Ijumaa, 3 Julai 2020

UWEZO WA KUSIKILIZA MASHAURI YA JINAI WAFIKIA ASILIMIA 105.06

Na Magreth Kinabo na Innocent Kansha - Mahakama

Jumla ya mashauri ya jinai 24,698 yalifunguliwa katika ngazi mbalimbali za Mahakama nchini na kati ya hayo, mashauri 25,950, sawa na asilimia 105.06 ya mashauri yote yaliyofunguliwa yalisikilizwa na kumalizika kati ya mwezi Januari na Julai Mosi, mwaka huu.

Mkurugenzi wa Menejimenti ya Usimamizi wa Mashauri wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Deusdedith Kamugisha alisema mashauri hayo yalifunguliwa katika ngazi mbalimbali za Mahakama kuanzia Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu pamoja na Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za wilaya nchini kati ya mwezi Januari na Julai Mosi mwaka huu . 
Akitoa taarifa ya uendeshaji  wa mashauri hayo kwenye kikao kazi cha robo  mwaka ya pili ya mwaka wa  kimahakama cha mwaka huu kilichohusisha wadau wa Kamati ya Kitaifa ya  Haki Jinai alisema Mahakama hivi sasa ina uwezo wa kusikiliza mashauri yote yanayoingia mahakamani ili kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati.

‘‘Taarifa hii inaelezea hali ya ufunguaji na usikilizaji wa mashauri ya jinai kwa kipindi cha Januari hadi Julai Mosi, 2020 kwa Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu, Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya nchi nzima.“Kwa upande wa Mahakama ya Rufani Tanzania, jumla ya mashauri ya jinai 297 yalifunguliwa na mashauri 210 yalisikilizwa sawa na asilimia 70.7 ya mashauri yote yaliyofunguliwa katika kipindi hicho,’’ alisema Kamugisha huku akisema wastani wa mzigo wa mashauri ni 737 kwa jopo la majaji wa tatu.

Alisema Mahakama Kuu ya Tanzania, mashauri ya jinai 2,561 yalifunguliwa na 2,618 yalisikilizwa sawa na asilimia 102.2. Wastani wa mzigo wa mashauri ni  345 kwa kila Jaji wa Mahakama     Kuu  ya Tanzania.

Kamugisha alisema katika Mahakama za Hakimu Mkazi jumla ya mashauri 5,338 yalifunguliwa, 5,566 yalisikilizwa sawa na asilimia 104.3 ya mashauri ya jinai yaliyofunguliwa. Hivyo wastani wa mzigo wa mashauri ni  198 kwa kila Hakimu.

“Mahakama za Wilaya mashauri 16,169 yalifunguliwa, mashauri 17,254 yalisikilizwa sawa na asilimia 97.5.Hadi kufikia Julai Mosi, 2020 wastani wa mzigo wa mashauri kwa Mahakama za Wilaya ni 96 kwa kila Hakimu,”alisisitiza
.
Aliongeza kwamba  mashauri 333 yalifungiliwa katika Mahakama za Watoto, 302 yalisikilizwa sawa na asilimia 90.6.

Kwa upande wa ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai    nchini, ambayo imewakilishwa na Naibu Kamishna wa Polisi Bw.Saleh Ambika alieleza kuwa lengo kuu la ofisi yake ni kuhakikisha upelelezi wa makosa ya jinai unafanyika na unakamilika kwa haraka zaidi kadri iwezekanavyo.

“Upelelezi wa makosa ya jinai una hatua mbalimbali na unahusisha taasisi mbalimbali za mfumo wa haki jinai kuna wakati mwingine Polisi wanahitaji kupata ripoti zinazotoka mamlaka nyingine kukamilisha upelelezi ili kumfikisha mtuhumiwa mahakamani kwa wakati,” alisema Ambika.

Alifafanua kuwa upelelezi unaohusisha sampuli za kitu fulani, Kitengo cha Upelelezi lazima kishirikiane na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali wakatiKmwingine sio rahisi kupata ripoti kwa kadri ya matarajio ya upelelezi wako, pia taasisi hiyo inataratibu zake za kiuchunguzi ili kukamilisha hilo,

Ambike alisema ushirikiano wadau hao upo kwa kiwango cha kutosha, hivyo hilo ndio lengo la kamati hiyo ni  kuisaidia Mahakama ya Tanzania kufikia ajenda ya kupunguza mlundikano wa mashauri mahakamani. 

Mkurugenzi Msaidizi  kutoka Idara ya Huduma za Uangalizi kwa wafungwa wanaotumikia vifungo vya nje ya Magereza, Bw. Charles Nganze alisema wafungwa 706 walitumikia adhabu mbadala ya kufanya usafi wa mazingira kwenye maeneo ya Makaburi ya Kinondoni, mabwawa ya Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) , wizara na zahanati mbalimbali.

Naye  Kamishna Msaidizi wa Magereza, Bw,Willington Kamuhuza, alishukuru jitihada zilizofanywa na wadau hao zimesaidia kupunguza msongamano wafungwa kwa asilimia 0.73.Pia  aliongeza kwamba kwa kutumia  Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) jumla ya mikoa 16 iliyo na magereza mashauri hayo yamesikilizwa kwa njia ya Mahakama Mtandao baada ya kuwezeshwa kuwa na vifaa vya TEHAMA kutoka Mahakama ya Tanzania.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Uondoshaji wa Mashauri ya Jinai, ambaye pia ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania,  Mhe. Sharmillah Sarwatt alisema  lengo kikao hicho ni  kutathmini utendaji  kazi  na kupanga  mikakati ya kupunguza mlundikano wa mashauri  ya aina hiyo.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Uondoshaji wa Mashauri ya Jinai ambaye pia ni Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Sharmillah Sarwatt (kushoto) na Katibu wa kikao hicho Naibu Msajili  Mwandamizi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe Messe Chaba (kulia).

Mkurugenzi wa Menejimenti ya Usimamizi wa Mashauri Mahakama ya Tanzania, Mhe. Deusdedith Kamugisha akitoa taarifa leo ya uendeshaji wa mashauri ya jinai  katika kipindi cha Januari, mwaka huu hadi Julai Moi, mwaka huu kwenye kikao kazi cha robo mwaka ya pili ya mwaka wa  kimahakama cha mwaka huu kilichohusisha wadau wa Haki Jinai.
Mwakilishi kutoka katika ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai    nchini (DCI), ambayo imewakilishwa na Naibu Kamishna wa Polisi. Bw.Saleh Ambika akifafanua jambo.


 Kamishna Msaidizi wa Magereza, Bw,Willington Kamuhuza,(kushoto) akizungumza jambo kwenye kikao hicho. (Kulia ) ni Mkurugenzi wa Menejimenti ya Usimamizi wa Mashauri Mahakama ya Tanzania, Mhe. Deusdedith Kamugisha.
Baadhi ya wadau hao wakiwa katika kikao hicho.






Hakuna maoni:

Chapisha Maoni