Mkoa wa Kigoma, Ubalozi mdogo wa Burundi na wengine.
Wakili Mfawidhi wa Serikali, Bw. George Kalenda akitoa salamu katika hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini iliyofanyika jana tarehe 02 Februari, 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu Kigoma.
Mwenyekiti wa Jukwaa la Mawakili wa Kujitegemea Tanganyika (TLS), Bw. Eliutha Kivyiro akitoa salamu zake wakati wa hafla ya Kilele cha Siku ya Sheria nchini iliyofanyika katika viunga vya Mahakama Kuu Kigoma.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni