Jumamosi, 4 Septemba 2021

WATUMISHI WA MAHAKAMA WATAKIWA KUTOA HUDUMA ZINAZOENDANA NA UBORA WA MAJENGO YA SASA

Na Lydia Churi- Mahakama, Moshi

Watumishi wa Mahakama ya Tanzania wametakiwa kutoa huduma bora kwa wananchi zinazoendana na ubora wa majengo ya Mahakama yaliyojengwa na yanayoendelea kujengwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Akizungumza na Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Arusha, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka watumishi hao kuzingatia maadili na weledi na kutoa huduma bora kwa Watanzania ili haki iweze kupatikana kwa wakati.

“Tumejenga majengo sita ya vituo Jumuishi vya Utoaji haki katika miji ya Dodoma, Morogoro, Mwanza na hapa Arusha kwa lengo la kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi hivyo huduma mnazotoa ni lazima ziendane na uzuri wa majengo haya” alisema.

Aliwataka watumishi wa Mahakama kuzingatia mambo matano muhimu wanapotekeleza majukumu yao ya kila siku. Prof. Ole Gabriel aliyataja mambo hayo kuwa ni kutobaguana kwa namna yoyote, kuacha uvivu na uzembe, kutojihusisha na vitendo vya rushwa na ukosefu wa maadili, pamoja na kutochelewesha mashauri mahakamani pasipokuwa na sababu za msingi.

Aidha, Mtendaji Mkuu pia aliwasisitiza watumishi wa Mahakama Kuu kanda ya Arusha kuongeza kasi kwenye matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha utendaji kazi, kuongeza uwazi katika mnyororo wa utoaji haki na kukabiliana na changamoto ya upungufu wa watumishi wa kada mbalimbali.

“Mahakama inakabiliwa na upungufu wa watumishi 10,320 wa kada mbalimbali hivyo matumizi ya Tehama yatasaidia kupunguza changamoto hiyo kwa kiasi kikubwa. Hivi sasa Mahakama ina jumla ya watumishi 5,835 kwa nchi nzima”alisema Prof. Ole Gabriel.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania anaendelea na ziara yake ya kukagua miradi ya ujenzi wa majengo ya Mahakama na kuungumza na watumishi wa Mahakama kwa lengo la kujitambulisha. Tayari amekagua ujenzi wa jengo la makao makuu ya Mahakama, Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki vilivyopo Dodoma na Arusha pamoja na majengo ya Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za wilaya yaliyopo Dodoma, Manyara na Arusha.

 

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kamda ya Arusha wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel alipozungumza nao wakati wa ziara yake kwenye kanda hiyo . Lengo la ziara hiyo ni kujitambulisha kwao na kutoa maelekezo ya utendaji kazi.

Jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki lililomalizika kujengwa jijini Arusha  

Watumishi wa Mahakama Kuu ya Tanzania kamda ya Arusha wakiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (Mbele katikati) mara baada ya kuzungumza wakati wa ziara yake kwenye kanda hiyo 

Muonekano wa ndani wa Jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki lililomalizika kujengwa jijini Arusha  
Muonekano wa ndani wa Jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki lililomalizika kujengwa jijini Arusha  
 Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akisikiliza maelezo ya ijenzi kutoka kwa Mkandarasi.
  Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akitazama ramani ya Jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki  kilichopo jijini  Dodoma.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni