Jumanne, 3 Februari 2026

MAHAKAMA MANYARA YAAHIDI USHIRIKIANO KWA WADAU ILI KULETA MAENDELEO YA TAIFA

Na. Christopher Msagati-Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin C. Mugeta ameahidi kutoa ushirikiano katika ufanikishaji wa shughuli za maendeleo nchini ambazo zinafanyika kwa ajili ya mustakabali wa ustawi na maendeleo ya Taifa.

Mhe. Mugeta ameyasema hayo jana tarehe 02 Februari, 2026 katika maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2026 ambayo Kikanda yameadhimishwa katika viwanja vya Mahakama Kuu Manyara wilayani Babati mkoani Manyara.

“Mazingira mazuri ya upatikanaji wa haki yanasaidia katika ustawi wa Taifa na maendeleo yake kwa ujumla, tumebaini kuwa mashauri yakikaa mahakamani kwa muda mrefu, wananchi hukosa muda wa kushiriki katika shughuli zao za kiuchumi na kijamii, hivyo maendeleo huzorota…

…Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, itaendelea kuboresha zaidi huduma hii ya msingi kwa kuendelea kutoa hukumu zenye weledi lakini pia kwa kufupisha muda wa kusikiliza mashauri na hivyo kuwawezesha wananchi kupata muda wa kufanya shughuli zao za kiuchumi kwa mustakabali wa maendeleo ya Taifa letu,” alisema Mhe. Mugeta.

Akiongea kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mkuu wa Wilaya ya Babati Mhe. Emmanuela Kaganda alisema Serikali itaendelea kufanya kazi bega kwa bega na Mhimili wa Mahakama kwa kuwezesha upatikanaji wa mazingira rafiki ya utendaji kazi ikiwemo kuipatia Mahakama mahitaji ya muhimu ambayo yataiwezesha Mahakama kufanya kazi zake pasipo matatizo yoyote.

“Kaulimbiu ya maadhimisho ya Siku ya Sheria Mwaka huu, inaonesha jinsi ambavyo maendeleo ya taifa lolote yanavyostawi kwa kutegemea upatikanaji wa Haki na Amani. Aidha, Mkoa wetu wa Manyara umegubikwa na wimbi kubwa la makosa ya ukatili wa kijinsia na mengineyo mengi ambayo yanakwamisha maendeleo ya taifa letu kwa namna moja ama nyingine. Ninaviasa vyombo vya Haki Jinai kuendelea kushirikiana kwa pamoja ili tuweze kuwa na Taifa lenye nidhamu na maendeleo,” alisema Mhe Kaganda.  

Kwa upande wake, Bw. Lameck Butuntu ambaye ni mwakilishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali alisema, Mahakama ina mchango mkubwa katika kuwezesha uwekezaji kutoka kwa watu mbalimnbali wa ndani na hata nje ya nchi.

“Wawekezaji katika miradi mbalimbali ya kiuchumi hupenda kuwekeza katika maeneo ambayo kuna mazingira salama yasiyokuwa na migogoro lakini pia ambayo yana tija katika upatikanaji bora wa Haki, hivyo ni rai yetu kuwa Mahakama iendelee kufanya kazi kwa bidii na kwa kuboresha zaidi upatikanaji wa huduma hususani kwa kujenga miundombinu wezeshi ya kuwavutia wawekezaji,” alisema Bw. Butuntu.

Mahakama Kuu Kanda ya Manyara imeungana na Mahakama za Kanda na Mikoa mingine nchini kuadhimisha Siku ya Sheria kwa Mwaka 2026, yenye Kaulimbiu isemayo “Mchango wa Mahakama katika Ustawi na Maendeleo ya Taifa” kaulimbiu ambayo imesisitiza umuhimu wa Mhimili wa Mahakama katika ukuaji wa maendeleo ya kiuchumi na Kijamii kwa kuzingatia Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2050.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta akitoa hotuba ya Siku ya Sheria Nchini kwa Wananchi na wadau waliohudhuria katika viwanja vya Mahakama Kuu Manyara.

Mwakilishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mkoa wa Manyara Bw. Lameck Butuntu akitoa hotuba yake ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2026 mbele ya Wananchi na wadau waliohudhuria katika viwanja vya Mahakama Kuu Manyara.


Meza Kuu wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu Manyara.

Mkuu wa Wilaya ya Babati Mhe Emmanuela Kaganda akitoa hotuba yake kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2026 katika viwanja vya Mahakama Kuu Manyara.

1.     Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin Mugeta akiwa na Meza Kuu katika maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini kwa Mwaka 2026, (wa pili kulia) ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora, kulia ni Mwakilishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mkoa wa Manyara Bw. Lameck Butuntu, (wa tatu kushoto) ni Mkuu wa Wilaya ya Babati Mhe. Emmanuela Kaganda, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Manyara Mhe. Nenelwa Mwihambi na . wa kwanza kushoto ni Bw. Tadei Lister ambaye ni Mwenyekiti wa Mawakili wa Kujitegemea Mkoa wa Manyara.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. Ilvin C. Mugeta akikagua gwaride maalumu lililoandaliwa katika maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini mwaka 2026.

 (Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni