Jumamosi, 24 Oktoba 2020

SIMAMIENI MAADILI KULINDA HESHIMA YA MAHAKAMA: JAJI KIONGOZI

 Na Lydia Churi- Mahakama, Geita

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt.  Eliezer Feleshi amewataka watumishi wa Mahakama kusimamia maadili wanapotekeleza majukumu yao ya kila siku ili kutoa huduma bora kwa wananchi na kulinda heshima ya Mhimili huo.

Akizungumza kwa nyakati tofauti na Watumishi wa Mahakama za wilaya za Bukombe na Chato mkoani Geita, Jaji Kiongozi pia amewataka watumishi hao kufanya kazi kwa kushirikiana na kupendana wao kwa wao na wadau wote wa Mahakama wakiwemo wananchi wanaofika mahakamani kutafuta haki zao.

“Simamieni maadili ya kazi zenu, tuwe na ushirikiano mwema sisi wenyewe Pamoja na wadau wa Mahakama”, alisistiza Jaji Kiongozi.

Katika kuboresha utendaji kazi, Jaji Kiongozi aliwashauri watumishi wa Mahakama kujiendeleza kielimu ili wawe na uwezo wa kufanya kazi Zaidi ya moja. Aidha, aliwataka watumishi hao kujifunza na kuifahamu vizuri Taasisi wanayofanyia kazi.

Watumishi wapatiwe mafunzo/ ujuzi mbalimbali ili kuwawezesha kutekeleza vema majukumu yao ya kila siku. Alisema watumishi wa kada za chini mara nyingi wamekuwa wakisahaulika kupatiwa mafunzo hivyo ameutaka uongozi wa Mahakama kuhakikisha watumishi hao pia wanapatiwa mafunzo ya kuboresha utendaji kazi wao.  

Kuhusu usikilizwaji wa mashauri, Dkt. Feleshi amewataka Majaji na Mahakimu kusikiliza mashauri kwa haraka na ikiwezekana wasikilize hata siku ya Jumamosi ili kuondoa msongamano wa mashauri mahakamani. Alisema mashauri yanayopaswa kupewa kipaumbele ni yale ambayo watuhumiwa wake hawana dhamana ili kuondoa msongamano magerezani.

Jaji Kiongozi amewasisitiza Mahakimu kuhakikisha wanamaliza kwa haraka  mashauri hususan ya Mirathi na yale ya Ndoa. “Mashauri ya Ndoa yana athari kubwa kwa familia hasa Watoto, lakini pia mashauri ya Mirathi nayo yanaathiri Watoto yatima, Wajane na Wagane hivyo hayana budi kumalizika kwa wakati”, alisisitiza Jaji Kiongozi.

Akizungumza katika ofisi za wakuu wa wilaya za Bukombe na Chato, Jaji Kiongozi  amelishauri jeshi la polisi kuharakisha kufanya upepelezi ili mashauri yamalizike kwa wakati.

“Polisi harakisheni upelelezi, yapo mashauri yanayosubiri polisi kumaliza upelelezi na Mkurugenzi wa Mashtaka kutoa vibali”, alisema Dkt. Feleshi.

Alisema Mahakama imejiwekea mikakati ya kumaliza mashauri kwa wakati ikiwemo Majaji na Mahakimu kupangiwa idadi ya mashauri wanayopaswa kumaliza katika kipindi cha mwaka moja. Majaji wanatakiwa kusikiliza mashauri 220 na Mahakimu mashauri 250.

Jaji Kiongozi amemaliza ziara yake ya siku tano ya kikazi katika Kanda ya Mwanza ambapo alikagua shughuli za utendaji kazi katika Mahakama za wilaya za Nyamagana, Ilemela, Misungwi, Kwimba, Magu, Ukerewe na Sengerema. Jaji Kiongozi pia alitembelea Mahakama za wilaya za Bukombe, Chato Geita pamoja na Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt.  Eliezer Feleshi akishuka kwenye Kivuko akitoka Mkoani Geita kwenye ziara ya Ukaguzi baada ya kumaliza. Nyuma yake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Mwanza Mhe. Sam Mpaya Rumanyika. 


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt.  Eliezer Feleshi (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Mahakama wa kanda Mwanza na Makao Makuu ya Mahakama Kuu baada ya kumaliza kuzungumza na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Bukombe.  
Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Bukombe wakimsikiliza Jaji Kiongozi alipokuwa akizungumza nao.  
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt.  Eliezer Feleshi akizungumza na atumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Bukombe 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni