Jumanne, 5 Mei 2026

ENDELEZENI UZALENDO KATIKA UTENDAJI KAZI WENU; JAJI MSTAAFU, MHE. DKT. STEVEN BWANA

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana ametoa rai kwa watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Kigoma kufanya kazi kwa uzalendo ili kujenga Mahakama yenye sifa njema katika Taifa lenye umoja na uzalendo wa kweli katika utumishi wa umma.

Akizungumza katika kikao kifupi na watumishi wa Mahakama hiyo jana tarehe 04 Mei, 2026 alipotembelea Mahakama Kuu Kigoma, Mhe. Bwana alisema, “Nimeambiwa mnafanya vizuri Kigoma, ni rai yangu kwenu kuendelea kufanya kazi kwa kujituma, uzalendo wa kweli kwa Taifa na bila kuangalia utapata nini kesho, maana kazi zako zitakupa kukua, kuaminiwa na kutengeneza nafasi kubwa zaidi katika utumishi wenu.”

Jaji Mstaafu huyo amewaeleza watumishi hao kukumbuka kuwa shughuli zao za kila siku ndio msingi na kichocheo cha maendeleo ya Taifa na kusisitiza kuwa, “Wastaafu tulifanya sehemu yetu, ambapo teknolojia katika Mahakama kipindi hicho ilikuwa kidogo sana lakini tulifanya kwa uzalendo na kujituma na shughuli za kusikiliza mashauri na utawala zilifanyika vema.”

Aidha, Mhe. Dkt. Bwana alisema kuwa, ni mara yake ya kwanza kufika mkoani Kigoma, hivyo ni vema kuacha alama ya zawadi ya kitabu chake kiitwacho, ‘Maisha yangu, Utumishi wangu” chenye Tawasifu yake, ili kiwekwe kwenye Maktaba ya Mahakama hiyo hatimaye watumishi waweze kusoma maudhui ya kitabu hicho na kuongeza weledi wa kizalendo katika eneo la maisha ya utumishi wa umma.

Naye Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile alipata wasaa wa kumzungumzia walau kwa kifupi Jaji Mstaafu, Mhe. Dkt. Steven Bwana kupitia kitabu chake kuwa ni moja ya Majaji wa Rufani ambaye alihudumu kwa weledi, kujituma kwa uzalendo mkubwa wakati wa kipindi chake, hivyo kufika kwake Kigoma ni jambo la muhimu na kuigwa na watumishi wa sasa hasa kwa umakini wake na utumishi uliotukuka katika kuwahudumia wananchi katika nafasi mbalimbali alizowahi kuaminiwa na Mahakama ya Tanzania.

Kwa upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa, alitoa neno la shukrani kwa Jaji Mstaafu, Mhe. Dkt. Bwana aliyeambatana na Mkewe kutembelea Mahakama Kuu Kigoma.

Aidha, Mhe. Mbelwa alimuomba Jaji huyo kupanda mti ili kuacha alama ya ujio wake wa kutembea kituo hicho, hata hivyo Jaji Mstaafu huyo aliridhia kupanda mti kama kumbukumbu ya ujio wake Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana (kulia) akimkabidhi Kitabu cha wasifu wake Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Karichuba Rwizile wakati Jaji Mstaafu huyo alipotembelea Mahakama Kuu Kigoma jana tarehe 04 Mei, 2026.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile akisoma Kitabu alichokabidhiwa na Jaji msatafu wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dr. Steven Bwana kwa ajili ya watumishi kusoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile (katikati) akimkaribisha Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana (kulia) alipowasili katika viunga vya Mahakama Kuu Kigoma jana tarehe 04 Mei, 2026. Aliyesimama kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. John Nkwabi.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akitoa neno la shukrani kwa Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Steven Bwana (hayupo katika picha), na mkewe kwa niaba ya watumishi wa Mahakama Kanda ya Kigoma.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana, na  Mkewe wakikata keki maalum ya upendo iliyoandaliwa kwa ajili yao walipotembelea Mahakama Kuu Kigoma.

Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana akipanda mti katika eneo la mbele ya jengo la Mahakama Kuu Kigoma alipotembelea Mahakama hiyo jana tarehe 04 Mei, 2026.

 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Agustine Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na 
Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Steven Bwana (kushoto) na mkewe, Mama Steven Bwana.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Njombe)

 

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni