Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports)
Netiboli leo tarehe 2 Octoba, 2022 imeyaanza mashindano ya Shirikisho la
Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) kwa kutoa onyo kali kwa timu
pinzani baada ya kuwabamiza timu ya RAS Mtwara kwa vikapu 40:4.
Mchezo huo ambao umechezwa katika Viwanja vya Polisi
Chumbageni kuanzia majira ya saa 11 jioni ulianza kwa kasi huku Timu ya
Mahakama ikilisakama goli la wapinzani wao na haikuchukua muda ikaanza kutupia
vikapu.
Mchezo huo ambao ulichezwa kwa dakika 40 mara zote
uliegemea upande mmoja kufuatia umahiri wa wachezaji wa Mahakama ambao
walikuwa imara na walicheza kwa umahiri mkubwa.
Wachezaji wote walicheza kwa ushirikiano wa hali ya
juu na kulishambulia lango la wapinzani wao kwa mwendo wa karne ya 21, hivyo
kutupia tupia vikapu mara kwa mara.
Mwiba na nyota wa mchezo huyo walikuwa wachezaji wa Mahakama Sports Filomena Haule
na Upendo Matunda ambao kila dakika walikuwa wanatupia vikapu, kiasi cha mashabiki
wao kuwabatiza kwa jina la Mayele.
Mashabiki wa Timu ya RAS Mtwara waliojitutumua mwanzo kuwatia
moyo wachezaji wao walitokomea kusikojulikana baada ya Timu yao kugeuzwa
mdebwedo na Timu ya Mahakama ya Tanzania.
Hadi mwisho wa mchezo, Mahakama Sports ilishatupia
vikapu 40 huku RAS Mtwara wakiambulia vikapu vinne (4) tu na kwenda
kujiburudisha na korosho walizokuja nazo.
Akizungumza baada ya mechi hiyo, Mwalimu wa Timu
Mtumwa Sululu amesema siri ya ushindi huo ni vijana wake kucheza kitimu, kuwa
na nidhamu na kuzingatia programu aliyokuwa ameiweka.
"Nawapongeza sana vijana wangu kwa ushindi huu mnono. Tunajipanga kwa mechi inayokuja na niwahakikishie vipigo kama hivi vitaendelea," alisema.
Wachezaji walioiwakilisha Mahakama ni Filomena Haule, Upendo Matunda, Nyange Simola,
Veronica Kajobi, Diane's Akanganyila, Shani Ally, Tarita Kayuni. Wachezaji wa
akiba walikuwa Marikia Nondo, Margaret Kanyaga, Agnes Kilian,Jackline Paul,
Adeudata Mkonkosha.
Viongozi wa Mahakama Sports ambao wamerongozana na timu
mbalimbali ni Mwenyekiti Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu
Mkuu Robert Tende, Katibu Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab
Ally, Timu Meneja Antony Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile.
Mashindano ya SHIMIWI ambayo yalianza jana tarehe 1
Octoba, 2022 yanatarajiwa kufunguliwa rasmi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassimu Majaliwa tarehe 5 Octoba, 2022. Kauli mbiu
ya mashindano ya SHIMIWI 2022 ni “Michezo hupunguza magonjwa yasiyo ambukiza na
kuongeza tija mahala pa kazi.”
Mashindano hayo ambayo yanashirikisha michezo
mbalimbali yatafanyika katika viwanja tofauti tofauti nane ambavyo ni Viwanja
vya Mkwakwani, Shule ya Sekondari Popatlal, Galanos Sekondari, Bandari, Shule
ya Tanga, Polisi Chumbageni na Viwanja vya Gymkhana.
Wachezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Netiboli (juu na chini) wakijiandaa kutupia vikapu kwenye gori la RAS Mtwara.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni