Jumanne, 23 Januari 2018

RAIS MAGUFULI KUWA MGENI RASMI SIKU YA SHERIA


Na Lydia Churi 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli anatarajiwa kuwa mgeni Rasmi kwenye kilele cha Maadhimisho ya wiki ya Sheria na siku ya Sheria nchini yatakayofanyika Februari Mosi mwaka huu katika viwanja vya Chimala jijini Dar es salaam.

Aidha, maadhimisho ya siku ya Sheria nchini yatatanguliwa na Maonesho ya Wiki ya Sheria yatakayoanza Januari 27 hadi 31. Maonesho hayo yatazinduliwa rasmi na RaisMstaafu wa awamu ya nne Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete siku ya Jumapili Januari 28 mwaka huu. Kabla ya uzinduzi huo, Dkt. Kikwete ataongoza Matembezi maalum ya kuadhimisha wiki ya Sheria yatakayoanzia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mpaka viwanja vyaMnazi Mmoja jijini Dar es salaam.

Akizungumzia Maadhimisho hayo, Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma aliwaambia Waandishi wa Habari leo jijini Dar es salaam kuwa Mahakama ya Tanzania imedhamiria kutoaElimu kwa Umma kuhusu dhana ya Usuluhishi kwa kumaliza migogoro kabla ya kuipeleka migogoro hiyo Mahakamani (Alternative Dispute Resolution)pamoja na dhana ya matumizi ya TEHAMA katika Mahakama nchini.

Alisema Mahakama itatumia siku hizo tano kutoa elimu ya sheria na Msaada wa kisheria kwa wananchi. Aidha, wiki hiyo ya Elimu ya Sheria pia itatumika kuwajengea wananchi uelewa na uwezo wa kusuluhisha mashauri kwa maridhiano bila kupitia mkondo wa kimahakama.

Mahakama itahakikisha kuwa wananchi watakaohudhuria wanapata fursa ya kutosha ya kupata uelewa wa kazi za wadau na kupewa ufafanuzi kuhusu mashauri mbalimbali.
Alizitaja huduma zitakazotolewa kuwa ni taratibu za ufunguaji wa mashauri katika ngazi za Mahakama kuanzia Mahakama za Mwanzo hadi Mahakama ya Rufaa pamoja na kituo cha usuluhishi wa Migogoro, taratibu za kesi za Mirathi, vyeti vipya vya Mawakili, pamoja na Msaada wa kisheria.

Huduma nyingine zitakazotolewa kwenye wiki ya elimu ya sheria ni pamoja na kushughulikia malalamiko kuhusu kuchelewa kwa kesi za jinai na ya wadaawa ambao kesi zao zimechelewa, kushughulikia mashauri ya muda mrefu na kutoaElimu kwa Umma kwa ujumla.

Kwa mujibu wa JajiMkuu, katika wiki ya Sheria na siku ya Sheria kutakuwa na ushiriki wa wanafunzi na waalimu kutoka shule kadhaa za sekondari, washauri wa wanafunzi (Dean of Students) kutoka Chuo kikuu cha Dar es salaam, Chuo kikuu Mzumbe, Chuo kikuu cha Ruaha Iringa pamoja na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza na Waandishi wa Habari leo jijini Dar es salaam. Mhe. Jaji Mkuu alikuwa akizungumzia Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na kilele cha siku ya Sheria nchini.
  
Alisema lengo la kuwashirikisha wanafunzi katika Maadhimisho hayo ni kuwajengea misingi ya maadili mema naufahamu wa umuhimu wa Mahakama katika kusaidia kuendeleza Amani ya nchi, utulivu na umoja wa taifa.

Mwaliko huo maalum kwa wanafunzi unaashiria mwanzo wa ushirikiano baina ya Mhimili wa Mahakama na wanafunzi ili kuwajenga kwenye msingi wa maadili na kuchukia vitendo vya rushwa.

Jaji Mkuu pia ametoa rai kwa wananchi na wadau wote wa sheria nchini kutembelea Maonesho ya wiki ya Sheria ili kujifunza na kupata huduma mbalimbali za kisheria kutoka kwa waheshimiwa Majaji, Mahakimu, Wasajili, Watendaji, Mawakili wa Serikali na Mawakili wa kujitegemea ambaowatakuwa tayari kuwasikiliza na kuwahudumia.

Aidha, wadau wakuu katika wiki ya Sheria watakaotoa huduma kwenye Maonesho hayo ni Mahakama ya Zanzibar, Tume ya Utumishi wa Mahakama, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka, Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa vitendo (Law School of Tanzania) na Tume ya Kurekebisha Sheria.

Wadau wengine ni Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS), Taasisi zinazotoa msaada wa kisheria (Legal Aid), TAKUKURU, Polisi, Magereza na Mkemia Mkuu wa Serikali.
 
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Katarina Revokati akizungumza wakati wa Mkutano na Waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam. Wa kwanza kulia ni Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akifuatiwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Ferdinand Wambali.
  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni