Alhamisi, 29 Septemba 2022

MWENYEKITI TUME YA KUREKEBISHA SHERIA ATEMBELEA UJENZI WA MAHAKAMA KUU TABORA

Na Amani Mtinangi – Mahakama, Tabora

Mwenyekiti wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mstaafu, Mhe. January Msoffe jana tarehe 28 Septemba, 2022 alitembelea mradi wa ukarabati na upanuzi wa jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tabora.

Lengo la ziara ya Mhe. Msoffe, ambaye aliambatana na viongozi wa Mahakama Kuu Tabora ilikuwa kujionea hatua za maendeleo za mradi huo unaotekelezwa na Kampuni ya M/S CRJE (East Africa) LTD katika Manispaa ya Tabora ambao kwa sasa upo katika hatua za mwisho.

Baada ya kutembelea na kupatiwa maelezo kuhusu utekelezaji wa mradi huo, Mwenyekiti wa Tume hiyo alipongeza na kusifu kazi kubwa na nzuri inayoendelea kufanywa na timu ya Mkandarasi akishirikiana na Wakala wa Majengo Tanzania na Mahakama ya Tanzania.

Mhe. Msoffe alijionea mabadiliko makubwa yaliyofanyika ukilinganisha na kipindi cha nyuma wakati akija kusikiliza mashauri ya Mahakama ya Rufani. Aliongeza kuwa ubunifu mzuri umeliwezesha jengo hilo kukidhi mahitaji ya watumishi na wadau wote wa Mahakama kama ilivyo kwenye majengo mengi ya kisasa yanayojengwa na Mahakama.

Naye Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tabora, Mhe. Amour Khamis alisema kuwa mradi huo utakapomalizika na kuanza kutumika utawezesha watumishi, wadau na wateja kuwa na mazingira mazuri ya kufanyia kazi na kupokea huduma tofauti na ilivyokuwa awali.

Alisema kabla ya ukarabati na upanuzi huo kulikuwa na uhaba wa vyumba, ufinyu wa ofisi na kukosekana kwa mifumo thabiti ya usalama wa jengo na watumiaji wake. Mhe. Amour aliushukuru uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kuwezesha utekelezaji wa mradi huo.

Akitoa maelezo ya utangulizi kwa Mwenyekiti wa Tume hiyo kwa niaba ya Mshauri Mwelekezi wa Mradi, ambaye ni Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Mbunifu Majengo, Bw. Malimi Masala alisema mifumo yote inayohitajika imezingatiwa ili kulifanya jengo hilo kuwa rafiki kwa watumiaji wote hata wenye mahitaji maalum.

Kwa upande mwingine Mhandisi Majengo kutoka TBA Goodluck Sanga alisema kuwa mradi huo uliopo katika hatua za mwisho unatekelezwa kwa kuzingatia mahitaji yote muhimu ya kimahakama, afya ya watumiaji na usalama wa jengo kama uwepo wa mifumo ya TEHAMA, umeme, mifumo ya kuzimia moto, maji na pia mandhari nzuri kwa kuweka bustani za majani.

Kaimu Mtendaji wa Mahakama, Kanda ya Tabora, Bw. Ginaweda Nashon alieleza kuwa Mahakama Kuu Tabora itakuwa tayari kulipokea jengo hilo baada ya mifumo muhimu kukamilika na kufanya kazi ipasavyo. Alisema baadhi ya samani za ofisi zipo njiani na utengenezaji wa mapazia unaweza kukamilika muda wowote kuanzia sasa.

Akahimiza kukamilika kwa shughuli zote muhimu ili jengo hilo lianze kutumika. Mradi huo ambao ulianza kutekelezwa tarehe 16 Julai, 2021 unatarajia kumalizika na kukabidhiwa hivi karibuni tayari kwa watumizi.

Mwenyekiti wa Tume ya Kurekenisha Sheria Tanzania, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mstaafu, Mhe. January Msoffe akisaini katika kitabu cha wageni alipotembelea mradi wa ukarabati na upanuzi wa Mahakama Kuu Tabora.
Muonekano kwa mbele wa jengo la Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tabora.

Mbunifu Majengo Malimi Masala (wa kwanza kushoto) akitoa maelezo kuhusu maendeleo ya mradi. Katika picha ni Mhandisi Majengo kutoka TBA Goodluck Sanga (wa pili kushoto), Mwenyekiti wa Tume ya Kurekebisha Sheria nchini, Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. January Msoffe (wa tatu kushoto), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amour Said Khamis (wa nne kushoto), Jaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Tabora, Mhe. Bahati alema (watano kushoto) na Afisa TEHAMA, Bw. Nestory Peter Kurwa (kulia).


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni