Jumamosi, 19 Desemba 2020

WATAYARISHENI WAHITIMU KUFANYA KAZI KWA KUTUMIA TEHAMA: JAJI MKUU

 Na Lydia Churi-Mahakama, Lushoto

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amekitaka Chuo cha Uongozi wa Mahakama- Lushoto kuwatayarisha wahitimu wake kufanya kazi kwa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) kwa kuwa Mhimili huo unajiimarisha katika Teknolojia ili kuondokana na matumizi ya karatasi.

Akizungumza wakati wa Mahafali ya Ishirini ya Chuo hicho ambapo alikuwa ni Mgeni rasmi, Jaji Mkuu alisisitiza umuhimu wa Chuo hicho kutoa wahitimu watakaoweza kumudu matumizi ya Tehama kutokana na mabadiliko makubwa katika karne ya 21 yanayogusa nafasi ya Mahakama katika utoaji wa haki, hasa ulazima wa matumizi hayo kama nyenzo wezeshi katika utoaji wa haki.

Nawasihi mboreshe matumizi ya Tehama katika kufundishia Astashahada na Stashahada ili kuweza kupata faida katika Teknolojia hiyo inayokua kwa kasi sana”, alisema Jaji Mkuu.

Alisema wahitimu wa chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto hawana budi kwenda sambamba na Mapinduzi makubwa yanayoendelea katika matumizi ya Tehama katika huduma za kimahakama ikiwemo ulazima wa kufahamu namna Kanuni za ufunguaji wa mashauri kwa njia ya kielekitroniki zinavyotumika kila siku.

Prof. Juma alisema ingawa Uongozi wa Mahakama ya Tanzania uliamua kuwa matumizi ya Tehama si hiyari tena bali ni lazima ili Mhimili uweze kutoa huduma zake kwa ufanisi zaidi, lakini bado matumizi ni madogo kulinganisha na uwekezaji mkubwa uliofanyika hadi sasa.

Alikitaka Chuo hicho kujiimarisha ili kitoe mafunzo kwa watumishi wa Mahakama kwenye eneo la Utoaji haki Mtandao (migration to e-judiciary, e-justice). Alisema ni muhimu kwa Chuo hicho kutoa watumishi walioiva katika matumizi ya Tehama ili kuendana na uwekezaji mkubwa uliofanyika kwenye eneo hilo la Teknolojia.

Akimnukuu Rais wa Awamu ya Tatu Hayati Benjamin William Mkapa katika Utangulizi aliouandika kwenye Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 (Tanzania Development Vision 2025), Prof. Juma alisema Hayati Mkapa alitoa picha ya ushindani kwa wanaohitimu katika hii Karne ya 21, hivyo wahitimu hao wajiweke kwenye utayari wa kushindana katika  ushindani uliotajwa na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 na watarajie kufanya kazi na kuishi katika Karne ambayo imejipambanua kwa ushindani.

“Wenye Astashahada na Stashahada watakaoshinda ni wale tu ambao wataonyesha uwezo mkubwa ki-teknolojia, uzalishaji wenye tija, uwezo wa kujisomea kila siku na kujiongezea maarifa, na wenye ujuzi wa hali ya juu wanaoweza kufanya udhubutu kwenye maamuzi”, alisisitiza Jaji Mkuu.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo hicho, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald Ndika amewataka wahitimu wa chuo hicho kutambua kuwa elimu waliyoipata ni mwanzo wa safari ya kupata elimu ya juu kutokana na kukua kwa utandawazi.

“Ni vizuri mkajua kwamba ni wajibu wenu kuendeleza kujifunza mbinu mpya za kuyakabili mabadiliko yanayotokana na utandawazi” alisema Jaji Ndika.

Wakati huo huo, Mkuu wa Chuo hicho ambaye pia ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Paul Kihwelo aliwaasa wahitimu kuishi katika misingi ya maadili waliyofundishwa chuoni hapo.

“Kuna mambo ya msingi ya kitabia ya kuyaishi na kuyapa hadhi yake stahiki katika maisha yenu yote. Siku zote muishi maisha ya uadilifu”, alisema.  

Mahafali ya ishirini ya chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto yaliambatana na kilele cha sherehe za kutimiza Miaka Ishirini tangu kuanzishwa kwa chuo hicho Oktoba 22 mwaka 2000. Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania Mhe. Barnabas Albert Samatta alizindua rasmi shughuli za masomo tarehe 6 Disemba 2000 na Rais wa Awamu ya Tatu, Hayati Benjamin William Mkapa alizindua rasmi chuo hiki tarehe 3 Machi 2001.

 

Wahitimu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama- Lushoto wa Astashahada wakiwa kwenye Maandamano tayari kwa kuanza kwa sherehe za Mahafali yao. Haya ni Mahafali ya 20 ya chuo hicho tangu kuanzishwa kwake.

Wahitimu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama- Lushoto wa Stashahada wakiwa kwenye Maandamano tayari kwa kuanza kwa sherehe za Mahafali yao. Haya ni Mahafali ya 20 ya chuo hicho tangu kuanzishwa kwake.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (kushoto) ambaye pia alikuwa ni Mgeni Rasmi kwenye Mahafali ya 20 ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto akiwa kwenye Maandamano tayari kwa kuanza kwa sherehe za Mahafali hayo.

Wahitimu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama- Lushoto wa Astashahada wakiwa kwenye sherehe za Mahafali yao. Haya ni Mahafali ya 20 ya chuo hicho tangu kuanzishwa kwake.
Wahitimu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama- Lushoto wa Stashahada wakiwa kwenye sherehe za Mahafali yao. 
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza wakati wa  sherehe za Mahafali yao. Haya ni Mahafali ya 20 ya chuo hicho tangu kuanzishwa kwake.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akikabidhiwa Zawadi na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto Jaji Mhe. Dkt. Gerald Ndika wakati wa sherehe za Mahafali ya 20 ya chuo hicho.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni