Jumanne, 23 Januari 2018

JAJI MKUU ATAKA MAHAKAMA ISIINGILIWE MAMLAKA YAKE YA KIKATIBA

Na Lydia Churi
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewakumbusha na kuwasihi viongozi wote wa Serikali wenye mamlaka za kikatiba na kisheria kubaki ndani ya maeneo yao ya kikatiba na kujiepusha kuingilia maeneo yaliyo ndani ya Haki, Hadhi na Mamlaka ya Kikatiba ya Mahakama.

Akizungumza leo jijini Dar es salaam Jaji Mkuu amesema kuwa Mahakama haitasita kumchukulia hatua mtu yeyote atakayeingilia Mamlaka ya Kikatiba ya Mhimili huo. Pia amewakumbusha Majaji na Mahakimu kuhakikisha wanalind a hadhi na uhuru wa Mahakama kwa kuwachukulia hatua wale wanaovunja amri halali za Mahakama.

“Niwakumbushe kwamba anayelinda hadhi na uhuru wa Mahakama ni Hakimu, Jaji na Mahakama husika, kama umetoa amri unaona kuna mtu anaivunja, mwite na kumuuliza kwa nini asichukuliwe hatua”, alisisitiza Jaji Mkuu.

Akitolea mfano wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Prof. Juma alisema Mhimili huo unapoingili wa Mamlaka yake ya kikatiba, muhusika huitwa mbele ya kamati, kuhojiwa na kuchukuliwa hatua, hivyo aliwataka Mahakimu na Majaji nao kuchukua hatua kwa yeyote atakayeingilia Mhimili wa Mahakama. 

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza na Waandishi wa Habari leo jijini Dar es salaam. Wa pili kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Ferdinand Wambali na wa pili kulia ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Hussein Kattanga. Wa kwanza kushoto ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Katarina Revokati na wa kwanza kulia ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Ilvin Mugeta.  

“Nawakumbusha wananchi na viongozi mbalimbali nje ya Mahakama kuwa kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania, mamlaka ya Utoaji haki ni ya Mahakama tu”, alisema.
Alisema Sheria ndiyo inayoipa nguvu Mahakama na kutaka kila Mhimili kubakia kwenye eneo lake na Mamlaka yake ili kusiwepo na migongano.Aliongeza kuwa kuanzia sasa Majaji na Mahakimu watakuwa wakali kwa yeyote atakayeingilia uhuru wa Mahakama.

“Mahakama haiingilii Mamlaka aliyopewa mwinginekama vile Mamlaka ya Polisi, Mwendesha Mashitaka, Takukuru ama Taasisi nyingine yeyote, Hakimu au Jaji hawezi kuingilia, hivyo tunawataka waliopewa Mamlaka yao wabaki huko waliko, na tukifanya hivyo hatutakuwa na migongano yoyote,” alisema Jaji Mkuu.

Naye Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Ferdinand Wambali alisema kasi ya usikilizwaji wa mashauri katika Mahakama za ngazi zote nchini ni ya kubwa. Alisema Mahakama imefanikiwa kupunguza idadi ya hukumu ambazo bado hazijatolewa.

Alisema mwaka 2017 wakati wa kuanza kwa mwaka wa Mahakama, kulikuwa na jumla ya hukumu 880 ambazo hazijatolewa lakini hivi sasa kuna hukumu 440 ambazo bado hazijatolewa lakini muda wa kutoa hukumu hizo bado haujamalizika. Baada ya shauri kumaliza kusikilizwa hukumu inapaswa kutolewa  ndani ya siku 90.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza na Waandishi wa Habari leo jijini Dar es salaam. Kushoto ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Ferdinand Wambali. 
 
 Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Ferdinand Wambali akizungumza na Waandashi wa Habari leo jijini Dar es salaam. Kushoto Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Katarina Revokati.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni