Ijumaa, 26 Februari 2021

MAHAKIMU WATAKIWA KUELIMISHA WANANCHI SHERIA NA TARATIBU ZA MAHAKAMA

Na Lydia Churi- Mahakama

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma ametoa wito kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo kuwaelimisha wananchi sheria na taratibu za kimahakama ili kuongeza uelewa wa masuala ya sheria kwa watanzania.

Akizungumza mara baada ya kuwaapisha Mahakimu wakazi 70 leo jijini Dar es salaam, Jaji Mkuu amewataka Mahakimu hao kuwasaidia wananchi kuelewa taratibu zote zinazohusu mashauri yaliyo mahakamani.

Tusiwaachie wadaawa waondoke mahakamani bila kujua hatua mbalimbali ambazo shauri litapitia hadi kukamilika” alisema Jaji Mkuu.

Alisema katika nchi yenye changamoto ya wananchi wengi kutofahamu sheria na taratibu za kimahakama kama ilivyo kwa Tanzania; Mahakimu na Majaji wanao wajibu mkubwa wa kuelimisha Umma.

Kuhusu masuala ya maadili, Jaji Mkuu amewataka Mahakimu hao kufanya kazi kwa uadilifu kwa kuwa wao ni nguzo muhimu ya utawala wa sheria na wamepewa mamlaka ya mwisho kwa mujibu wa Ibara ya 107A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika utoaji haki.

Alisema kiapo walichoapa Mahakimu hao kinawakumbusha Ibara ya 107B ya katiba  ambayo imetambua Uhuru wa Mahakimu katika kutoa haki bila ya kuingiliwa na mamlaka nyingine.

Aidha amewashauri Mahakimu walioapishwa kuhakikisha wanasoma na kuzielewa Sheria zote zinaosimamia uendeshaji wa mashauri ya Mahakama za Mwanzo ikiwa ni pamoja na kujua pale Sheria inapofanyiwa marekebisho.

Amesema ili wawe Mahakimu bora na wa kutegemewa wanapaswa kufanya utafiti wa kutosha kabla ya kuandika hukumu au kutoa maamuzi ya mashauri watakayosikiliza. “Someni pia maamuzi ya Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani yaliyowekwa kwenye mfumo wa kuhifadhi mashauri (TANZLII).

Katika kuhakikisha mashauri hayakai kwa muda mrefu mahakamani, Jaji Mkuu amewataka Mahakimu hao kutoa hukumu kwa wakati. Alifafanua kuwa katika Mahakama za Mwanzo mashauri yanapaswa kumalizika ndani ya miezi sita na endapo litabaki mahakamani kwa zaidi ya muda huo, itakuwa ni mlundikano wa mashauri.

Wakati huo huo, Prof. Juma amewataka Mahakimu kutoruhusu Mawakili kuchelewesha mashauri kwani kwa kufanya hivyo husababisha kuwepo kwa mlundikano wa mashauri katika Mahakama za Mwanzo. Aliwataka pia Mawakili wasitumike kuzuia usuluhishi kwa kuwa usuluhishi ni takwa la katiba.

Kuhusu rushwa na maadili, Mahakimu hao wametakiwa kujiepusha na vitendo hivyo pamoja na mazingira yeyote yanayoweza kupelekea wananchi kukosa imani na Muhimili wa Mahakama.

Jumla ya Mahakimu wakazi 70 waliapishwa leo na kufanya idadi ya Mahakimu walioapishwa ndani ya wiki moja kufikia 140.

Baadhi ya Mahakimu Wakazi wakila kiapo mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani) leo katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es salaam. Jumla ya Mahakimu 70 waliapishwa. 
Baadhi ya Mahakimu Wakazi wakila kiapo mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani) leo katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es salaam. Jumla ya Mahakimu 70 waliapishwa. 

Baadhi ya Mahakimu Wakazi wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza leo katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es salaam. Jumla ya Mahakimu 70 waliapishwa. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni