Jumatano, 12 Oktoba 2022

MAHAKAMA SPORTS KAMBA WANAUME, WANAWAKE ZATINGA FAINALI KIBABE MASHINDANO SHIMIWI

·Baada ya kuwafumua Mambo ya Ndani, Waziri Mkuu Sera

·Wapinzani wapoteana, kila mmoja aondoka na njia yake

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake na Wanaume leo tarehe 12 Octoba, 2022 zimetinga katika hatua ya fainali baada ya kuzichakaza vibaya timu za Mambo ya Ndani na Waziri Mkuu Sera katika mchezo wa nusu fainali kwenye mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa.

Mahakama Sports Wanawake ilifikia hatua ya nusu fainali baada ya kuwanyoa RAS Iringa, huku Kamba Wanaume wakifika katika hatua hiyo baada ya kushinda rufaa yake dhidi ya Timu ya Uchukuzi ambayo ilichezesha mamluki kwenye robo fainali.

Ilikuwa mchezo wa Kamba Wanawake ulioanza kuchezeshwa majira ya saa moja asubuhi katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagala ambapo Mahakama Sports waliwakaba koo Waziri Mkuu Sera kila mbinu waliyotumia. Mchezo huo mzuri wa nusu fainali ulianza kwa Waziri Mkuu Sera kuwavizia Mahakama Sports ili waweze kuwatoa kwenye mchezo.

Hata hivyo, Mahakama Sports ambao walionekana kuwa na stamina na nguvu za kutosha walisimama imara na kufanikiwa kuwagalagaza wapinzani wao katika mzunguko wa kwanza.

Mzunguko wa pili ulipoanza Mahakama Sports hawakuwa na mjadala na mtu ambapo Waziri Mkuu Sera alikamuliwa mara moja na kuachwa hawana cha kufanya zaidi ya kujisalimisha na kuwaacha Mahakama Sports wakiondoka na ushindi.

Baada ya mchezo huo, Kamba Wanaume ilifuata ambapo Mambo ya Ndani walianza kwa kasi kwa kuwavuta Mahakama lakini kabla ya kupata ushindi kibao kikawageukia ambapo Mahakama Sports iliwapigisha kwata kwa mvuto mmoja na kujikuta wanalamba nyasi katika mzunguko wa kwanza.

Katika mzunguko wa pili, Mahakama Sports haikutoa nafasi yoyote kwa wapinzani wao kujitutumua na haikuchukua muda wakaumaliza mchezo huo bila kumhurumia mtu yoyote ambapo walitoa kichapo cha maana kwa Mambo ya Ndani na kuwafanya wapinzani hao kupoteana na baadaye kuondoka katika uwanja kila mmoja na njia yake.

Kwa matokeo hayo, Timu ya Mahakama Sports imetinga fainali ambapo Kamba Wanaume itakutana na Ikulu, ambao katika hatua ya makundi walikipata cha moto, huku Kamba Wanawake wakikutana na Uchukuzi.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema bado hawajamaliza kwani lengo lao walilojiwekea ni kuchukua ubingwa.

"Tunatambua wapinzani wetu walijaribu kutuzuia kwa kuchezesha mamluki baada ya kuwawashia moto mkali, lakini sisi hatuzuiliki. Yoyote atakayekuja mbele yetu atapokea kichapo na siku ya fainali kichapo kitakuwa kikali zaidi. Ikulu tunawajua, tuliwachapa kwenye makundi na kwenye fainali watapata haki yao," alisema.

Wachezaji wa Kamba Wanawake ni Zahara Abdallah, Beatrice Dibogo, Judith Mwakyalagwe, Melina Mwinuka, Dotto Mlandula, Rebecca Mwakabuba, Salma Mwamende, Sarafina Mkumbo, Mariam Mayala, Zawadi Amir, Namweta Mcharo, Valeria Ntyangili, Anna Hebron, Lucy Mbwaga, Rose Mwalongo na Tumaini Kizito.

Katika mchezo wa Kamba Wanaume, Mahakama Sports inawakilishwa na Leonard Kazimzuri, Yuda Mgalla, Patrick Mundwe, Denis Kipeta, Joseph Chokela, Mjuni Denis, Komba Mussa, Mochiwa Marko, Abdul Mumini, Mushi Martin, Magesa Phabian, Emmanuel Datsan, Robert Oguda, Rajab Mwaliko, Fidelis Choka na Exavery Kasembe.

Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa Shaibu Kanyochole.

Bendera ya Mahakama ya Tanzania ikipepea katika Mashindano ya SHIMIWI Tanga.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake ikijiandaa kuwashughulikia Waziri Mkuu Sera.

Timu ya Waziri Mkuu Sera ikijiandaa kukamuliwa na Mahakama Sports.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake (juu) ikiwashughulikia Timu ya Waziri Mkuu Sera (chini) ambao walilamba tamu chini na baadaye kusambaratika.

Wababe wa Kamba wakiondoka eneo la tukio baada ya kumshughulikia mtu. 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume ikijiandaa kwa mapambano na Mambo ya Ndani.



Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume (juu) ikiwashughulikia Wizara ya Mambo ya Ndani (chini) na baadaye kuwasambaratisha kabisa(chini)

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) (juu na chini) ikishangilia baada ya wapinzani wao kugeuzwa mdebwedo.


Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume ikipokea mapokezi ya kibingwa katika Viwanja vy Shule ya Sekondari ya Popatlal baada ya ushindi huo.























Hakuna maoni:

Chapisha Maoni