- Rais, Mhe. Dkt. Samia ampongeza Mhe. Ndejembi kwa kushika wadhifa huo
- Amtaka Makamu wa Rais huyo kuwa tayari kujifunza
- Asema bidii, nidhamu, weledi na utayari vitamsaidia kutekeleza majukumu yake ipasavyo
Na MARY GWERA,
Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 29 Agosti, 2026 amemuapisha
Mhe. Deogratius John Ndejembi kuwa Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hafla ya Uapisho huo imefanyika katika Viwanja vya Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma na kushuhudiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Viongozi mbalimbali wa kitaifa akiwemo pia Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Waziri Mkuu wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, Mawaziri, Viongozi wengine na Wageni waalikwa mbalimbali.
Uteuzi na uapisho wa Mhe.
Ndejembi unakuja baada ya kujiuzulu kwa aliyekuwa Makamu wa Rais wa Tanzania,
Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi
tarehe 25 Agosti, 2026 ikiwa ni pamoja na kupitishwa na kuidhinishwa kwa
kauli moja ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Spika, Mhe.
Mussa Azzan Zungu, kufuatia pendekezo lililoridhiwa na Kamati Kuu pamoja na
Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Akizungumza mara baada ya
hafla hiyo, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amempongeza na kumpa pole Mhe.
Ndejembi kwa kupewa jukumu hilo kubwa katika umri wake mdogo, huku akibainisha kuwa,
uamuzi huo ulilenga kurudisha nafasi hiyo kwa vijana wenye nguvu, ari, na kasi
ya kujituma serikalini.
“Nitumie fursa hii
kukupa pole Mhe. Ndejembi katika umri mdogo tumekutwisha jukumu kubwa bila
kukushauri, lakini kipekee nivishukuru sana vikao vya Chama Cha Mapinduzi, Kamati
Kuu na Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi kwa kupendekeza na kuliridhia
jina la Mhe. Deogratius John Ndejembi katika nafasi ya Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na hii ni baada ya kuzingatia sifa na vigezo
alivyo navyo, ikiwa ni pamoja na umri wake, ambao kwa kweli bado ni kijana
mwenye nguvu, ari, na kasi ya kujituma na kutekeleza shughuli za Serikali. Kwa
kauli moja tuliamua nafasi ile tuirudishe kwa vijana na tuendelee kulea, imetoka
kwa kijana, tumeirudisha kwa kijana, sasa kijana tukuombe ukakue si kwa umri
lakini ukakue akili,” amesema Rais, Mhe. Dkt. Samia.
Aidha, Mhe. Dkt.
Samia amesema kuwa hana shaka na utendaji kazi wa Makamu wa Rais, Mhe.
Deogratius Ndejembi kwani kabla ya wadhifa huo alishika nafasi mbalimbali za
uongozi serikalini na sekta binafsi, hivyo, uzoefu huo utamsaidia katika
kutekeleza majukumu ya dhamana hiyo aliyopewa.
“Hakuna shule
inayosomesha Umakamu wa Rais, hakuna. Ila sifa zako za bidii, nidhamu, weledi,
na utayari wako wa kujifunza, kufuatilia, na kusimamia utekelezaji wa shughuli
mbalimbali zitakusaidia kutimiza majukumu hayo. Nakuhimiza neno kujifunza;
kujifunza ni pamoja na kusoma kwa wengine waliopo nawe,” amesisitiza.
Mambo makuu
aliyoyasisitiza Rais Samia kwa Makamu wa Rais mpya ni pamoja na Ukuaji wa
Kiakili na Nidhamu, kuwa na bidii,
nidhamu, weledi na utayari wa kujifunza kutoka kwa viongozi wengine na
waliotangulia.
Kadhalika, Mhe. Dkt.
Samia amemkumbusha Makamu wa Rais, Mhe. Ndejembi kutambua kuwa, cheo
alichopewa ni dhamana kutoka kwa Watanzania na sio ufalme, hivyo anapaswa
kuwatumikia wananchi wote bila ubaguzi au kujali tofauti zao.
“Nakusihi uweke
maanani kwamba cheo ni dhamana. Cheo hiki tulichokupa si ufalme; ni
dhamana. Dhamana uliyopewa na Watanzania kupitia Chama Kikuu kinachoongoza
Dola, Chama Cha Mapinduzi, na kupitia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa hiyo nenda ukawatumikie bila kujali tofauti zao,” amesisitiza Rais Samia.
Vilevile amemsisitiza kuwa
na Uzalendo na Uadilifu kwa kutekeleza majukumu kwa utii, uaminifu, utu,
busara, hekima na maarifa huku akimtanguliza Mwenyezi Mungu mbele.
Mbali na hayo, Rais, Mhe.
Dkt. Samia amezungumzia kuhusu Utekelezaji wa Mipango ya Maendeleo: Kazi
kubwa ya kusimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM pamoja na Dira ya Taifa ya
Maendeleo, 2050.
“Tunayo mambo mengi tuliyoahidi kupitia Ilani ya Chama chetu ya mwaka 2020-2025 na kwenda mbele 2030. Aidha, kama unavyofahamu, tumeanza utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya miaka 25 inayokuja, ambayo imebeba matamanio na matarajio makubwa ya maendeleo kwa wananchi wetu," amesema.
Ameongeza kuwa, ili kutekeleza yote hayo kwa maslahi
yanayostahili wananchi na taifa kwa ujumla, wanahitaji umoja, mshikamano,
ushirikiano, utulivu, na uongozi bora na ushirikiano kwakuwa mambo hayo ni muhimu kuyazingatia katika utekelezaji majukumu na kuyafikia matamanio na matarajio ya
Watanzania.
Aidha, Rais Samia
amewashukuru Viongozi mbalimbali pamoja na Mabalozi na Wakuu wa Mashirika ya
Kimataifa waliohudhuria hafla hiyo, akieleza kuwa mahudhurio yao yanadhihirisha
amani, utulivu, na uimara wa Katiba na mifumo ya kisiasa ya Tanzania katika
kuendesha mabadiliko ya uongozi kwa amani bila misukosuko.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akimuapisha Mhe. Deogratius John Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo tarehe 29 Agosti, 2026 katika Viwanja vya Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma. Anayeshuhudia katikati ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

.jpg)

.jpg)












Hakuna maoni:
Chapisha Maoni