Jumatano, 12 Oktoba 2022

MAHAKAMA SPORTS BABA LAO

·Waichapa RAS Simiyu tano ikiingia nusu fainali

·Wakubali mziki wao hauchezeki

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Timu ya Mahakama Sports Mpira wa Miguu Wanaume leo tarehe 12 Octoba, 2022 imeingia katika hatua ya nusu fainali kwa kishindo kikubwa baada ya kuigaragaza RAS Simiyu kwenye mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa.

Mahakama Sports iliichapa Timu ya RAS Simiyu mabao 5:1 katika mechi ya robo fainali baada ya kutandaza kabumbu safi na la kuvutia. Mchezo huo umevuta hisia za washiriki wengi wa SHIMIWI kufuatia mizengwe iliyokuwa imesababishwa na Timu ya Uchukuzi hapo awali.

Mchezo huo ambao umechezwa kuanzia majira ya saa tatu asubuhi ulianza kwa kasi huku timu zote mbili zikishambuliana kwa zamu. RAS Simiyu walikuwa wa kwanza kulisalimia lango la Mahakama katika dakika za mwanzo mwanzo, lakini bao hilo lilikataliwa kutokana na mfungaji kuwa katika nafasi ya kuotea.

Baada ya kuingia kwa bao hilo, Mahakama Sports wakachachamaa na kulisakama lango la wapinzani wao mara kwa mara. Winga machachari wa Mahakama Sports Shamte Seif alifungua kalamu ya magori kwa timu yake katika dakika ya 10 ya mchezo baada ya kuukwamisha mpira katika nyavu kufuatia pasi ya upendo kutoka kwa Mshambuliaji hatari Martin Mapinduzi.

Dakika nne baadaye, Mshambuliaji huyo aliweka mpira kwenye kamba baada ya kupokea pasi mpenyezo kutoka kwa Kiungo wa Juu Gabriel Tabana na kuiandikia timu yake bao la pili.

Pamoja na magori hayo, Mahakama Sports iliendelea kutandaza kandanda safi na kushambulia lango la RAS Simiyu kama nyuki na kufanikiwa kupata bao la tatu katika dakika ya 31 ya mchezo kupitia Frank Obadia aliyepokea pasi nyororo kutoka kwa mshambuliaji Martin Mapinduzi.

Hadi timu zote mbili zinaenda katika mapunziko, ubao wa matokeo ulikuwa unasomeka 3:0. Kipindi cha pili kilipoanza, RAS Simiyu walilishambulia lango la Mahakama kwa dakika za mwanzo na kufanikiwa kupachika bao baada ya mabeki kutoka timu pinzani kujichanganya.

Kuingia kwa bao hilo kuliwaamsha wachezaji wa Mahakama na kuanza kumiriki mpira na kucheza pasi fupi fupi zilizowachanganya wapinzani wao. Katika dakika ya 54, Frank Obadia aliingia tena kwenye nyavu baada ya kupachika bao safi kufuatia pasi ya upendo kutoka kwa Kiungo Gabriel Tabana.

Mahakama Sports ilizidisha mashambulizi kila wakati na kuwafanya wapinzani wao kukata pumzi na kupoteana, hatua iliyowapa mwanya mwingine wachezaji wa Mahakama kutumia udhaifu wa RAS Simiyu kupachika bao la tano na la mwisho kwa mchezo huo kutoka kwa mshambuliaji Martin Mapinduzi.

Katika vipindi vyote viwili, timu zote zilifanya mabadiliko ya wacgezaji, ambayo yaliinufaisha Mahakama Sports ambo waliweza kupata mabao mawili katika kipindi cha pili.

Hadi mwamuzi anapuliza kipenga cha kumaliza mpambano huo, matokeo ya mchezo huo yalikuwa yanaonyesha 5:1 kwa Mahakama na RAS Simiyu, mtawaliwa. Kufuatia ushindi huo, Mahakama Sports itamenyana na Timu ya Ulinzi katika hatua ya nusu fainali.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Katibu wa Mahakama Sports Robert Tende amewapongeza wachezaji wote kwa kujituma na kuipigania timu kwa ujumla ili ipate matokeo mazuri. Amewaomba wachezaji hao kuendelea kujipanga kwa mechi inayofuata kwani hatua waliyofikia siyo mchekea.

Kwa upande wake, Mwalimu wa Timu hiyo Spear Mbwembwe aliwataka wachezaji kukaza uzi zaidi, kwani safari bado haijaisha. Amewatumia salamu wapinzani wao wanaokuja kuwa kazi inaendelea.

“Ndugu yangu, suala lilotuleta Tanga ni kuchukua kombe, kwa hiyo bado hatujamaliza. Nadhani vijana wangu wameanza kunielewa sasa. Kuna mtu atapigwa nyingi hapa, mtashangaa. Tunamsubiri huyo anayekuja naye apate zake, hatuna kitu kingine sisi,” alisema.

Wachezaji wa Mpira wa Miguu walioiwakilisha Mahakama katika mchezo huo walikuwa Fahamu Kibona; Iman Patson; Gisbert Chentro; Akida Mzee; Emmanuel Mwamole; Selemani Magawa; Frank Obadia; Gabriel Tabana; Martin Mpanduzi; Mwinjuma Bwanga, Shamte Seif, Hassan Aufi; Nassoro Mwampamba; Kelvin Rutalemwa; Shabiru Hood; David Mnubi; Beatus Simwanza na Timoth Mwakisambwe.

Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa Shaibu Kanyochole.

Mashindano ya SHIMIWI ambayo yalianza tarehe 1 Octoba, 2022 na kufunguliwa rasmi tarehe 5 Octoba, 2022 yanafanyika katika viwanja tofauti tofauti ikiwemo Viwanja vya Mkwakwani, Shule ya Sekondari Popatlal, Galanos Sekondari, Bandari, Shule ya Tanga, Polisi Chumbageni na Viwanja vya Gymkhana kwa kuhusisha michezo kadhaa.

Timu ya Mahakama Sports Mpira wa Miguu Wanaume.


Mchezaji wa Timu ya Mahakama Sports akimiriki mpira.
Mchezaji wa Timu ya Mahakama Sports akiusindikiza mpira kwenye nyavu.
Mwamuzi wa mchezo huo akionyesha ishara ya kupeleka mpira katikati ya uwanja baada ya Timu ya Mahakama Sports kupachika bao.
Wachezaji wa Timu ya Mahakama Sports wakilisakama lango la wapinzani wao.

Mwalimu wa Timu ya Mahakama Sports  Spear Mbwembwe kiongea na wachezaji wakati wa mapumziko.

Wachezaji wa Timu ya Mahakama Sports (juu na chini) wakishangilia baada ya kupachika bao huku mlinda mlango wa RAS Simiyu akidaka panzi kwenye lango lake.



Benchi la Ufundi, wachezaji wa akiba na viongozi wa Timu ya Mahakama Sports Mpira wa Miguu Wanaume wakifuatilia kinachoendelea kwenye dimba.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni