Jumatatu, 7 Novemba 2022

JAJI MDEMU ATAKA UHAI CHAMA CHA MAJAJI NA MAHAKIMU DODOMA

Na Stanslaus Makendi- Mahakama, Dodoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, ambaye ni Mlezi wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (JMAT) Tawi la Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu amehimiza umoja, ushirikiano na uwajibikaji katika chama hicho ili kuongeza tija wanapotekeleza majukumu yao.

Mhe. Mdemu alitoa rai hiyo hivi karibuni katika mkutano wa JMAT Tawi la Dodoma uliofanyika katika Hifadhi ya Taifa ya Ruaha. Akiongea katika mkutano huo, Jaji Mfawidhi huyo aliwahimiza wajumbe wa chama hicho ambao walikuwa katika hifadhi hiyo kwa ajili ya kufanya utalii wa ndani kuwa na utaratibu wa kutembeleana na kubadilishana uzoefu ndani ya Mkoa, nje na ndani ya Kanda hiyo ili kuboresha mahusiano miongoni mwao.

Kadhalika, Jaji Mfawidhi huyo aliwahimiza Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya ndani ya Mkoa wa Dodoma kuhamasisha na kuhakikisha uhai wa chama unaendelea kuwepo na kuendelea kuimarika chama hicho katika maeneo yao kwani wao ndio walezi katika ngazi hizo, huku akisisitiza zaidi wanachama hao kutoa michango yao ya kila mwezi.

Akihitimisha kikao hicho, Mhe. Mdemu aliwasisitiza wajumbe wa JMAT Tawi la Dodoma kukumbuka na kuwajibika kujaza fomu za maadili, zoezi ambalo ni endelevu kwa mujibu wa Sheria na linapaswa kutekelezwa kabla ya tarehe 31 Disemba kila Mwaka. Aliwaomba Majaji na Mahakimu kujenga desturi ya kutembelea Magereza na kushiriki kutatua changamoto zinazobainika ili kuondokana na kero na malalamiko yanayoelekezwa mahakamani.

Majaji na Mahakimu waliotembelea hifadhi hiyo walipata fursa ya kujionea vivutio mbalimbali vya utalii na kupata mafunzo yanayohusu uhifadhi, historia ya Hifadhi ya Ruaha, namna inavyoendeshwa, changamoto zinazoikabili na mipango ya kuiboresha zaidi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma na Mlezi wa JMAT Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu (aliyesimama juu na chini) akisisitiza jambo alipokuwa anaongea na wajumbe wa chama hicho katika Hifadhi ya Ruaha hivi karibuni.

Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi, Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Ruaha, Bw. Godwell Ole Meing’ataki (aliyesimama) akitoa mafunzo kwa wajumbe wa JMAT Tawi la Dodoma (hawapo pichani) kuhusu masuala mbalimbali.
Miongoni wa wanyama wanaoonekana kwa urahisi katika Hifadhi ya Ruaha (picha juu na chini).

Picha ya wajumbe wa JMAT Tawi la Dodoma wakipumzika katikati ya ziara yao ya utalii wa ndani katika Hifadhi ya Ruaha.


 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni