Jumanne, 10 Oktoba 2017

MAHAKAMA KUU KANDA YA ARUSHA YAMALIZA MASHAURI YALIYOSAJILIWA JANUARI MPAKA AGOSTI MWAKA HUU



Na Lydia Churi- Mahakama, Arusha
Mahakama Kuu Kanda ya Arusha imefanikiwa kusikiliza na kumaliza kwa zaidi ya asilimia tisini mashauri yaliyofunguliwa katika kipindi cha mwezi Januari hadi Agosti mwaka huu.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu kanda ya Arusha Mhe. Angelo Rumisha, jumla ya mashauri 737 kati ya 805 yaliyosajiliwa kuanzia mwezi Januari hadi Agosti 2017, yamemalizika.

Alisema haya ni mafanikio ya kuridhisha kwa Mahakama Kuu kanda ya Arusha ambapo kila Mhe. Jaji amesikiliza na kumaliza wastani wa mashauri 245. Hivi sasa, Mahakama Kuu kanda ya Arusha ina jumla ya majaji watatu.

Katika kuhakikisha inaondokana na mlundikano wa mashauri kwenye Mahakama mbalimbali nchini, Mahakama ya Tanzania ilipanga idadi ya mashauri yatakayosikilizwa na Majaji na Mahakimu. Kwa mujibu wa mpango huo, kila Jaji anatakiwa kumaliza mashauri yasiyopungua 220 kwa mwaka na hakimu Mashauri 250.

Akifafanua takwimu za mashauri, Naibu Msajili alisema hadi kufikia Agosti 31, mwaka huu, Mahakama hiyo imebakiwa na mashauri 809 ambapo  kati ya mashauri hayo, 788 yana umri wa kati ya miaka 1-2, mashauri 17 yana umri kati ya miaka 3-5, mashauri 2 yana umri kati ya miaka 5-10 na mashauri mengine 2 yana umri wa zaidi ya miaka 10.

Alisema mashauri yote yenye miaka 10 na zaidi ni yale yaliyorudishwa kutoka Mahakama ya Rufani baada ya kikao cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kilichofanyika April mwaka huu.

Akizungumzia Mahakama za Hakimu Mkazi na za Wilaya kwa Mikoa ya Arusha na Manyara, Mhe. Rumisha alisema jumla ya mashauri 223 yana umri zaidi ya miezi 12, kati ya mashauri hayo, ni mashauri mawili tu ndiyo ambayo Mahakama zina mamlaka nayo ikiwa ni sawa na asilimia 1.3 ya mashauri yote yenye umri zaidi ya miezi 12 hivyo mashauri mengi ya mlundikano ni yale ambayo Mahakama hazina mamlaka nayo.
 Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Arusha Mhe. Sekela Moshi




 Naibu Msajili wa Mahakama Kuu kanda ya Arusha Mhe. Angelo Rumisha



Wakati huo huo, Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Arusha Mhe. Sekela Moshi amesema hivi sasa kanda yake imeanza kutekeleza Mikakati iliyojipangia ya kuondoa mashauri yote yenye muda mrefu Mahakamani.

Akiitaja mikakati hiyo, Kaimu Jaji Mfawidhi alisema tangu Oktoba 2 mwaka huu, kanda ya Arusha imekuwa ikifanya vikao vya kumaliza mashauri ya zamani ya madai ambapo mpango huo unatarajiwa kukamilika Oktoba 13, 2017.  

Alisema baada ya kukamilika kwa mkakati huo, kanda yake itaanza mkakati mwingine uliopangwa na Mahakama ya Tanzania wa kumaliza mashauri ya zamani chini ya mradi wa Benki ya Dunia unaotarajiwa kuanza Oktoba 16 na 17 mwaka huu. 

Alisema kanda ya Arusha ina mashauri ya zamani machache hivyo wanatarajia ifikapo Novemba  14, 2017 mashauri yote ya muda mrefu yatakuwa yamemalizika.

Wananchi wakiwa Mahakama Kuu kanda ya Arusha kwa ajili ya kupatiwa huduma za kimahakama.
Ofisi Maalum ya Malalamiko ya Mahakama Kuu kanda ya Arusha. Ofisi hii pamoja na nyingine zilizopo kwenye kanda ya Arusha hupokea wastani wa malalamiko 14 katika kipindi cha mwezi mmoja.
Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Edward Mbara akiwa ofisini kwake leo jijini Arusha.
Kwa mujibu wa Mtendaji, kanda ya Arusha imejiwekea mikakati ya kupambana na changamoto zilizopo ikiwa ni pamoja na kuzungumza na wadau wengine wa Haki ili kuona namna bora ya kuondoa mashauri ya muda mrefu mahakamani. Hatua hii itahusisha polisi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa mashauri ambayo Mahakama za chini hazina mamlaka nayo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni