Jumapili, 2 Oktoba 2022

MAHAKAMA SPORTS YAANZA MAMBO YAKE SHIMIWI TANGA

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume na Wanawake leo tarehe 2 Octoba, 2022 imeanza vizuri kwenye mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa baada ya kuwaadhibu vikali wapinzani wao, Timu za Haki na RAS Singida.

Ilikuwa Kamba Wanaume katika mchezo wa makundi ulioanza ambapo Timu ya Haki iliingia hofu na kusita kwa dakika kadhaa kuingia uwanjani mara baada ya kuwaona wababe hao wa Mahakama pamoja na kuitwa na wasimamizi wa mchezo huo mara kwa mara.

Haikumchukuwa Njiwa kumeza punje ya mtama pale mchezo ulipoanza ambapo Mahakama walitumia dakika sifuri kuwagaragaza Haki. Kadhalika, kazi ilikuwa nyepesi katika kipindi cha pili baada ya Timu ya Haki kuchekechwa vilivyo, hivyo kushindwa kabisa kufurukuta na kupoteza pointi zote tatu kwenye mchazo huo.

Baada ya mchezo huo wa upande wa wanaume kumalizika, mchezo wa Kamba Wanawake wa makundi ulianza kwa Mahakama Sports kukabiliana na RAS Singida. Katika hatua ya mwanzo, RAS Singida walinyofolewa kirahisi licha ya kuingia kwenye uwanjani huku wakihamasishana.

Mahakama Sports ilikuwa haijamaliza kwani katika hatua ya pili wapinzani hao wa watoa haki walijikuta wakilamba nyasi za uwanja baada ya kupokea ‘kamba mchomoko’ na hivyo kuachia pointi zote tatu katika mchezo huo wa awali wa makundi.

Akiongea baada ya kumalizika kwa mchezo huo, Katibu Mkuu wa Mahakama Sports Robert Tende amesema ushindi ambao Timu yake imeupata ni salamu tosha kwa wapinzani wao kwa vile wamejipanga kutoa haki sawa ambayo inaambatana na dozi takatifu kwa kila timu watakayokumbana nayo.

“Hapa bado hatujamaliza, ndiyo tunaanza. Nawaomba wenzetu wawe wavumilivu, wameamua kuingia kwenye mashindano haya wao wenyewe na hawajalazimishwa na mtu. Hivyo, watulie ili sindano iingie vizuri na wapate dozi kamili. Tulishasema tunatoa dozi ya kutwa mara tatu, wajifunze kilichotokea leo kama walikuwa hawajaelewa tulichokuwa tunamaanisha,” alisema.

Katika mchezo wa leo, Kamba wanaume iliwakilishwa na Leonard Kazimzuri, Yuda Mgalla, Patrick Mundwe, Denis Kipeta, Joseph Chokela, Mjuni Denis, Komba Mussa, Mochiwa Marko, Abdul Mumini na Mushi Martin. Wachezaji wa akiba walikuwa Magesa Phabian, Emmanuel Datsan, Robert Uguda, Rajab Mwaliko na Exavery Kasembe.

Kwa upande wa Kamba Wanawake wachezaji walikuwa Beatrice Dibogo, Judith Mwakyalagwe, Merino Mwinuka, Dotto Mlandula, Rebecca Mwakabuba, Salma Mwamende, Safina Mkumbo, Maria Mayala, Zawadi Amir, Namweta Mcharo. Wachezaji wa akiba walikuwa Valeria Ntyangili, Anne Hebron, Lucy Mbwaga na Rose Mwalongo.

Matokeo ya michezo mingine iliyochezwa kwenye kundi A kwenye Kamba wanaume ilikuwa RAS Dodoma ambayo haikufua dafu kwa Timu ya Ikulu, huku Kamba Wanawake ikishirikisha Timu ya Maji ambayo ilipata pointi moja dhidi ya Viwanda baada ya kutoshana nguvu kwenye hatua ya kwanza.

Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile.

Mashindano ya SHIMIWI ambayo yalianza jana tarehe 1 Octoba, 2022 yanatarajiwa kufunguliwa rasmi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassimu Majaliwa tarehe 5 Octoba, 2022. Kauli mbiu ya mashindano ya SHIMIWI 2022 ni “Michezo hupunguza magonjwa yasiyo ambukiza na kuongeza tija mahala pa kazi.”

Mashindano hayo ambayo yanashirikisha michezo mbalimbali yatafanyika katika viwanja tofauti tofauti nane ambavyo ni Viwanja vya Mkwakwani, Shule ya Sekondari Popatlal, Galanos Sekondari, Bandari, Shule ya Tanga, Polisi Chumbageni na Viwanja vya Gymkhana.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume kabla ya mchezo.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake kabla ya mchezo.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume ikijiandaa kumkamua mtu.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake (juu) ikiwashikisha adabu Timu ya RAS Singida (chini).

Mwamuzi wa mchezo akizitayarisha timu uwanjani kuanza mchezo.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume (juu) ikitoa dozi takatifu kwa Timu ya Haki (chini). Ukisikia dozi ya kutwa mara tatu ndiyo hii sasa!!!

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) ikishangilia baada ya kujizolea pointi zote kwenye mchezo wa kamba.

Raha iliyoje baada ya bendera ya Mahakama kupepea.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni