·Kamba Wanaume yawakalisha RAS Singida
·Wanawake wanyunyiza, wakamua Maji
Na
Faustine Kapama-Mahakama, Tanga
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba
Wanaume na Wanawake leo tarehe 3 Octoba, 2022 imeendeleza wimbi la ushindi kwenye
mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI)
yanayofanyika jijini hapa baada ya kuwachakaza vibaya wapinzani wao, Timu za RAS
Singida Wanaume na Maji Wanawake.
RAS Singida wamepata kile walichokuwa wanakitaka baada
ya kukumbana na kibano kikali kutoka kwa magwiji hao wa mchezo wa kamba nchini
na kuwafanya waondoke kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari Usagala wakiwa
vichwa chini. Kipigo kama hicho kiliwakuta Maji baada ya kunyunyizwa na baadaye
kukamuliwa na Mahakama kwenye viwanja hivyo.
Mchezo huo ambao ulifanyika majira ya saa moja asubuhi
ulianza kwa kuwakutanisha Kamba Wanaume katika kundi A na iliwachukua muda mchache
kwa Mahakama Sports kuwapumlia wapinzani wao pumzi ya moto na kuwafanya
wasiamini kilichokuwa kinaendelea.
Alisikia mchezaji mmoja kutoka timu pinzani akihoji, “Hivi
nyinyi mnakula nini?” Kichapo cha mbwa mwizi kiliendelea katika hatua ya pili
ambapo RAS Singida walionekana kuchanganyikiwa baada ya kuvutwa mara moja na
kukubali yaishe, hivyo kuachia pointi zote tatu zikienda kwa mabingwa hao
watetezi wa mchezo huo.
Baada ya mchezo huo wa upande wa wanaume kumalizika,Kamba
Wanawake ulifuata kwa Mahakama Sports kuwakamua Maji ambao walionekana si
lolote si chochote baada ya kupokea kipigo kikali na kukubali kutiririsha maji
kwenye viwanja hivyo katika awamu zote mbili za mchezo.
Katika kipindi cha pili, Maji walijaribu kuwatunishia
misuri Mabingwa hao watetezi katika mchezo huo. Hata hivyo, haikuchukua hata nusu
sekunde wakanyosha mikono na kuamua kuachia pointi zote tatu kwende kwa
Mahakama Sports. “Acha washinde bwana, sisi hatuwawezi,” alisikika mchezaji
mmoja kutoka timu pinzani akisema.
Akizungumza katika viwanja hivyo baada ya kumalizika
kwa mchezo huo, Katibu Mkuu wa Mahakama Sports Robert Tende amesema kazi
inaendelea na bado mapambano yanaendelea. “Nikwambie kitu kaka, safari hii hatuna
utani na mtu. Wembe ni ule ule, ni ushindi mbele kwa mbele, hakuna kurudi
nyuma,” alisema.
Katika mchezo wa leo, Kamba wanaume iliwakilishwa na
Leonard Kazimzuri, Yuda Mgalla, Patrick Mundwe, Denis Kipeta, Joseph Chokela,
Mjuni Denis, Komba Mussa, Mochiwa Marko, Abdul Mumini na Mushi Martin, Magesa Phabian, Emmanuel Datsan, Robert Oguda,
Rajab Mwaliko, Fidelis Choka na Exavery Kasembe.
Kwa upande wa Kamba Wanawake wachezaji walikuwa
Beatrice Dibogo, Judith Mwakyalagwe, Merino Mwinuka, Dotto Mlandula, Rebecca
Mwakabuba, Salma Mwamende, Safina Mkumbo, Maria Mayala, Zawadi Amir, Namweta Mcharo, Valeria Ntyangili, Anne Hebron, Lucy Mbwaga na Rose
Mwalongo.
Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti
Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu
Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony
Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile.
Mashindano ya SHIMIWI ambayo yalianza jana tarehe 1
Octoba, 2022 yanatarajiwa kufunguliwa rasmi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassimu Majaliwa tarehe 5 Octoba, 2022. Kauli mbiu
ya mashindano ya SHIMIWI 2022 ni “Michezo hupunguza magonjwa yasiyo ambukiza na
kuongeza tija mahala pa kazi.”
Mashindano hayo ambayo yanashirikisha michezo
mbalimbali yatafanyika katika viwanja tofauti tofauti nane ambavyo ni Viwanja
vya Mkwakwani, Shule ya Sekondari Popatlal, Galanos Sekondari, Bandari, Shule
ya Tanga, Polisi Chumbageni na Viwanja vya Gymkhana.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume (juu) ikiwakalisha RAS Singida (chini).
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni