Jumapili, 2 Oktoba 2022

BENDERA YA MAHAKAMA YAPEPEA SHIMIWI TANGA

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu Wanaume leo tarehe 2 Octoba, 2022 imeipeperusha vyema bendera ya Mahakama baada ya kuwachapa mabao 2-0 Timu ya Tume ya Utumishi katika mchezo wa kwanza hatua ya makundi kwenye mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa.

Mechi hiyo iliyochezeshwa kuanzia majira ya saa mbili asubuhi katika Viwanja vya Shule ya Sekondari ya Galanosi ilianza kwa timu zote mbili kusomana na kuusoma mchezo wote kwa ujumla, huku kukiwepo na mashambulizi ya hapa na pale.

Kulikuwepo na kosa kosa kadhaa katika kipindi cha kwanza ambapo Timu ya Mahakama ilikuwa ikilishambulia lango la wapinzani wao kama nyuki. Nayo Timu ya Tume ilipata mipira iliyokufa mara kadhaa kutokana na madhambi yaliyokuwa yanafanywa na wachezaji wa Mahakama.

Hata hivyo, timu hiyo ilishindwa kutumia nafasi hizo na kushindwa kupata mabao kutokana na umahiri wa walinzi na mdaka mishale wa Mahakama Sports. Hadi kipindi cha kwanza kinamalizika timu zote zilienda kwenye mapumziko zikiwa nguvu sawa.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi kwa timu ya Mahakama kulisakama lango la wapinzani wao. Mashambulizi hayo yalilipa ambapo katika dakika ya 43 ya mchezo Winga wa Kulia hatari Frank Obadia, “Aziz Ki” alifanikiwa kuukwamisha mpira wavuni na kuiandikia timu yake bao la kwanza na la kuongoza baada ya kuwachambua kama karanga mabeki wa timu pinzani.

Kupachikwa kwa bao hilo kuliwafanya Timu ya Tume kupoteana, hivyo kuchochea mashambulizi na hamasa kubwa kwa wachezaji kutoka Timu ya Mahakama ambao walikuwa wanafika katika lango la wapinzani wao mara kwa mara na kosa kosa za hapa na pale kutokana na kukosekana kwa utulivu.

Hata hivyo, ilipofika katika dakika ya 56, mwamba yule yule (Frank Obadia) aliwanyanyua mashabiki wa Mahakama Sports baada ya kufunga bao la pili kutokana na pasi mpenyezo iliyotoka kwa mshambuliaji hatari wa kati Beatus Semwanza na kuifanya timu yake kuongoza kwa mabao mawili.

Bao hilo lilifuatiwa na mashambulizi kadhaa kutoka timu zote mbili na ilibakia kidogo tu katika dakika za lala salama kwa Mchezaji namba 10 wa Mahakama Sports Martin Mpanduzi kuipatia timu yake bao la tatu baada ya kushindwa kuukwamisha mpira nyavuni akiwa yeye na kipa wa Timu ya Tume. Hadi mchezo una malizika, Mahakama Sports 2 na Timu ya Tume ya Utumishi 0.

Akizungumza baada ya mechi hiyo ya kusisimua, Mwalimu wa Mahakama Sports Spear Mbwembwe amewapongeza vijana wake kwa kujituma na kufanikiwa kupata ushindi huo. Amesema wataendelea kutoa dozi takatifu hata kwa timu zingine kwa vile wamedhamiria kuchukua kombe katika mashindano hayo.

“Nawapongeza sana vijana wangu, wamefanya vizuri. Ila bado sijaridhika na ushindi huu. Pamoja na kupata ushindi, sisi tunataka magori zaidi. Kwa vile leo ndiyo tumeanza nategemea mabao mengi zaidi kwenye mechi zijazo. Vijana wangu wote wapo vizuri sana, ila kwa leo nadhani walikuwa na hofu ya mchezo ndiyo maana hawa jamaa (Timu ya Utumishi) wamesalimika,” alisema.

Naye Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amesema mapambano bado yanaendelea. “Hatujamaliza kaka, ndiyo kwaaanza tunaanza. Wapinzani wetu wasifikiri hii ni nguvu ya soda. Tutawashangaza wengi mwaka huu. Tumekuja kuzoa kila kitu kwenye mashindano haya,” alisema.

Katika mchezo wa leo, Mahakama Sports iliwakilishwa na Fahamu Kibona; Iman Patson; Gisbert Chentro; Akida Mzee; Emmanuel Mwamole; Selemani Magawa; Frank Obadia; Gabriel Tabana; Martin Mpanduzi; Mwinjuma Bwanga na Shamte Seif. Wachezaji wa akiba walikuwa Hassan Aufi; Nassoro Mwampamba; Kelvin Rutalemwa; Shabiru Hood na Beatus Simwanza.

Mbali na Mwenyekiti, viongozi wengine ambao wameambatana na Timu ni Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile.

Mashindano ya SHIMIWI ambayo yalianza jana tarehe 1 Octoba, 2022 yanatarajiwa kufunguliwa rasmi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassimu Majaliwa tarehe 5 Octoba, 2022. Kauli mbiu ya mashindano ya SHIMIWI 2022 ni “Michezo hupunguza magonjwa yasiyo ambukiza na kuongeza tija mahala pa kazi.”

Mashindano hayo ambayo yanashirikisha michezo mbalimbali yatafanyika katika viwanja tofauti tofauti nane ambavyo ni Viwanja vya Mkwakwani, Shule ya Sekondari Popatlal, Galanos Sekondari, Bandari, Shule ya Tanga, Polisi Chumbageni na Viwanja vya Gymkhana.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu Wanaume ikiwa katika picha ya pamoja kabla ya mchezo.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu Wanaume pamoja na mashabiki (juu na chini) wakiwa katika picha ya pamoja baada ya ushindi

Mashabiki wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu Wanaume wakishangilia ushindi baada ya mpira kumalizika ambapo Timu ya Mahakama iliibuka mshindi kwa mabao 2:0 dhidi ya Tume ya Utumishi.
Katibu Mkuu wa Mahakama Mahakama Sports Robert Tende ( mwenye mpira) na Naibu Katibu Mkuu Theodosia Mwangoka (kushoto) wakishangilia kwa furaha pamoja na sehemu ya wachezaji baada ya ushindi huo.
Wachezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu Wanaume walikisakama lango la wapinzani wao.
Gorikipa wa Timu ya Tume ya Utumishi akilamba nyasi baada ya 'kutobolewa' na Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports).
Gorikipa wa Timu ya Tume ya Utumishi akilamba nyasi  kwa mara ya pili.
Wachezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu Wanaume wakipongezana baada ya kupachika bao la pili.
Wachezaji wa Timu ya Tume ya Utumishi wakiokoa moja ya hatari kwenye lango lao. 
Mwalimu wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Miguu Wanaume Spear Mbwembe akizungumza na wachezaji wake wakati wa mapumziko.

Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede (kushoto) akijadiliana jambo na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa Shaibu Kanyochole wakati wa mchezo huo.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni