Jumatano, 12 Oktoba 2022

MAGWIJI WA KUCHEZESHA MAMLUKI SHIMIWI WAKWAMA MAHAKAMANI

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Mbinu za Timu ya Uchukuzi kuikwamisha Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume kushiriki mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) zimegonga mwamba.

Hatua hiyo inatokana na uamuzi wa Kamati ya Rufani ya SHIMIWI kuikubali rufaa iliyowasilishwa na Mahakama Sports kupinga ushindi waliopata Uchukuzi kwenye mchezo huo kwa kuchezesha mamluki, yaani watu wasio na sifa ya kushiriki mashindano hayo.

Katika rufaa hiyo, Mahakama Sports iliwasilisha sababu za rufaa tano, ikiwemo mmoja wa waamuzi waliochezesha mchezo huo kuwa mwajiriwa wa Uchukuzi na baadhi ya wachezaji hawana sifa za kushiriki mashindano ya SHIMIWI.

Sababu zingine ilikuwa baadhi ya kadi za wachezaji wa Uchukuzi ziligushiwa, kutozingatiwa kwa kanuni za mchezo wa kamba na mwamuzi kuruhusu mchezaji aliyekatiwa rufaa ya kutokuwa mtumishi wa Wizara ya Uchukuzi kucheza wakati majibu ya rufaa bado hayajatolewa.

Wakati wa kusikiliza rufaa hiyo, uongozi wa Majakama Sports chini ya Mwenyekiti wake Wilson Dede uliunda timu ya wataaalamu ikiongozwa na  Mushi Martin kushughulikia rufaa hiyo ambayo ilijumuisha wanasheria nguli na maafisa utumishi waliobobea katika fani hizo.

Ilipofika wakati wa kusikiliza, Kamati ya Rufaa ilielekeza Mahakama Sports kuanza kuthibitisha sababu ya tatu, ambayo inahusu kugushi kwa kadi za wachezaji. Timu hiyo ya wataalamu iliwabana Uchukuzi vilivyo na kushindwa kufurukuta.

Baada ya kubanwa mbavu zote, kati ya wachezaji watatu waliolalamikiwa, mmoja alishindwa kabisa kuthibitisha uhalali wa utumishi wake. Mchezaji huyo alijaribu kujitutumua akaomba apewe muda wa kutosha kuwasilisha stakabathi ya mshahara.

Hata hivyo, timu ya Mahakama ikaanza kumwaga utalaamu wa matumizi Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) mbele ya Kamati na kuwaeleza kuwa stakabadhi hiyo inaweza kupatikana hata kwa njia ya mtandao kwa mtumishi kuweka namba yake ya cheki hata kwenye simu janja.

Baada ya kukabwa koo kila kona, Uchukuzi wakasalimu amri. Kutokana na hatua hiyo, Mahakama ikawa imethibitisha sababu hiyo ya kugushi kadi za wachezaji bila kuacha shaka yoyote kwa mchezaji huyo mmoja mamluki.

Timu hiyo ya Mahakama ilipoanza kuthibitisha sababu zingine kwa kuzingatia ushahidi mzito uliokusanywa, Mwenyekiti wa Kamati ya Rufaa akawasihi waiachie meza kwa vile sababu iliyothibitishwa ya kughushi inatosha kufikia uamuzi wa rufaa hiyo.

Kutokana na uamuzi huo, Uchukuzi ikanyang'anywa ushindi na Mahakama kufanikiwa kuchumpa hadi nusu fainali ambapo leo tarehe 12 Octoba, 2022 imepambana na Timu ya Wazara ya Mambo ya Ndani na kuitoa kamasi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Latifa Mansour aliitembelea kambi ya Timu ya Mahakama na kuwapa pole kufuatia misukosuko wanayopitia na kuwatia moyo. Aliwataka kuwa wavumilivu na kuendelea kudumisha nidhamu kama ilivyo desturi ya watumishi wa Mahakama.

Viongozi wa Mahakama Sports wamemtaarifu Jaji Mfawidhi huyo kuwa wachezaji wote wapo salama na wanazingatia taratibu zote za kambi na kuishi kwa nidhamu inayotakiwa. Wamemuhakikishia kuwa watazingatia maelekezo yake yote aliyoyatoa. 


Mwamba huyo na Mwanasheria Nguli Mushi Martin aliyeongoza Kamati Maalumu ya Mahakama ambayo iliwabana mbavu Uchukuzi mpaka wakasalimu amri.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Latifa Mansour (katikati aliyevaa kofia) akiwa katika picha ya pamoja na uongozi wa Mahakama Sports alipotembelea kambi ya Timu ya Mahakama.
Miamba ya mchezo wa kamba inayotisha. Usiyempenda amekuja sasa!


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni