Na WINFRED NZILANO-Mahakama Kisutu, Dar es Salaam
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Jingu, tarehe 27 Agosti, 2026, alifanya kikaokatika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, kuzungumza na watumishi.
Watumishi hao walitoka katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na Kinondoni, wawakilishi kutoka Mahakama za Wilaya Kivukoni, Temeke, Kigamboni, Ilala na Ubungo.
Hii ni mara yake ya
kwanza tangu ateuliwe na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kushika wadhifa huo. Dkt. Jingu aliambatana na
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya.
Kikao hicho kililenga
kufanya utambulisha kwa watumishi, kufahamu mwenendo wa utekelezaji wa majukumu
na kusikiliza changamoto zinazowakabili katika mazingira yao ya kazi.
Akizungumza katika kikao
hicho, Dkt. Jingu alitoa shukrani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa
uteuzi wake. Alieleza ujio wake ni sehemu ya juhudi za uongozi wa Mahakama
kuendelea kuwa karibu na watumishi na kupata uelewa wa moja kwa moja kuhusu
changamoto wanazokutana nazo katika kutekeleza majukumu yao.
Katika kikao hicho,
watumishi walipata fursa ya kuwasilisha changamoto, hoja na mapendekezo
mbalimbali yanayohusu mazingira ya kazi na utekelezaji wa majukumu yao. Dkt.
Jingu aliahidi kuzifanyia kazi kwa kuzingatia taratibu na mamlaka zilizopo.
Kwa upande wake, Msajili
Mkuu aliwasihi watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma
katika kutekeleza majukumu yao. Alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora kwa
wote wanaofika mahakamani ili kujenga taswira nzuri ya Mahakama kwa wananchi.
Naye Hakimu Mkazi
Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga, alitoa
shukrani kwa juhudi ambazo zimefanyika kuboresha masilahi ya watumishi na
miondombinu ya Mahakama.
Kikao hicho kimeonesha dhamira ya uongozi wa Mahakama ya Tanzania ya kuwa karibu na watumishi, kusikiliza changamoto zao na kuweka mazingira bora ya utendaji kazi.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mhe. Franco Kiswaga, akifanya utambulisho wa watumishi waliohudhulia katika kikao.
Mmoja ya watumishi akiwasilisha hoja wakati wa kikao hicho.
Picha ya pamoja na Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo.
Picha ya pamoja na Maafisa utumishi Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni, Mahakama ya Wilaya Kinondoni, Mahakama ya Wilaya Ilala, Mahakama ya Wilaya Kigamboni, Mahakama ya Wilaya Ubungo na Mahakama ya Wilaya Temeke.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni