Ijumaa, 13 Oktoba 2017

MAHAKAMA YASHAURIWA KUELIMISHA JUU YA MATUMIZI SAHIHI YA SIMU ZA MALALAMIKO



Na Lydia Churi-Mahakama, Manyara
Mahakama ya Tanzania imeshauriwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya matumizi sahihi ya namba za simu zilizotolewa kwa ajili ya wananchi kuwasilisha malalamiko yao kwa Mahakama pamoja na mapambano dhidi ya rushwa.

Akizungumza jana mjini Babati mkoani Manyara, Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoani humo, Jacob Swalle alisema upo umuhimu wa kuwaelimisha wananchi zaidi juu ya matumizi sahihi ya simu hizo kwa kuwa wengi wao wanazitumia kwa kupiga badala ya kutuma ujumbe.

Alisema licha ya changamoto za simu hizo, mabango yaliyosambazwa yenye namba hizo yamesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza malalamiko kwa wale  wanaotumia kwa usahihi.
  Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Manyara, Jacob Swalle

Kuhusu utekelezaji wa Mpango Mkakati wa miaka mitano wa Mahakama ya Tanzania, Mtendaji huyo alisema wanajitahidi kutekeleza nguzo zote tatu ili wananchi wapate haki kwa wakati. Alisema hivi sasa nakala za hukumu zinatoka kwa wakati.

Alisema ili kujenga taswira chanya kwa Mahakama, wamekuwa wakifanya vikao vya mara kwa mara na watumishi ili kukumbushana majukumu yao ya kutekeleza Mpango Mkakati ikiwa ni pamoja na umuhimu wa kuhudumia wateja vizuri na kufuata maadili
Kuhusu mikakati ya kuondosha mashauri ya muda mrefu Mahakamani, Bwana Swalle alisema wamekuwa wakifanya vikao na wadau pamoja na kuondoa changamoto zinazochelewesha kesi kumalizika mahakamani. Aidha, wamekuwa  wakiomba Mahakimu kutoka Arusha kusaidia kumaliza kesi kwa haraka. 

Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa wa Manyara inakabiliwa na changamoto za upungufu mkubwa wa watumishi kama Mahakimu, Makarani, wahudumu na walinzi. Mahakama hiyo hivi sasa ina hakimu moja tu.

Mahakama ya Tanzania ilianza kutekeleza Mpango Mkakati wa miaka mitano  pamoja na Mradi wa Maboresho ya Huduma za Mahakama tangu mwaka 2015 kwa lengo la kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili Mahakama ya Tanzania katika kutekeleza jukumu lake la msingi na la kikatiba la kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati.
   Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Manyara, Mhe. Devotha Kamuzora
   Jengo la Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Manyara likiwa katika hatua za mwisho
 Jengo la Mahakama ya Wilaya
  Jengo la Mahakama ya Mwanzo Karatu lililomalizika hivi karibuni

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni