Jumatatu, 21 Januari 2019

MAAFISA UGAVI NA WAJUMBE WA BODI YA ZABUNI YA MAHAKAMA YA TANZANIA WAPATIWA MAFUNZO


Na Mary Gwera, Mahakama-Morogoro

Mahakama ya Tanzania inaendelea kutoa Mafunzo kwa Watumishi wake wa Kada mbalimbali ili kuwajengea uwezo zaidi katika utendaji kazi na vilevile kwenda sambamba na kasi ya maboresho ya utoaji huduma yanayoendelea kufanyika ndani ya Mhimili huo.

Akifungua Mafunzo ya Menejimenti ya Ununuzi na Usimamizi wa Mikataba (Procurement and Contract Management PCM), yanayofanyika katika Ukumbi wa Magadu Mkoani Morogoro mapema Januari 21, Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Jaji Dkt. Paul Kihwelo alisema kuwa Mafunzo hayo ni muhimu kwani ni sehemu pia ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama.

“Mafunzo haya ni muhimu katika kuboresha utendaji kazi, hatuwezi kuimba wimbo wa Maboresho Mahakamani bila kuwawezesha Wataalam ambao wanachangia katika maboresho hayo,” alieleza Mhe. Jaji Dkt. Kihwelo.

Aidha Mkuu huyo wa Chuo alisema kuwa, Mafunzo hayo yanatolewa kwa Maafisa hao ikiwa suala la manunuzi ni nyeti na linachukua nafasi kubwa katika utekelezaji wa Mradi wa Maboresho wa huduma za Mahakama (CCP) ambapo kupitia mradi huo kuna ujenzi wa Mahakama mbalimbali, ununuzi wa Vifaa vya TEHAMA na kadhalika.

“Vitu vingi vinahitaji ununuzi, hivyo ni vyema Maafisa hawa na Wajumbe wa Bodi ya Zabuni kuongeza ujuzi zaidi katika usimamizi wa mikataba inayohusiana na masuala ya ununuzi ili kuepuka hoja zisizokuwa na msingi,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mwezeshaji ambaye pia ni Mkufunzi kutoka chuo cha ESAMI-Arusha, Bw. Felix Kamau alisema kuwa Mafunzo hayo yana faida kubwa kwani Washiriki wakifanya kazi kwa kuzingatia taratibu za manunuzi kwa ufasaha itasaidia kuondoa hoja zinazoibuliwa.

“Mbali na hilo, uandaaji wa mikataba kwa usahihi, unawezesha pia kuondoa nyongeza za kazi ‘variations’ ambazo kwa asilimia kubwa huongeza gharama katika miradi mbalimbali hatimaye Taasisi kuingia katika gharama zilizopo nje ya bajeti husika,” alieleza Bw. Kamau.

Naye, Mwenyekiti wa Bodi ya Zabuni ya Mahakama ambaye pia ni Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji-Mahakama ya Tanzania, Bw. Mathias Mwangu alisema kuwa Mafunzo haya ni muhimu kwani asilimia kubwa ya Bajeti, kwa maana ya bajeti ya Matumizi, ya kawaida na ya Maendeleo inahusisha Ununuzi.
 “Hoja nyingi za Ukaguzi za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali zinatokana na udhaifu katika menejimenti ya Mikataba, ukiukwaji wa Sheria, Kanuni na taratibu za Ununuzi, hivyo mafunzo yataongeza maarifa zaidi ya jinsi ya kukabiliana na mapungufu hayo,” alieleza Bw. Mwangu.
Mafunzo hayo ya siku tano (5) ambayo yameandaliwa na Mahakama ya Tanzania kupitia Chuo cha Uongozi wa Mahakama kwa kushirikiana na ESAMI yamehusisha jumla ya Washiriki 40 kutoka Kanda mbalimbali za Mahakama nchini.
Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Jaji Dkt. Paul Kihwelo akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya Menejimenti ya Ununuzi na Usimamizi wa Mikataba (Procurement and Contract Management PCM).
Mwezeshaji kutoka ESAMI, Bw. Felix Kamau akitoa Mada katika Mafunzo hayo.


Sehemu ya Washiriki wa Mafunzo wakifuatilia kinachojiri katika Mafunzo hayo.
 Mkufunzi kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Bw. Lameck Samson Lushoto akizungumza jambo katika Mafunzo hayo.
Washiriki wa Mafunzo wakiwa kazi za vikundi ‘group discussions.’  
Picha ya pamoja meza kuu na baadhi ya Wajumbe wa Bodi: Katikati ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Jaji, Dkt. Paul Kihwelo, kushoto ni Mwezeshaji kutoka ESAMI, Bw. Felix Kamau, kulia ni Mkurugenzi Msaidizi, Rasilimali Watu ambaye pia ni Mjumbe wa Bodi ya Zabuni ya Mahakama, Bi. Agatha Ng’ingo, waliosimama (katikati) ni Mwenyekiti wa Bodi ya Zabuni ya Mahakama, Bw. Mathias Mwangu, kushoto ni Mjumbe wa Bodi, Mhe. Amir Msumi na kushoto ni Mjumbe wa Bodi, Mhe. Warsha Ngh’umbu.
Picha ya pamoja, meza Kuu, baadhi ya Wajumbe wa Bodi pamoja na Maafisa Ugavi wanaoshiriki katika Mafunzo hayo. Maafisa hao wametoka Mahakama Kuu Masjala Kuu, Kanda ya Songea, Tanga, Arusha, Dodoma, Iringa, Mwanza, Shinyanga na Divisheni zote za Mahakama Kuu ya Tanzania.

(Picha na Mary Gwera, Mahakama)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni