Alhamisi, 29 Septemba 2022

MSAJILI MKUU ATAKA HUDUMA BORA ZITOLEWE KWA WANANCHI

Na Faustine Kapama – Mahakama.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma amewasihi wajumbe wa menejimenti ya Mahakama kuboresha utendaji na kuacha kufanya kazi kwa desturi na mazoea ya awali ili wadau wa ndani na wananchi kwa ujumla wapate huduma zilizo bora.

Mhe. Chuma alitoa wito huo jana tarehe 28 Septemba, 2022 alipokuwa anafunga mafunzo ya siku tatu kuhusu uongozi bora kwa wajumbe hao kutoka kurugenzi, vitengo na idara mbalimbali yaliyokuwa yanayofanyika katika Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki cha Masuala ya Familia Temeke jijini Dar es Salaam.

“Rai yangu kwenu ni kwamba, ushiriki wenu na tija ya mafunzo haya udhihirishwe katika ubora wa huduma mtakazokuwa mnatoa kwa umma na kwa watumishi wenzenu. Kwa kuzingatia mada zilizotolewa ni matumaini yangu kuwa tutaishi na kushirikiana vyema na watumishi walio chini yetu pamoja na viongozi kwa ujumla,” alisema.

Msajili Mkuu huyo aliwaomba wajumbe hao wa menejimenti kila siku kukumbuka na kujiuliza kwa namna gani wanawasaidia wale waliopo chini au juu yao katika utendaji wao wa kazi ili kufikia malengo ya taasisi, kwa maana ya Mhimili wa Mahakama.

Kadhalika, Mhe. Chuma aliwasihi kutoa ushauri, maoni na mapendekezo kwa uongozi wa Mahakama yenye mlengo wa kutatua changamoto mbalimbali katika uendeshaji wa shughuli za Mahakama. “Kazi yako kubwa kama kiongozi ni kuondoa vikwazo na kutatua changamoto na siyo kuwa sehemu ya tatizo. Tafuta majibu ya tatizo,” aliwaambia wajumbe hao.

Amesema kufanyika kwa mafunzo hayo kumekuwa chachu ya kuboresha uendeshaji wa shughuli za Mahakama katika Kurugenzi, Idara, Vitego na sehemu mbalimbali wanazofanyia kazi. Mhe. Chuma alisema kuwa ni matarajio ya uongozi wa Mahakama kuwa mafunzo hayo yamewaongezea ufanisi wa kazi ya msingi ya kutoa haki kwa wakati na kwa watu wote.

“Ni imani yangu kuwa mafunzo haya mahususi yamewaongezea ujuzi na weledi katika huduma ya utoaji haki kwa wakati kama inavyoelezwa na Dira ya Mpango Mkakati wetu. Aidha, ni imani yangu kuwa mafunzo haya yamewawezesha kuwa na uelewa wa pamoja katika maeneo (mbalimbali),” alisema.

Msajili Mkuu huyo aliwakumbusha washiriki wa mafunzo maneno yaliyowahi kusemwa na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo aliyoyasema tarehe 30 Aprili, 2021 wakati wa ufunguzi wa sehemu ya mafunzo chuoni hapo.

Alimnukuu Mhe. Dkt. Kihwelo akisema, “Haitoshi tu kuhudhuria mafunzo na kupata cheti. Inafaa zaidi ukipata mafunzo ukayatumie kwa ubora uliokusudiwa kwako wewe na kwa maafisa wengine wa Mahakama na kuleta mabadiliko chanya pamoja na kwamba mabadiliko wakati mwingine yana maumivu yake…...”

Awali, akitoa taarifa kwa ufupi kuhusu mafunzo hayo, Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu alimweleza Msajili Mkuu kuwa katika kipidi hicho cha siku tatu, wajumbe wa menejimenti wapatao 34 walipitishwa katika maeneo mbalimbali, ikiwemo utamaduni wa Mahakama ya Tanzania na fikra za kimkakati.

Bi. Ngungulu alitaja maeneo mengine yaliyoguswa wakati wa mafunzo hayo yaliyoanza tarehe 26 Septemba, 2022 ni namna ya kuhimili mihemuko, huduma ya wateja katika muktadha wa Mahakama, itifaki na utii, muundo wa Serikali na utawala wake, uongozi na maadili yake, usimamizi wa ofisi, uandishi wa taarifa, uwianisho wa taaluma na utu na udhibiti wa msongo wa mawazo na masuala ya kisaikolojia.

“Kwa mada hizi (washiriki wa mafunzo haya) walizojifunza, ni imani yetu sisi Sekretarieti na Kurugenzi ya Utawala na Rasilimali Watu kuwa tumejifunza, hatutoki kama vile tulivyokuja, tunatoka na kitu. Pengine kila mmoja wetu atajitahidi kukitumia kile alichojifunza hapa katika kuboresha utendaji wa kazi,” alisema.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma akisistiza jambo alipokuwa anafunga mafunzo ya wajumbe wa menejimenti ya Mahakama.
Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki cha Masuala ya Familia, Mhe. Ilvin Mugeta akieleza jambo wakati wa kufunga mafunzo hayo.
Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu akitoa taarifa fupi namna mafunzo hayo yalivyoendeshwa.

Mmoja wa washiriki, Bi. Glady Qambaita akitoa neno la shukurani kwa uongozi wa Mahakama kwa kuwezesha uwepo wa mafunzo hayo

Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo (juu na chini) wakifuatilia hotuba iliyokuwa inatolewa na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma (hayupo katika picha).


Sehemu nyingine ya washiriki wa mafunzo hayo (juu na chini) wakifuatilia jambo.



Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Secretarieti. 
Meza kuu ikiwa katika picha ya pamoja na washiriki wote wa mafunzo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni